Ijumaa, 3 Agosti 2018

WAZIRI NDALICHAKO AWATAKA WALIMU KUHAMASISHA WANAFUNZI KUSHIRIKI MAONESHO YA UBUNIFU


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako amewataka walimu wa shule za Sekondari kuwahamisha na kuwasaidia wanafunzi kuandaa bunifu zao  ili waweze kushiriki katika maonesho  mbalimbali ya sayansi, teknolojia na ubunifu yanayofanyika nchini.

Akizungumza katika sherehe za utoaji wa zawadi kwa washindi wabunifu walioshiriki katika Monesho ya nane ya taasisi ya Wanasayansi Chipukizi (YST) Jijini Dar es Salaam Waziri Ndalichako amesema ushiriki wa wanafunzi katika maonesho hayo utawasaidia kuinua vipaji vyao na kupenda masomo ya sayansi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikabidhi zawadi kwa washindi wa maonesho ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kutoka Shule ya Sekondari Msalato. Waziri Ndalichako  amewahimiza wanafunzi nchini kushiriki katika maonesho mbalimbali ya namna hiyo ili kukuza vipaji vyao.

Ndalichako amesema anatambua kuwa maonesho hayo yamesaidia mamia ya wanafunzi wa shule za sekondari nchini kuonyesha bunifu zao ambazo zimewawezesha  kuendelea kutafuta  maarifa ya kisayansi yatakayosaidia nchi kufikia  uchumi wa viwanda.

Waziri Ndalichako amesema Wizara yake kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia COSTECH) itaendelea kushirikiana na taasisi hiyo kuangalia namna bora ya kuinua vipaji na kuboresha tatifi zinazofanywa na wanafunzi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akimpongeza mmoja wa washindi wa kwanza wa bunifu zilizoonyesho katika maonesho ya Sayansi , Teknolojia na Ubunifu kutoka Shule ya Sekondari Msalato.

Katika kipindi cha miaka 7 iliyopita, Taasisi hiyo imeweesha zaidi wanafunzi elfu tano (5,000) kushiriki katika maonesho ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu pamoja na kutoa mafunzo kwa walimu zaidi ya 1000 wa shule za sekondari ya namna ya kusaidia na kuboresha tafiti zinazofanywa na wanafunzi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akishangilia na kufurahia pamoja na wanafunzi walioshinda zawadi mbalimbali katika maonesho ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu yaliyoshirikisha shule mbalimbali nchini.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni