Alhamisi, 30 Novemba 2017

Chuo Kikuu Huria chatakiwa kupanua wigo wa udahili.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kassim Majaliwa amekitaka Chuo kikuu Hiria nchini kuhakikisha kinaongeza ubora wa utoaji Elimu na kupanua wigo wa udahili kwa wanafunzi wa chuo hicho.

Waziri Mkuu Majaliwa ametoa kauli hiyo wakati wa mahafali ya 33 ya Chuo hicho ambayo yamefanyikia mkoani Singida na kusisitiza kuwa Umuhimu wa Chuo kikuu huria uko bayana katika kuhakikisha malengo ya serikali ya kutekeleza sera ya uchumi wa viwanda inafikiwa kupitia wataalamu wanaomaliza chuoni hapo.

Waziri Majaliwa amesema Serikali ya awamu ya Tano inatambua na inaunga mkono juhudi zinazofanywa na uongozi wa chuo hicho huku wakisisitizwa kuzingatia vigezo, taratibu za utoaji wa Elimu iliyo bora ili wapatikane wataalamu ambao ni bora kwa maslahi ya Taifa.
Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema Serikali inatambua mchango wa Chuo hicho katika kipindi cha miaka 25 ambapo kimekuwa kikitoa  Elimu katika masafa ya mbali hali ambayo inahitaji mwanafunzi kuwa na nidhamu ya hali ya juu ili kifikia malengo.

Kutokana na juhudi hizo Waziri Ndalichako ameahidi Serikali itaendelea Kuimarisha miundombinu ya Tehama ili Elimu hiyo ya masafa iweze kuwafikia watu wengi zaidi.
Waziri Ndalichako amewataka wahitimu kutumia vyema ujuzi na kuhakikisha wanaimarisha utendaji kazi katika serikali na hata Sekta binafsi.

Pia amewataka wahitimu kujenga nadhani pamoja na kuwa na ari katika  uwajibikaji ikiwa ni pamoja na kuwa mabalozi katika Shughuli ambazo watakuwa wanazifanya.






Jumatatu, 27 Novemba 2017

Waziri Ndalichako: Watendaji wajibikeni acheni kulipana stahili ambazo hazifuati miongozo na nyaraka za Serikali

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amezitaka Taasisi zilizochini ya Wizara yake kuwajibika katika nafasi zao za uongozi na siyo kusubiria mpaka kiongozi wa juu aibue changamoto zinazojitokeza katika maeneo yao.

Waziri Ndalichako amesema hayo leo mkoani Morogoro wakati wa Kikao kazi kilichohusisha  Menejimenti ya Wizara na Taasisi zake cha kujadili na kujengeana uwezo kuhusu namna  bora ya kubaini na  kukabiliana na viashiria hatarishi katika maeneo ya kazi.(Risk Identification and Risk Managment).
Waziri Ndalichako amesema kupitia kikao kazi hicho watendaji wataweza kujifunza na kubaini mapema viashiria ambavyo vitaonekana kukwamisha utekelezaji wa mipango ya wizara.
"lengo  hapa ni kuzuia madhara badala ya kusubiri madhara yatokee, hivyo kupitia kikao kazi hiki watendaji watajifunza kwa lengo la kuzuia na kutekeleza malengo ya Wizara kama yalivyokusudiwa,"amesema Waziri Ndalichako
Waziri Ndalichako pia amezitaka Taasisi na Watendaji wa Wizara hiyo kuanzia leo kuacha mara moja kulipana stahili ambazo hazifuati miongozo na nyaraka za serikali.
Profesa Ndalichako ametaja baadhi ya stahili ambazo zimekuwa zikilipwa bila kufuata taratibu na miongozo hiyo kuwa ni pamoja na posho za kujikimu, Nyumba,  umeme na simu.
Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu ,  Sayansi na Teknolojia Dkt.  Leonard Akwilapo amesema mkutano huo umelenga kuondoa viashiria hatarishi ambavyo vimekuwa vikikwamisha ufanisi katika utendaji kazi wa wizara na kuwataka washiriki wa mkutano huo kuandaa mpango mkakati wa kuweza kutambua mapema viashiria hatarishi na kuvifanyia kazi ili kufikia malengo  ya wizara.
Kikao kazi hicho ambacho kimeanza leo kitahusisha pia  Wakurugenzi wasaidizi, waratibu wa miradi na wasaidizi wa miradi, wathibiti ubora wa shule kanda, wakuu wa vyuo vya Elimu ya Ualimu, na watumishi kutoka kila Idara wa wizara hiyo.



Rais Magufuli azindua hospitali ya Mloganzila

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amezindua rasmi hospitali ya Taaluma na Tiba ya chuo kikuu cha afya na sayansi shirikishi MAMC, kilichopo wilaya ya Ubungo mkoani pwani ambapo amewataka Wakala wa Majengo ya Serikali (TBA) kuhakikisha wanakamilisha mara moja ujenzi wa mabweni, madarasa na kumbi za mihadhara katika Chuo hicho.

Rais Magufuli ametoa rai hiyo wakati wa uzinduzi wa hospitali hiyo ambapo amesema  tayari serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 13 kwa ajili ya ujenzi huo na kuwa Kati ya fedha hizo tayari  kiasi cha shilingi bilioni Nne kimelipwa kwa TBA  ili kuanza ujenzi huo na kwamba ujenzi utakapokamilika utawezesha udahili wa wanafunzi 15,000 wa afya na tiba kwa mara moja tofauti na ilivyokuwa awali wanafunzi 4500 Pekee ndiyo walioweza kudahiliwa. 

Rais Magufuli pia ameitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknojia na wizara ya Afya kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha hospital hiyo inatekeleza majukumu yake kwa weledi ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Wakati wa uzinduzi huo Rais Magufuli amesifu na kupongeza jitihada zilizofanywa na Serikali ya awamu ya Nne chini ya uongozi wake Rais mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete za kuhakikisha eneo la ujenzi linapatikana na ujenzi unafanyika na hatimaye wananchi kupata huduma za afya.

Naye Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia profesa Joyce Ndalichako amesema uwepo wa Chuo hicho chenye mitambo na vifaa vya kisasa kutalisaidia Taifa kupata wataalamu wenye uwezo ambao itsaidia kuondoa changamoto ya uhaba wa wataalnu wa afya hapa nchini.


Ijumaa, 24 Novemba 2017

Dkt. Akwilapo awataka wahitimu wa ADEM kusimamia kanuni na taratibu katika utendaji kazi.

 Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leornard Akwilapo amewataka wahitimu wa kozi za Uongozi na Usimamizi wa Elimu zinazotolewa na Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) kuhakikisha wanasimamia utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka(2014), Sheria, Kanuni na Taratibu za Elimu ili kupunguza migogoro shuleni

Katibu Mkuu ameyasema hayo katika mahafali ya Ishirini na tano (25) yaliyofanyika katika Chuo hicho kilichopo Bagamoyo Mkoani Pwani ambapo amewataka ADEM  kuendelea kusimamia utekelezaji wa Mtaala kwa ufanisi, kutoa takwimu sahihi za shule, kupanga mipango ya maendeleo ya shule inayotekelezeka, kusimamia fedha za elimu bila malipo kwa ufanisi.

Eneo lingine ambalo Katibu Mkuu ametaka litiliwe mkazo ni    pamoja na kudhibiti nidhamu za wanafunzi mara warudipo katika vituo vyao vya kazi.

Dkt. Akwilapo amesema mafunzo ya uongozi na usimamizi wa Elimu pamoja na Ukaguzi wa Shule ni muhimu katika kuwapa uwezo walimu na viongozi wa elimu kufanya kazi zao kwa weledi, ufanisi na kwa kujiamini zaidi hususani katika kipindi hiki cha maendeleo makubwa ya sayansi na teknolojia.

Amewataka wahitimu kuwa chachu ya mabadiliko katika Uongozi na Utawala Bora pamoja na  Uthibiti Ubora wa Shule nchini kwa kutumia ujuzi, maarifa, stadi na mbinu mpya walizozipata katika mafunzo ikiwa ni pamoja na   maarifa waliyoyapata kuyaeneza kwa walimu ambao hawajapata fursa ya kupata mafunzo hayo.





Chuo Kikuu Ardhi chaadhimisha miaka 10

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Majaliwa kassim Majaliwa amekitaka Chuo Kikuu cha Ardhi nchini kuendelea kutekeleza mpango mkakati waliojiwekea ili kufikia malengo yanayo kusudiwa na Taifa.

Waziri Mkuu  Majaliwa ameyasema hayo wakati wa maadhimisho ya miaka 10 ya chuo hicho ambapo amekitaka , Chuo hicho kuwa na kamapuni itakayosimamia ujenzi katika maeneo mbalimbali hapa nchini na siyo jina la Chuo kutumika vibaya na kuratibu sifa ya Chuo.
Waziri Majaliwa amesema  Chuo hicho kimekuwa kikiisaidia serikali kujenga majengo yenye viwango kwa garama nafuu, hivyo amezitaka taasisi za serikali kukitumia Chuo hicho katika ujenzi wa majengo mbalimbali.

 Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema Chuo kikuu cha Ardhi kimekuwa kikifanya vizuri katika ujenzi, usanifu wa majengo na kwa kutambua kazi ya Chuo hicho  tayari Wizara imetoa zaidi ya bilioni 2 kwa ajili ya ujenzi wa vyuo vya Ualimu, na shule.
Baada ya kukamilika kwa mkutano huo, Waziri Ndalichako alikutana na wanafunzi wa Chuo hicho kwa ajili ya kusikiliza changamoto mbalimbali ambapo wanafunzi walimweleza Waziri kuwa hadi sasa hawajaingiziwa mikopo yao kwa kile kilichoelezwa kuwa wanafunzi bado hawajafungua Akaunti, na ndiyo Wizara alipohitaji maelezo kutoka kwa Afisa mikopo majibu ambayo waziri hakuridhika nayo na ndiyo alipoomba maelezo.

Hata hivyo kutokana na maelezo ambayo hakuridhika nayo,Waziri aliamua kuondolewa mara moja kwa afisa mikopo katika Chuo hicho.


Jumanne, 21 Novemba 2017

China na Tanzania kuendelea kushirikiana katika Sekta ya Elimu

Jamhuri ya Watu wa China imesema itaendela kuisaidia Tanzania katika sekta ya Elimu kwenye eneo la Elimu ya Juu, utoaji wa mafunzo ya Ufundi pamoja na kusaidia garama za uchapishaji wa vitabu vya masomo ya Sayansi kwa ajili ya shule za  msingi na Sekondari.

Kauli hiyo imetolewa na Balozi wa Jamuhuri ya watu wa China nchini Tanzania Wang Ke wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia  Profesa Joyce Ndalichako katika ofisi ndogo zilizopo jijini Dar es Saalam.

Katika mazungumzo yao Waziri Ndalichako amesema garama za uchapaji wa Vitabu ni kubwa hivyo ni vyema Wizara ikawa na mitambo yake ya kuchapia vitabu ambayo itakuwa endelevu suala ambalo Balozi Wang Ke  amekubaliana nalo na kuitaka Wizara kuandaa maombi ya mashine hiyo ili ubalozi uweze kufanyia kazi.


Jumatatu, 20 Novemba 2017

Waziri Ndalichako: Ili shule isajiliwe lazima ikidhi vigezo

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema ili shule isajiliwe lazima iwe imekidhi vigezo ikiwa ni pamoja na kuwa na madarasa ya kutosha, nyumba za walimu, ofisi za walimu, matundu ya vyoo, pamoja na maabara endapo shule itakuwa ni ya Sekondari.

Waziri Ndalichako ameyasema hayo wakati akizungumza na wananchi wa halmashauri ya Mbulu iliyopo mkoani Manyara ambapo amesema ni kweli serikali inahitaji ziwepo shule nyingi ambazo zinavigezo, siyo kuwa na shule ambazo hazina vigezo.

"Shule za nyasi katika Serikali hii ya awamu ya tano zitabaki kuwa historia kwa kuwa serikali inajenga na kuboresha miundombinu ya kujifunzia na ile ya kufundishia, sasa ili shule isajiliwe lazima iwe imekidhi vigezo siyo bora shule bali tunahitaji shule zilizobora na zenye viwango vinavyokubalika" amesema Waziri Ndalichako.

Waziri Ndalichako amesema   kazi ya usajili ni nyepesi sana ambayo haichukui muda mrefu endapo vigezo vinakuwa vimetimia,  lakini kazi kubwa ni kuhakikisha miundombinu bora inayokubalika inakuwepo ili shule iweze kusajiliwa.

 Hivyo amewasihi wadau wote wa Elimu kuhakikisha shule zinapojengwa zinazingatia na kukidhi  vigezo kabla ya kusajiliwa.



Alhamisi, 16 Novemba 2017

Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii yakagua Shule ya Ihumwa

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya huduma za maendeleo ya jamii imepongeza juhudi zinazofanywa na Wizara ya Elimu, Sanyasi na Teknolojia kwa kushirikiana na OR TAMISEMI katika kuboresha miundombinu ya shule, ikiwa ni pamoja na kusimamia fedha zinazotengwa kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu hiyo.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Peter Serukamba wakati kamati hiyo ilipotembelea na kukagua ujenzi wa vyumba vya madarasa 9, matundu ya vyoo na jengo la Utawala katika shule ya msingi Ihumwa ujenzi ambao umetekelezwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia programu ya Lipa kulingana na Matokeo, yaani P4R.
Ziara hiyo imejionea madarasa mapya 9, ukarabati wa vyumba vya madarasa 11, Jengo la utawala na ujenzi wa vyoo ambavyo vyoye vimegharimu milioni 168.

Mwenyekiti wa kamati hiyo pia amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu kutoa fedha kwa ajili ya kuchimba kisima katika shule ili kuondoa adha ya upatikanaji wa maji katika shule hiyo.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia amemhakikishia Mwenyekiti wa kamati hiyo kuwa Wizara imepokea maelekezo na kuahidi kuyafanyia kazi.



Ijumaa, 10 Novemba 2017


Kauli ya Serikali kuhusu udahili na utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu mwaka 2017/18 iliyotolewa na Prof.  Joyce Ndalichako (MB) - Bungeni, Dodoma; Novemba 09, 201

#Udahili wa wanafunzi walioomba kujiunga na vyuo vya elimu ya juu ulifanyika kwa awamu tatu na ulihusisha jumla ya vyuo na taasisi za elimu ya juu 67.
#Katika awamu ya kwanza majina 77,756 yakipokelewa TCU, wanafunzi 44,627 walichaguliwa.

#Baada ya uhakiki waombaji 36,831 waliidhinishwa na kujiunga na shahada ya kwanza. Waombaji 7,796 walikuwa na kasoro mbalimbali kwenye taarifa zao hivyo kukosa sifa ya kujiunga na vyuo.

#Awamu ya pili ililenga waombaji waliokosa udahili awamu ya kwanza ambapo jumla ya waombaji 19,488 walijitokeza na walioidhinishwa kuwa na sifa za kujiunga ni 9,525.
#Awamu ya tatu ilikuwa kwa ajili ya kutoa nafasi ya mwisho kwa wanafunzi waliokosa vyuo ambapo jumla ya waombaji 7,418 waliidhinishwa kujiunga na vyuo.

Hadi kukamilika kwa awamu ya  tatu waombaji 63,737  waliidhinishwa kujiunga na vyuo  na  waombaji 28,466 kati yao walikuwa wamechaguliwa zaidi ya chuo kimoja.

#Serikali katika mwaka wa fedha 2017/18 imepanga kutumia Shilingi Bilioni 427.54 kugharamia mikopo kwa ajili ya wanafunzi wenye uhitaji na waliodahiliwa na vyuo vya elimu juu hapa nchini.

#Mikopo hii ni kwa ajili ya wanafunzi 122,623 ambapo wanafunzi 30,000 ni wa mwaka wa kwanza na wanafunzi 92,623 ni wanaoendelea na masoma.

#Katika robo ya kwanza ya mwaka huu wa masomo, Wizara imepokea Shilingi Bilioni 147.06 kwa ajili ya ada za wanafunzi na kwa ajili ya kugharamia chakula, malazi, vitabu, viandikia na mahitaji maalum ya masomo.

#Utoaji wa mikopo umezingatia vigezo vilivyowekwa ambavyo ni ulemavu, uyatima na uhitaji hasa katika programu za kipaumbele.

*Changamoto Zilizojitokeza Katika Utoaji wa Mikopo. 
                           
#Baadhi ya waombaji kutozingatia mwongozo na maelekezo ya uombaji kwa kutoambatanisha nyaraka muhimu zinazothibisha uhitaji wao.

#Baadhi ya wanafunzi waliopangiwa mikopo kuamua kuripoti kwenye vyuo tofauti walivyothibitisha udahili wa awali ambapo mikopo yao  imelipwa kwenye vyuo tofauti na waliporipoti.

#Dhana ya mikopo ni ya elimu ya juu ni kwa ajili ya wanafunzi wote na hivyo hata wanafunzi wasio na sifa kulingana na vigezo kutaka wapate mikopo.

*Hatua Zilizochukuliwa Kukabiliana na Changamoto Zilizojitokeza. 

#Kupokea taarifa na nyaraka za ziada na kusahihisha taarifa za maombi kutoka kwa wahitaji walioshindwa kukamilisha taarifa husika wakati wa kipindi cha maombi.

#Kukamilisha utaratibu wa kufungua dirisha la rufaa ili baadhi ya wanafunzi watakaokuwa hawajapangiwa mikopi kufikia tarehe 10/11/2017 waweze kuwasilisha rufaa zao ili wale watakaofanikiwa kwenye rufaa wapangiwe mikopo kabla ya tarehe 30/11/2017.

#Kupokea taarifa za usajili za wanafunzi wenye mikopo ili wale ambao mikopo iko vyuo tofauti ihamishwe kwenye vyuo walivyoripoti.

#Serikali imeshawaagiza wakuu wote wa vyuo vya Elimu ya Juu kuacha urasimu katika utoaji wa fedha kwa wanufaika wa mikopo.

#Inasikitisha sana kuona kuwa baadhi ya vyuo vinadiriki hata kuwakataa wanafunzi waliowadahili wao wenyewe.

#Nampongeza Rais Dkt. Magufuli kwani haijawahi kutokea, fedha kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu zikatolewa mwezi mzima kabla ya vyuo kufunguliwa 

Jumatano, 8 Novemba 2017

Katibu Mkuu ataka fedha za tafiti zitumike kama zilivyopangwa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt Leornard Akwilapo amesema Serikali itahakikisha fedha zilizotolewa  na Serikali ya Sweden kupitia Shirika la Kimataifa la misaada la nchi hiyo (SIDA) zinatumika kama zilivyokusudiwa kwa ajili ya masuala ya tafiti na kuhakikisha matokeo tarajiwa yanapatikana kikamilifu.

Dkt. Akwilapo ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa maadhimisho ya miaka 40 ya ushirikiano katika tafiti kati ya Tanzania na Sweden yanayofanyika jijini Dar es Salaam ambapo nchi ya Sweden imetoa zaidi ya bilioni 78 kwa ajili ya kuendeleza masuala ya tafiti kwa kipindi cha 2015 hadi 2020.

Dkt Akwilapo amezitaja taasisi zilizonufaika na zinazoendelea kunufaika na ushirikiano huo kuwa ni Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Chuo Kikuu Ardhi (ARU), Chuo Kikuu cha tiba na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambao wamekuwa wakifanya tafiti katika masuala mbalimbali ya kitaaluma na kijamii. 


Ushirikiano kati ya Tanzania na Sweden umewezesha Tanzania kupata wataalam 455 katika ngazi ya uzamili na 82 katika ngazi ya uzamivu kwa mwaka 1998 hadi 2009 na mpaka sasa zaidi ya wanafunzi 200 wanaendelea na masomo ya katika ngazi uzamili na wengine 80 katika ngazi uzamivu kutokana na ushirikiano Kati ya nchi hizo mbili.




Jumanne, 7 Novemba 2017

Naibu Katibu Mkuu Dkt. Semakafu asisitiza umuhimu wa kuboresha Sera na Programu za watot

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Avemaria Semakafu amesema zaidi ya watoto milioni mia mbili duniani hawafikii malengo kutokana na umasikini  na utapiamlo wanaoupata wakiwa katika umri mdogo.

 Dkt. Semakafu ameyasema hayo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa pili wa kimataifa wa kujadili maendeleo ya makuzi ya watoto na kusisitiza kuwa kupitia mkutano huo wadau wataweza kuboresha sera na kuwa na programu ambazo zitasaidia katika makuuzi ya watoto wa kitanzania.

Kupitia mkutano huo wadau watapata fursa ya kuwa na uelewa wa pamoja, kushirikisha uzoefu kati ya nchi moja na nyingine pamoja na kushawishi wadau kuweka nguvu ya pamoja kwa ajili ya watoto.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Chuo Kikuu Cha Aghakan Tanzania na Taasisi ya IHD Profesa. Kofi Marfo amesema kuwa maendeleo na makuzi ya watoto hutegemea  wazazi, familia na  jamii  kwa ujumla amesisitiza pia suala la  lishe bora kwa watoto, kukua na kuandaa vituo vya afya na hospitali kwa ajili ya upatikanaji wa huduma zilizo bora.

Mkutano huo wa siku tatu umeanza leo na umehusisha nchi ishirini na tano ambapo Tanzania mwenyeji wa Mkutano huo.





Jumatatu, 6 Novemba 2017

Makamu wa Rais afungua Kongamano la Elimu, Waziri wa Elimu ashiriki

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema kuwa Elimu ya Ufundi ndiyo nguzo muhimu ya kufikia ajenda ya serikali ya kuwa Tanzania ya viwanda na kufikia uchumi wa kati ifikapo 2025.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati akifungua kongamano la kimataifa la wadau wa Elimu ya Ufundi na mafunzo jijini Dar es salaam, na kusisitiza kuwa dira ya Maendeleo ya 2025 imeipa Elimu kipaumbele cha juu kwa kuwa ndiyo kitovu katika kuleta mabadiliko ya kiuchumi katika jamii.

Makamu wa Rais amesema kuwa serikali kipitia baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi litaendelea kusimamia na kuratibu utoaji wa mafunzo katika taasisi za Elimu ya Ufundi ili Taifa liwe na wataalamu wa kutosha na wenye weledi katika fani mbalimbali kwa Maendeleo ya Taifa.

Viongozi wengine walioshiriki mkutano huo wa siku tatu ni pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa. Joyce Ndalichako, Naibu Katibu Mkuu Dkt. Avemaria Semakafu, Wakuu wa Taasisi  na wadau mbalimbali.


Kauli mbiu katika mkutano huo ni Wekeza katika Elimu ya Ufundi na Mafunzo kwa Tanzania kuwa ya uchumi wa viwanda.



Alhamisi, 2 Novemba 2017

Ndalichako: Tanzania imedhamiria kufikia malengo ya maendeleo endeleve

Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania imedhamiria kufikia malengo ya Maendeleo endelevu kwa kuhakikisha inatimiza malengo yaliyowekwa ikiwa ni pamoja na kutoa Elimu bure kuanzia Elimu ya awali mpaka kidato cha Nne, uboreshaji wa miundombinu ya kujifunzia na kufundishia, uboreshaji wa vyuo vya ualimu pamoja na kuboresha mazingira kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu.

Hayo yameelezwa jana na Waziri wa Elimu , Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako wakati akihutubia mkutano mkuu wa 39 wa UNESCO, Mjini Paris nchini Ufaransa, ambapo katika kufikia malengo hayo walimu 68,799 tayari wamepatiwa mafunzo maalumu ya mtaala ulioboreshwa, KKK.

Waziri Ndalichako aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa suala la wanafunzi wenye mahitaji maalumu bado linahitaji kuangaliwa kwa mapana zaidi hivyo kuziomba nchi wanachama kutoa kipaumbele katika kuandaa  mazingira ambayo yatakuwa rafiki kwa wanafunzi wa kike na wale wa kiume ambao wana mahitaji maalumu.

Waziri Ndalichako Pia alieleza kuwa tayari vifaa vya maabara na vitabu kwa shule za Sekondari limesambazwa kwa nchi nzima ili kutilia mkazo masomo ya Sayansi.


Waziri Ndalichako pia tayari ameshiriki mikutano mbalimbali inayohusu tume za UNESCO zilizoanza oktoba 30, 2017 ambapo amepokea taarifa zinazohusu fursa mbalimbali za namna ya kupata misaada ya maendeleo kutoka UNESCO na washirika wake wa kimataifa.

Pia kupitia mkutano huo Mkuu viongozi wa Tume za Taifa za  UNESCO  duniani wanapata fursa ya kukutana na kubadilishana uzoefu na kupeana mbinu mbalimbali za kuandika kazi miradi kwa maslahi ya nchi zao.

Mkutano huo mkuu wa 39 wa UNESCO ulianza Oktoba 30, 2017 ambapo  Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni -UNESCO -IRINA BOKOVA alisema Tume hiyo  imekuwa na mafanikio kutokana na  ushirikiano inaoupata kutoka kwa nchi wanachama.

Katika mkutano huo waziri wa Elimu Profesa Ndalichako ameambatana na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa Balozi Samwel Shelukindo, Mkurugenzi wa Sera na Mipango Petro Lyatuu kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO  Dkt. Moshi Kimizi.

Mkutano huo Mkuu hufanyika kila baada ya miaka miwili na unahusisha nchi zote wanachama za UNESCO.




Jumatano, 1 Novemba 2017

Waziri kuwasilisha msimamo wa Tanzania kwa UNESCO leo


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce   Ndalichako leo anawasilisha taarifa  yenye msimamo wa Serikali ya  Jamuhuri ya muungano wa Tanzania katika mkutano mkuu wa 39 wa shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi, Utamaduni, habari na Mawasiliano -UNESCO.

 Waziri Ndalichako pia tayari ameshiriki mikutano mbalimbali inayohusu tume za UNESCO zilizoanza oktoba 30, 2017 ambapo amepokea taarifa mbalimbali zinazohusu fursa mbalimbali za namna ya kupata misaada ya maendeleo kutoka UNESCO na washirika wake wa kimataifa, pia viongozi wa Tume za Taifa za  UNESCO  duniani kubadilishana uzoefu na kupeana mbinu mbalimbali za kuandika kazi miradi kwa maslahi ya nchi zao.

Mkutano huo mkuu wa 39 wa UNESCO ulianza juzi Oktoba 30, 2017 ambapo  Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni -UNESCO -IRINA BOKOVA alisema Tume hiyo   ina nguvu kwa sababu ya ushirikiano inaoupata kutoka kwa nchi wanachama.

Katika mkutano huo waziri wa Elimu Profesa Ndalichako ameambatana na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa Balozi Samwel Shelukindo, Mkurugenzi wa Sera na Mipango Petro Lyatuu kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO  Dkt. Moshi Kimizi.
Mkutano huo Mkuu hufanyika kila baada ya miaka miwili na unahusisha nchi zote wanachama za UNESCO.