Jumatano, 4 Julai 2018

SERIKALI YAANZA KUKARABATI VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI.


·         PROFESA MDOE ASISITIZA MATUMIZI YA FORCE AKAUNTI

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe amewataka wakuu wa Vyuo vya maendeleo ya Jamii nchini na Maboharia kutumia kikamilifu utaalamu watakaoupata katika mafunzo ya namna ya kutumia Force Account na kuhakikisha wanasimamia kikamilifu shughuli za ujenzi na ukarabati katika vyuo hivyo.

Profesa Mdoe ametoa kauli hiyo Mjini Morogoro wakati akifungua mafunzo ya siku tatu kwa washiriki hao na kusisitiza kuwa   Serikali kwa sasa inakarabati vyuo vya Maendeleo ya Wananchi, hivyo mafunzo watakayoyapata yakawe chachu ya kusimamia kazi hiyo kwa umakini na uadilifu ili thamani ya matumizi ya fedha iweze kuonekana.

“Ni vizuri mkashiriki mafunzo haya kikamilifu kwa kuwa matokeo ya mafunzo haya yataonekana katika utekelezaji wa miradi na kila mtu atawajibika kwa nafasi yake, thamani ya Fedha lazima iende ikaonekana katika utekelezaji wa uboreshaji wa vyuo hivi vya FDCs,” alisisitiza Profesa Mdoe.
Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe akizungumza na wajumbe (hawapo pichani) wakati wa mafunzo ya matumizi ya Force Account Mjini Morogoro. Amewataka wajumbe kutumia utaalamu watakaoupata katika kusimamia ujenzi na ukarabati katika vyuo vyao.

Profesa Mdoe amesema matumizi ya utaratibu wa Force Akaunti ni mzuri kwa kuwa gharama zinazotumika katika ujenzi na ukarabati ni ndogo na hii inatokana na kutumia wataalam na vifaa vya vinavyonunuliwa na kusimamiwa Taasisi husika.

Mradi wa Kukuza Ujuzi na Stadi za Ajira umeanzishwa kwa lengo la kutekeleza vipaumbele vya Serikali vilivyoainishwa katika mkakati wa Serikali wa kufikia Tanzania ya Viwanda ifikapo 2025, lakini pia kuwezesha vijana kupata ujuzi kwa vitendo kuliko nadharia pamoja na kujengea uwezo vyuo vya kati.
Wajumbe wa Kikao wakifuatilia hotuba ya Kaimu Katibu Wizara ya Elimu, Saynsi na Teknolojia Profesa James Mdoe wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya matumizi ya Force Account kwa Wakuu wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi, Maboharia na Wahasibu yaliyofanyika mjini Morogoro.

Mafunzo hayo ya siku tatu yanahusisha Wakuu wa vyuo vya FDCs 11, Wahasibu na maboharia na yanatarajiwa kukamilika kesho kutwa.
Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Saynsi na Teknolojia Profesa James Mdoe akiwa katika picha ya pamoja  na baadhi ya Washiriki wa mafunzo ya namna ya kutumia force Account yaliyofanyika Mjini Morogoro.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni