Alhamisi, 1 Oktoba 2015

MAMLAKA YA ELIMU TANZANIA YATOA MKOPO WA SHILINGI BILIONI 3 KWA TAASISI YA ELIMU TANZANIA


 Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) imeingia makubaliano na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) ya Mkopo wa Shilingi Bilioni tatu. Mkopo huu umetolewa na TEA ili kuiwezesha Taasisi ya Elimu Tanzania Kufanya utafiti wa kubaini mahitaji ya maboresho kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali wa elimu, Kuandaa mitaala na  mihtasari ya masomo ya Elimu ya Msingi na Kuandika vitabu vya kiada kwa Darasa la III hadi la VI ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014.

Mkataba huo umetiwa saini tarehe 30 Septemba, 2015 na Joel Laurent Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TEA na Dkt. Leonard Akwilapo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TET na kushuhudiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Prof. Sifuni Mchome ambapo Mkopo  huo ni nafuu unatarajiwa kulipwa katika kipindi cha  miaka 6.
Matokeo tarajiwa kutokana na Mkopo huo ni Pamoja na uwepo wa Mitaala inayoendana na wakati na inayokidhi mahitaji ya sekta na shirikishi, uwepo wa mihutasari ya masomo itakayosambazwa katika kila shule kama ilivyoainishwa katika mitaala na uwepo wa vitabu vya kiada kulingana na mtaala ili kuepusha kuwa na vitabu vinavyotofautiana.


Aidha, ufadhili huu unalenga kuiongezea Taasisi ya Elimu Tanzania kutekeleza majukumu yake kwa njia yenye tija na kuongeza mapato ya Taasisi na utakuwa ni chachu ya kuboresha mfumo wa upatikanji wa vitabu sahihi kulingana na mitaala nchi nzima kupitia TIE.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni