Jumamosi, 27 Oktoba 2018

DHAMIRA YA SERIKALI YA KUWA NA CHUO KIKUU CHA KILIMO BUTIAMA IKO PALEPALE


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amesema dhamira ya Serikali ya kumuenzi baba wa Taifa Mwalimu Jullius K. Nyerere kwa kuwa na Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi na Teknolojia, (MJUNAT) iko palepale.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo akiwa Wilayani Butiama mkoani Mara mara baada ya kutembelea Chuo hicho kwa lengo la kukagua miundombinu yake, pamoja na kuzungumza na watumishi wanaofanya kazi chuoni hapo.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Mara Adam Malima wakitoka nje mara baada ya kukagua  bwalo la chakula katika Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi na Teknolojia cha Mwalimu Nyerere.

Akizungumza na Watumishi wa Chuo hicho pamoja na viongozi wa Mkoa na wale wa Wilaya ya Musoma na Butiama amesema hivi sasa Serikali iko katika hatua za mwisho za makabidhiano ya miundombinu hiyo kutoka kwa aliyekuwa mmiliki wa majengo hayo Nimrod Mkono.


Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu Moshi Kabengwe na Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia CPA (T) Rose Waniha wakifuatilia jambo wakati wa kikao cha Waziri kwenye Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi na Teknolojia cha Mwalimu Nyerere kilichopo Wilayani BUTIAMA mkoani Mara.

Waziri Ndalichako amesema lengo la kuwa na Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi na Teknolojia ni kumuenzi baba wa Taifa kwa kutambua mchango wake katika suala la kilimo na kuwa suala hili pia limeanzishwa kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi.


“Mchakato huu ulianza mwaka 2016 na kuwa hapo awali majengo haya yalikuwa yanamilikiwa na Nimrod Mkono, hivyo Serikali haiwezi kujenga au kuboresha bila kuwa na maandishi ya kisheria ya umiliki halali. Napenda kueleza kuwa makabidhiano yako katika hatua za mwisho ili Serikali iweze kuendelea na taratibu nyingine” alisema Ndalichako.
Waziri Wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akipokelewa na Watumishi katika Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi na Teknolojia cha Mwalimu Nyerere, kilichopo Butiama, Mkoani Mara.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni