Ijumaa, 31 Agosti 2018

KATIBU MKUU WIZARA YA ELIMU AWATAKA WAKUU WA VYUO VYA UALIMU KUFUATA TARATIBU KATIKA UTENDAJI


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo amewataka Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali kuacha kufanya kazi kwa mazoea badala yake wafuate taratibu wakati wa kutekeleza majukumu yao ya kikazi ikiwa ni pamoja na kushirikisha watumishi na wanafunzi wa Chuo taarifa za mapato na matumizi ya fedha.

Dk. Akwilapo ameyasema hayo leo Jijini Dodoma wakati alipokutana na Wakuuu wa Vyuo hivyo kwa lengo la kujadili mafanikio, changamoto na mikakati waliyonayo katika kuhakikisha majukumu na uendeshaji wa vyuo yanatekelezeka bila changamoto ili waweze kufikia azma ya kuandaa walimu bora.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo akizungumza na Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali (hawapo pichani) katika kikao kazi cha kujadili mafanikio, changamoto na Mikakati bora ya kuwezesha Vyuo  kutekeleza majukumu yake bila changamoto Mkoani Dodoma. 

Pia Katibu Mkuu huyo amewataka Wakuu wa Vyuo kuwasirikisha wale wanaowasimamia katika kuandaa mikakati ya utendaji ili waweze kutoa mchango katika kutekeleza mikakati hiyo na kufikia malengo mapana ya Wizara ambayo ni kutoa Elimu bora.

Katika hatua nyingine Dk. Akwilapo amewataka Wakuu wa Vyuo hao kuanisha mahitaji ya rasilimali watu ambayo inahitajika vyuoni inayoendana na kozi zinazofundishwa katika Chuo husika ili kuepuka kuwa na rasilimaliwatu isiyoendana na mahitaji ya Chuo. 
Baadhi ya Wakuu wa Vyuo wakifuatilia maelekezo ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo wakati wa kikao cha pamoja kilichofanyika leo  Agosti 31, 2018 katika Chuo Kikuu cha Dodoma Jijini Dodoma.  

Naye Mwenyekiti wa Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Ualimu Morogoro Agustine Sahili amesema wanaishukuru Wizara kwa kuandaa vikao vya aina hiyo kwani vinawasaidia kuwakumbishia taratibu za kazi na kuahidi kutekeleza yale yote waliyoagizwa ili kuimarisha utendaji katika maeneo ya kazi.

Kikao kazi hicho kimeshirikisha Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali 35 vilivyopo hapa nchini.
Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali wakiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo 

PROF. MDOE AITAKA ESPJ KUACHA ALAMA NA KUTEKELEZWA KATIKA MUDA ULIOPANGWA


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe ameutaka Mradi wa Kukuza Ujuzi na Stadi za Kazi kwa lengo la kuzalisha ajira (ESPJ) kuhakikisha inatekeleza vizuri malengo ya mradi yaliyokusudiwa ikiwa ni pamoja na kuonyesha thamani ya fedha ili Taifa liweze kufikia malengo ya nchi ya kufikia uchumi wa viwanda hadi ifikapo mwaka 2025.

Profesa mdoe ametoa maagizo hayo mkoani Morogoro wakati wa kikao kazi cha waratibu wanaohusika na mradi wa ESPJ kutoka kwenye Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na sekta binafsi na kusisitiza kuwa mradi huo unatakiwa kufanya mambo ambayo yataacha alama ikiwa ni pamoja na  kuhakikisha unafanyika katika muda uliopangwa.

“Bado tuko nyuma katika utekelezaji, wadau na viongozi wanajiuliza umuhimu wa huu mradi, sasa tutekeleze vizuri mradi  ili thamani ya fedha ionekane. Mradi huu upo kwenye moyo wangu nitafurahi kuona unaacha alama na katika kujifunza tuangalie namna mradi wa EP4R ulivyoacha alama, sasa ESPJ na yenyewe ifanye hivyo hivyo,”amesema Profesa Mdoe.
Naibu katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe akizungumza na Waratibu wa Mradi wa Kukuza ujuzi na Stadi za Kazi kwa lengo la kuzalisha ajira (ESPJ), hawapo pichani ambapo ameutaka mradi huo utekelezwe na uwe na matokeo chanya.

Naibu Katibu Mkuu huyo pia amesema kuwa kiuhalisia mradi umechelewa kuanza sasa katika kuutekeleza lazima umakini uwepo ili matokeo chanya ya mradi huo yaweze kuonekana.

Kikao kazi hicho kinahusu uwasilishaji wa  ripoti mbalimbali zinazohusu utekelezaji wa mradi , ikiwa ni pamoja na kufanyika majadiliano ya pamoja kwa lengo la kujengeana uwezo kutoka Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Idara ya Elimu ya juu, Kitengo cha Sheria, Idara ya Sera na Mipango, mratibu kutoka ofisi ya TPSF, pamoja na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini.
Waratibu wa Mradi wa Kukuza ujuzi na Stadi za Kazi kwa lengo la kuzalisha ajira (ESPJ) wakiwa katika kikao kazi cha kujengeana uwezo mara baada ya kuwasilishwa kwa ripoti mbalimbali kuhusu utekelezaji wa mradi huo. Kikao hicho kinafanyika kwa siku mbili, Agosti 31 mpaka Septemba 1 mkoani Morogoro.


MINISTRY OF EDUCATION, SCIENCE AND TECHNOLOGY

SCHOLARSHIP TENABLE IN BRAZIL FOR THE ACADEMIC YEAR 2018/2019
Call for Application
The General Public is hereby informed that, the Republic of Brazil under the Coordination of the Improvement of Higher Education Personnel (CAPES) is offering PhD Scholarships to Tanzanian Citizen.  Successful candidates will be required to pursue their studies in various public higher learning institutions in Brazil for the academic year 2018/2019.  For more information the modes of application and other requirements please follow the provided links.
Mode of Application

All Applicants are requested to complete application online on http://www.inscricao.copess.gov.br/individual.

Through which you will find link that will guide you to register and fill application form and upload all documents required and finally submit online.

The following are the documents required to be uploaded as attachments:-

i                      Page of your Passport;
ii                   Birth Certificate ;
iii                 Academic Certificates ;
iv                 Academic Transcripts;

NB: Detailed information regarding the Scholarships can be accessed from the following webpage: http://www.inscricao.copess.gov.br/individual/cooperacao
International/multinational/pec-pg
This is issued by




Permanent Secretary
Ministry of Education, Science and Technology
University of Dodoma
College of Business and Law
Block 10
P .O. Box 10
40479 Dodoma.
Deadline for applications is 31th August, 2018

Alhamisi, 30 Agosti 2018

DK. SEMAKAFU: WATHIBITI UBORA WA SHULE HAKIKISHENI ELIMU INAYOTOLEWA NCHINI INAKIDHI VIGEZO.


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. AveMaria Semakafu amewataka Wathibiti Ubora wa Shule nchini kutumia taaluma zao kuhakikisha kwamba Elimu inayotolewa nchini ni ile inayozingatia vigezo, kanuni na taratibu za nchini na si vinginevyo.

Dk Semakafu ameyasema hayo Mkoani Morogoro wakati wa kufungua mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni (SWASH) kwa wathibiti ubora wa Shule wa Wilaya ambapo amesema kwa kufanya hivyo kutasaidia kujua changamoto zinazokwamisha upatikanaji wa Elimu bora katika maeneo yao.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu akizungumza na Wathibiti Ubora wa Shule wa Wilaya (hawapo pichani) wanaoshiriki mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni (SWASH) yanayofanyika katika Chuo Cha Ualimu Morogoro mkoani Morogoro kuanzia Agosti 27 hadi 31, 2018

Dk. Semakafu pia amewataka Wathibiti ubora kufanya utafiti, kuainisha changamoto zilizopo katika maeneo mbalimbali ya shule pamoja na kuandaa ripoti na mapendekezo ambayo wanadhani Programu ya SWASH itaweza kusaidia kutatua.

“Mafunzo haya mliyoyapata yaende kuwasaidia katika kufanya tafiti, kuanisha changamoto zilizopo katika maeneo mbalimbali ya shule pamoja na kuandaa ripoti na kutoa mapendekezo, ambayo yatasaidia kuimarisha utendaji na kuwashirikisha wale ambao hawajapata mafunzo hayo kwa kuwa sasa mmekuwa na uelewa mpana kuhusiana na masuala ya huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni,” amesema Semakafu


Baadhi ya Wathibiti Ubora wa Shule wa Wilaya wakifuatilia hotuba ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu wakati akifungua mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni (SWASH), mafunzo ambayo yanafanyika  mkoani Morogoro kuanzia Agosti 27 hadi 31, 2018.

Amewataka pia kuhamasisha upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo wanayofanyia kazi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha Elimu ya afya na mazingira safi yanapatikana Shuleni ili watoto waweze kupata Eimu bila changamoto yoyote.

Mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni   yameshirikisha Wathibiti Ubora wa Wilaya 48 kutoka Mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, Lindi, Pwani, Morogoro, Iringa, Singida na Manyara.
Wathibiti Ubora wa Shule wa Wilaya wanaoshiriki mafunzo ya Muongozo wa Huduma ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira Shuleni (SWASH) wakiwa katika picha ya pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu mkoani Morogoro

Jumatano, 29 Agosti 2018

SERIKALI HAITAMVUMILIA ATAKAYEFANYA SHULE KUTOKUWA SEHEMU SALAMA KWA WANAFUNZI


Serikali imesema haitavumilia mtu yeyote ambaye atafanya matendo yatakayoashiria kwamba shule si mahala salama kwa mwanafunzi, pamoja na kuwatia hofu wazazi waogope kuwaruhusu watoto kwenda kupata Elimu.

Kauli hiyo ya Serikali imetolewa leo na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknlojia Profesa Joyce Ndalichako siku moja baada ya kuwepo kwa taarifa juu   mwalimu Respicius Patrick wa Shule ya Msingi Kibeta iliyopo mkoani Kagera kumpiga hadi kumsababishia kifo mwanafunzi Sperius Eradious mwenye umri wa miaka 13 wa darasa la tano.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiwakabidhi sheria na kanuni Wajumbe wa Bodi mpya ya Baraza la Mitihani Tanzania katika uzinduzi wa Bodi hiyo uliyofanyika jijini Dar es Salaam

Waziri Ndalichako amesema Shule ni mahala salama kwa wanafunzi kujifunza, kitendo hicho kilichofanywa na mwalimu huyo ni kinyume na malengo ya serikali  ambayo imekuwa ikiboresha Elimu na kufanya kazi kubwa ya kuhakikisha watoto wanapata Elimu bora na tena kwenye mazingira mazuri.

“ Suala ambalo limefanywa na huyu Mwalimu ni kinyume kabisa na maadili ambayo Mwalimu anatakiwa kuwa nayo, kwa umri ambao mwanafunzi alikuwa nao Mwalimu ndiyo alitakiwa awe msaada mkubwa wa kumuelimisha na kumfundisha mwanafunzi,niendelee kuwaomba Watanzania waendelee kuwa watulivu, wakati vyombo vya Sheria vinaendelea kufanya kazi yake,” alisema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wataalamu wa waandaaji wa walimu wa somo la hesabu (hawapo pichani) jijini Dar es Salaam, ambapo amewataka walimu kuangalia namna nzuri ya kumuandaa mwanafunzi kupenda somo la hesabu.

Katika hatua nyingine Waziri Ndalichako amewataka wataalamu wa somo la hesabu kuangalia namna bora ya kuimarisha ufundishaji wa somo la hilo ili kuwezesha walimu  kufundisha na kuhamasisha wanafunzi kupenda somo hilo.

Waziri Ndalichako amesisitiza hilo katika kongamano la tano la wataalumu wanaoandaa walimu wa somo la hesabu Barani Afrika kuwa ni muhimu kuangalia mbinu wanazopewa walimu wanaofundisha somo hilo kama zinawasaidia kufundisha kwa kutumia njia shirikishi.
Kongamano linalowakutanisha wataalamu wa hesabu linafanyika jijini Dar es Salaam kwa kwa lengo la kuimarisha ufundishaji wa somo la hesabu ambapo mgeni rasmi katika kongiomano hilo ni Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako.  

Kupitia kongamano hilo amewataka kuangalia pia namna nzuri ya kuwezesha walimu wa hesabu kuondoa dhana potofu kwa wanafunzi kuwa somo hilo ni gumu, na kusisistiza kuwa mwanafunzi akielewa hesabu inamuwezesha kumudu masomo mengine vizuri kutokanana kutumia zaidi mantiki katika kutatua hesabu.

Akiwa jijini Dar es salam Waziri Ndalichako pia amezindua bodi ya Baraza la Mitihani la Tanzania ambapo amewataka wajumbe wa Baraza hilo kuhakikisha mitihani inaandaliwa katika ubora unaotakiwa na wahakikishe wanakuwa  na umakini katika uendeshaji wa Kazi zote zinazohusiana na mitihani.

Jumanne, 28 Agosti 2018

WAZIRI NDALICHAKO AWATAKA WALIMU WA DARASA LA KWANZA NA LA PILI KUONESHA UMAHIRI KATIKA KUFUNDISHA STADI ZA KKK


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amewataka walimu walioshiriki mafunzo ya kujengewa uwezo wa kumudu Stadi za Kusoma Kuandika na Kuhesabu (KKK) kuonesha umahiri unaotakiwa katika kufundisha Stadi hizo ili kuleta mabadiliko chanya miongoni mwa wanafunzi wa darasa la kwanza na la pili pindi watakaporejea katika vituo vyao vya kazi.

Waziri Ndalichako ameyasema hayo mkoani Morogoro wakati akifunga mafunzo hayo ambapo amesema pamoja na mambo mengine ana imani kuwa kupitia mafunzo hayo walimu wa darasa la kwanza na la pili wameongeza mbinu ambazo watazitumia kuwafundishia wanafunzi waweze kumudu stadi hizo kwani ndio msingi bora wa kumudu masomo yanayofundishwa kwenye darasa la tatu hadi darasa la saba.

“Nyumba imara hujengwa na msingi imara hivyo mafunzo haya ni muhimu sana kwenu walimu mnaofundisha Darasa la kwanza na la pili ili muweze kuwaandaa wanafunzi kumudu vyema masomo katika ngazi za Elimu zinazofuata” Alisisitiza Ndalichako

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiongea na walimu (hawapo pichani) wakati wa kufunga mafunzo ya uimarishaji wa Stadi za KKK. Amewataka walimu hao kutumia mbinu walizopata, upendo na hamasa kuwafundisha watoto ili wapate ujuzi na maarifa yatakayoleta tija katika Taifa

Waziri Ndalichako alisema lengo la Serikali ni kuendelea kuwapatia walimu wengi mafunzo ya ufundishaji wa Stadi za KKK pamoja na mbinu zingine za ufundishaji.

“Mtakumbuka Agosti 18, 2018 nilizindua matumizi ya Vikaragosi katika kufundisha Stadi za Kusoma Kuandika na Kuhesabu kwa Wanafunzi wa darasa la kwanza na la pili jijini Dar es Salaam, hizi zote ni juhudi za Serikali kuhakiksha ufundishaji unaimarika na wanafunzi wanaelewa” Aliongeza Waziri Ndalichako
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akipokea Kitabu cha Picha kama zawadi kutoka kwa walimu walioshiriki mafunzo ya kuimarisha Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) katika Chuo cha Ualimu Morogoro, Mjini Morogoro.

Katika hatua nyingine Waziri Ndalichako amewataka Walimu wote nchini kuunga mkono juhudi za serikali za kuunda bodi ya utaalamu wa walimu kwa kuwa ina lengo la kuutambua ualimu kama taaluma na utaalamu ikiwa ni pamoja na kulinda hadhi ya mwalimu.

Mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kumudu Stadi za KKK yanatolewa kwa walimu 1600 wa mikoa ya Dar es Salaam, Geita, Kagera, Mwanza na Tanga ambayo shule zake zina mkondo zaidi ya mmoja. 
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akigawa cheti kwa mmoja wa walimu walioshiriki mafunzo ya uimarishaji wa Stadi za KKK wakati wa kufunga mafunzo hayo yaliyofanyika katika Chuo cha Ualimu Morogoro, Mkoani Morogoro.

Jumatatu, 27 Agosti 2018

WAANDISHI WA HABARI WATAKIWA KUANDIKA HABARI ZA SAYANSI NA TEKNOLOJIA

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia DK Leonard Akwilapo amewataka Waandishi wa habari nchini kujikita katika kuandika habari za Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ili kuleta matokeo chanya katika kuelekea uchumi wa viwanda. 

Akizungumza wakati wa kutoa tuzo za umahiri kwa waandishi wa habari wa masuala ya Sayansi na Teknolojia zilizoandaliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia kupitia Jukwaa la Bioteknolojia kwa Kilimo jijini Dar es Salaam amesema kuwa Dunia inategemea Sayansi na Teknolojia katika kuleta mabadiliko  endelevu ya kimaendeleo
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo  akimkabidhi mmoja wa washindi wa tuzo za umahiri kwa waandishi wa habari ya Sayansi na Teknolojia zilizoandaliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia kupitia Jukwaa la Bioteknolojia kwa Kilimo zilizofanyika jijini Dar es Salaam

Aidha, ameipongeza tume hiyo kwa kuona umuhimu wa kutoa taarifa ya nini inafanya kwa wananchi kwa kuwahusisha waandishi wa habari ambao wamekuwa wakitoa taarifa hizo kwa jamii kupitia vyombo vya habari

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia Dk. Amos Nungu amesema tuzo hizo zimeshirikisha kazi 56 kutoka katika vyombo 10 vya habari na kutoa wito kwa Waandishi wa Habari kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kuelimisha jamii mambo mbalimbali yanayohusu Sayansi na Teknolojia.

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo  akizungumza na waandishi wa habari pamoja na wanasayansi (hawapo pichani) wakati wa kutoa tuzo za umahiri kwa waandishi wa habari wa Sayansi na Teknolojia ambapo amewataka waandishi wa habari kujikita katika kuandika masuala ya sayansi na teknolojia ili kuwezesha wananchi kufikia uchumi wa viwanda wakiwa na taarifa sahihi

Alhamisi, 23 Agosti 2018


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA

    Anuani ya simu “ELIMU”
   Simu: 026  296 35 33
   Baruapepe:info@moe.go.tz
   Tovuti: www.moe.go.tz
  



  
     Chuo cha Masomo ya 
     Biashara na Sheria,
     Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Jengo Na. 10,
     S. L. P. 10,
     40479 DODOMA.           

   
TAARIFA KWA UMMA

KUHUSU MUSWADA WA SHERIA YA BODI YA KITAALAMU YA WALIMU TANZANIA

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Agosti 21, 2018 imewasilisha maelezo kuhusu Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu Tanzania katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Jijini Dodoma.
Muswada wa Sheria hii unalenga kuanzisha Bodi ya Kitaalam ya Walimu Tanzania itakayosimamia utaalamu wa ualimu nchini kwa walimu wote walio katika Utumishi wa Umma na Sekta Binafsi kuanzia walimu ngazi ya Astashahada, Stashahada na Shahada.

Pamoja na mambo mengine, Bodi itakayoundwa kwa Sheria hiyo: itasajili, itaweka viwango vya ubora wa ualimu, itasimamia maadili na miiko ya ualimu ya kitaalamu, itafanya tafiti kuhusu masuala ya utaalam wa ualimu na kusimamia maendeleo ya utaalamu wa ualimu kwa ujumla.

Uanzishwaji wa Bodi hiyo ni utekelzaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 inayohimiza Serikali kuhuisha Mfumo na Muundo wa Uongozi, Usimamizi na Uendeshaji wa Sekta ya Elimu ili uwe na tija na uwajibikaji, na kuhakikisha kuwa maadili na haiba ya walimu yamezingatiwa katika ngazi zote za elimu na mafunzo.

Inatarajiwa kwamba, baada ya Sheria inayopendekezwa kutungwa na kutekelezwa ipasavyo, matokeo yafuatayo kupatikana:

a) Walimu wote nchini kutambuliwa na kusajiliwa na chombo cha kitaalamu, hivyo kuwepo kwa mfumo madhubuti wa kushughulikia walimu watakao kwenda kinyume na maadili ya utaalamu wa ualimu.
b) Kuwa na mfumo mzuri wa usimamizi, uthibiti na uendelezaji wa utaalamu wa ualimu.
c)  Kulindwa kwa hadhi ya taaluma na utaalamu wa ualimu kwa kuzuia watu wasiokidhi vigezo na viwango stahiki kufanya kazi ya ualimu.
d)Walimu waliopo katika utumishi wa ualimu kuwa na sifa kulingana na matakwa ya Sheria inayopendekezwa, na hivyo jamii kupata elimu yenye viwango stahiki.

Muswada tajwa unatarajiwa kusomwa kwa mara ya pili na ya tatu katika Mkutano wa Kumi na Mbili (12) wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaotarajiwa kuanza Septemba 4, 2018.  
Wizara inawakaribisha wananchi kushiriki kikamilifu katika hatua zote za utungwaji wa Sheria hii ili kuweza kupata Sheria bora kwa maslahi mapana ya walimu na nchi kwa ujumla.

Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA
21/8/2018





Jumanne, 21 Agosti 2018

MAPENDEKEZO YA MUSWADA WA SHERIA YA BODI YA KITAALAMU YA WALIMU YAWASILISHWA KWENYE KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE


Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imewasilisha mapendekezo ya Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu Tanzania kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Akiwasilisha mapendekezo hayo Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa William Ole Nasha amesema Bodi hiyo itasimamia usajili, weledi na maadili ya kitaalamu ya walimu katika sekta ya umma na binafsi.

Naibu Waziri amesema kupitia bodi hiyo Pia itainua  hadhi ya taaluma ya ualimu kwa kusajili walimu wote kulingana na viwango vya ubora wa ualimu na kuwapa leseni ya kufundisha katika ngazi stahiki.

 Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akiwasilisha Mapendekezo ya Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Jijini Dodoma


Pia kupitia bodi hiyo ya kitaalamu itakuwa na jukumu la kuimarisha utaalamu wa walimu kwa kuchochea ari ya kujiendeleza kitaalamu miongoni mwa walimu na kuongeza fursa  za ajira katika soko la ndani na nje ya nchi.

Naibu Waziri Ole Nasha amesema utaalamu wa ualimu hapa nchini umekuwa ukisimamiwa na vyombo mbalimbali ambavyo vililenga kwenye ajira, maslahi ya walimu na maadili ya walimu kiutumishi huku masuala ya usimamizi na maendeleo ya utaalamu wa ualimu kutokuwa na sheria na chombo mahususi cha kuyasimamia. 

Amesema  kuundwa kwa Bodi mahsusi ya kusimamia Utaalamu wa Walimu ni suala la msingi katika kuinua ubora wa Elimu nchini na suala hili limezingatiwa kwenye Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 iliyotamka bayana kuwa Serikali itahuisha Mfumo na Muundo wa Uongozi, Usimamizi na Uendeshaji katika Sekta ya Elimu ili uwe na tija na uwajibikaji.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akiwasilisha Mapendekezo ya Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Jijini Dodoma

Pia Sera hiyo imetamka kuwa Serikali itahakikisha kuwa maadili na haiba ya ualimu na watumishi wengine yanazingatiwa katika ngazi zote za Elimu na mafunzo hivyo kuanzishwa kwake kuna tija katika usimamizi wa Utaalamu wa Ualimu.

Walengwa wa Bodi ya Kitaalam ya Walimu Tanzania inayopendekezwa itamhusu mtu yeyote aliyefuzu mafunzo ya ualimu katika Chuo cha Ualimu au Chuo Kikuu kinachotambuliwa na mamlaka husika katika ngazi ya Astashahada, Stashahada, Shahada, Shahada ya Uzamili na  Uzamivu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akiwa na Viongozi Wakuu wa Wizara, Wakurugenzi na watumishi wengine wa Wizara wakiwasili katika viwanja vya Bunge kwa ajili ya kuwasilisha Mapendekezo ya Muswada wa Sheria ya Bodi ya Kitaalamu ya Walimu kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii 

Jumapili, 19 Agosti 2018

SERIKALI KUTUMIA MBINU ZOTE ZA UFUNDISHAJI KUWEZESHA WATOTO KUJIFUNZA


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako amesema Serikali itatumia mbinu zote za ufundishaji ili kuwezesha watoto kujifunza kwa ufanisi.

Waziri Ndalichako amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa ufundishaji wa maudhui yaliyoandaliwa kwa mfumo wa kietroniki ambayo yatatumia Vikaragosi (Cartoon) kufundishia watoto wa madarasa ya chini.

 Waziri Ndalichako amesema njia hii Itasaidia watoto kuelewa kwa  urahisi kwani wapo  watoto wanaoelewa kwa kuona, kushika na kisikiliza.




Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na Wadau wa Elimu ( Hawapo Pichani)  wakati wa uzinduzi wa ufundishaji wa maudhui yaliyoandaliwa kwa mfumo wa kietroniki ambayo yatatumia Vikaragosi (Cartoon)


"ikumbukwe kwamba hakuna njia bora kuliko nyingine katika kufundisha, wapo watoto  wanaoelewa zaidi kwa kuona, kusilikiza ama Kufanya kwa vitendo hivyo ni muhimu kutumia njia zote ili tusiache mtoto yeyote bila kuelewa" Amesisitiza Waziri Ndalichako

Waziri Ndalichako amesema matumizi ya Vikaragosi yataleta ari kwa watoto kujifunza kwani wakati wa majaribio ya vikaragosi hivyo walionyesha hali ya kutaka kujifunza kwa kutumia.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akionyesha DVD zenye maudhui ya Kietroniki ambazo zitatumika kufandishia madarasa ya chini wakati wa uzinduzi wa ufundishaji wa maudhui yaliyoandaliwa kwa mfumo wa kietroniki ambayo yatatumia Vikaragosi (Cartoon)

Aidha, Waziri wa Elimu amewataka Maafisa Elimu Kata kote nchini kuhakikisha wanafatilia kwa ukaribu ufundishaji kwa kutumia Vikaragosi hivyo pindi  vitakaposambazwa shuleni.

Jumamosi, 18 Agosti 2018

DK. SEMAKAFU AKEMEA VITENDO VYA UNYANYAPAA DHIDI YA WANAFUNZI WENYE MAHITAJI MAALUMU.

Naibu Katibu Mkuu Dk. Ave Maria Semakafu amewataka walimu wanaofundisha wanafunzi wenye mahitaji maalumu kuacha vitendo vya unyanyapaa kwa wanafunzi hao, kwa kuwa taaluma waliyonayo inahitaji upendo na uvumilivu.

Dk. Semakafu ametoa kauli hiyo mkoani Mwanza wakati akizungumza na walimu hao ambao wanashiriki mafunzo maalumu ya siku 10 ya kuchambua mtaala ulioboreshwa wenye lengo la kuwajengea uwezo walimu wanaofundisha wanafunzi wenye ulemavu wa akili, wasioona na wanafunzi viziwi.
Naibu Katibu Mkuu akizungumza na walimu wanaoshiriki mafunzo ya kuchambua mtaala ulioboreshwa yanayofanyika katika Chuo Cha Ualimu Butimba mkoani Mwanza

Dk. Semakafu amesema pamoja na mambo mengine amewataka walimu kuacha masuala ya vitengo na badala yake walimu wafanye kazi zao kwa weledi, ikiwa ni pamoja na kuwa wanaharakati katika masuala ya Elimu.

“Walimu naomba niwaambie ukweli huko kwenye shule zetu tumeanzisha vitengo ambavyo havina sababu yoyote na tumekuwa hatufanyi kazi zetu kwa weledi, wengine hatufundishi kwa visingizo vya kuwa tunasimamia vitengo, tuache mara moja na badala yake tufundishe watoto wetu kwa weledi,” alisisitiza Dk. Semakafu.
Walimu wanaofundisha wanafunzi wenye mahitaji maalumu wakifuatilia mafunzo ya kuchambua mtaala mpya ulioboreshwa mkoani mwanza.

Katika mafunzo hayo baadhi ya Walimu walitaka kufahamu kuhusu suala la wanafunzi kuishia Darasa la Sita ambapo Dk. Semakafu alieleza kuwa Elimu inaongozwa na Sheria na Sheria yetu ya Elimu Msingi ni miaka Saba hivyo Sheria ya Elimu haijabadilika.


Mafunzo hayo yanashirikisha walimu 132 wanaofundisha wanafunzi wenye mahitaji maalumu kutoka mikoa wa Kagera, Geita, Kigoma, Mara, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Rukwa na Tabora.
Naibu Katibu Mkuu Dk. Ave Maria Semakafu akikagua vifaa katika maabara ya Baiolojia katika Chuo Cha Ualimu Butimba, mkoani Mwanza