Jumanne, 16 Agosti 2016

Wizara za Elimu Zanzibar na Tanzania Bara kuendeleza Ushirikiano

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia  Mhe.Prof. Joyce Ndalichako mwishoni mwa wiki amekutana na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Riziki Pembe Juma  ambapo walizungumzia masuala mbalimbali yahusuyo Sekta ya Elimu ikiwemo kuendeleza  ushirikiano wa masuala ya Elimu ambao umekuwepo tangu awali.

Mhe. Riziki alisema anatamani kuona walimu kutoka Zanzibar wanapata nafasi ya kukutana na walimu wenzao kutoka bara ili waweze kubadilishana na kupeana uzoefu wa  mbinu mbalimbali za ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi ili kuweza kuboresha elimu itolewayo.

 ‘Kuna maeneo tofautitofauti katika kufundisha yanahitaji kutumia mbinu mbalimbali ili wanafunzi wetu waweze kuelewa, si vibaya walimu hawa wakakutana na kubadilisha uzoefu wa namna ya kufundisha katika maeneo hayo’ alisema Mhe. Riziki

Akizungumza katika kikao hicho cha kuimarisha mahusiano, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Ndalichako alisema ni vizuri kuendeleza misingi ya Ushirikiano katika masuala ya elimu ili kudumisha Muungano wetu. Alisema Wizara ya elimu ni kubwa na inafanya kazi kwa kushirikiana na taasisi zake ambazo zina mamlaka kisheria ikiwa ni pamoja na kutoa miongozo kulingana na maeneo wanayoyasimamia.

Ili kwenda sambamba na kudumisha ushirikiano uliopo baina ya Tanzania Bara na Zanzibar  Waziri Ndalichako alizitaka taasisi  za elimu zinazoshughulika na Masuala ya Muungano kutoa taarifa kwa wakati ili kutochelewesha utekelezaji wa masuala ya elimu kwa upande wa Zanzibar na kuleta changamoto zisizokuwa za lazima hapo baadae.

Aidha Katika kuendeleza ushirikiano kwa upande wa walimu kupeana uzoefu, Prof Ndalichako aliliagiza Baraza la Mitihani la Tanzania kwa kuanzia lipitie script za matokeo ya kidato cha sita kwa upande wa Zanzibar  ili kuona maeneo ambayo wanafunzi wameshindwa zaidi ili kuweza kundaa utaratibu wa kuwakutanisha walimu wanaofundisha masomo hayo waweze kupeana uzoefu kwa lengo la kuboresha.


Naye Naibu Waziri wa elimu Mhe. Mhandisi . Stellah Manyanya alisema ni vizuri Wizara ikaratibu utaratibu wa watendaji wa masuala ya kielimu kutoka Bara kukutana na wale wa Zanzibar ili kuzungumzia mambo mbalimbali yanayoleta chanagamoto katika utekelezaji wa masuala ya kielimu kwa lengo la kuboresha.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni