Jumatano, 31 Oktoba 2018


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA

Anuani ya simu “ELIMU”
Simu: 026  296 35 33
Baruapepe:info@moe.go.tz
Tovuti: www.moe.go.tz



  
Chuo cha Masomo ya  Biashara na Sheria,
Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Jengo Na. 10,
S. L. P. 10,
40479 DODOMA.           



TAARIFA KWA UMMA
KUFANYA MALIPO KUPITIA MFUMO MPYA WA SERIKALI WA GePG
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia inapenda kuutaarifu Umma ya kwamba kuanzia tarehe 01 Novemba 2018, itahamia rasmi katika mfumo wa kukusanya mapato ya Serikali kwa njia ya kieletroniki ujulikanao kama ‘Government e-Payment Gateway’ (GePG) kwa matakwa ya Sheria ya Fedha za Umma, Sura 348.

Wizara, itaanza kutumia mfumo huu kwenye makusanyo yake yote ya mapato kwa Vyuo vya Ualimu vya Serikali, Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi na Kanda za Uthibiti Ubora wa Shule. Hivyo mteja atapaswa kufika au kuwasiliana na kituo husika anachotaka kufanya malipo ili kupata namba ya utambulisho wa malipo husika (Payment Control Number) kabla ya kufanya malipo.

Wizara kwa kushirikiana na Wataalamu wa mfumo kutoka Wizara ya Fedha na Mipango itahakikisha mfumo huu unafanya kazi bila kuathiri utoaji wa huduma. Aidha, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia inaungana na Wizara na Taasisi nyingine za Serikali zinazotumia mfumo huo kwa mafanikio. Baadhi ya Wizara na Taasisi hizo ni Polisi, Brella, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi, TRA, Bodi ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) pamoja na Mamlaka ya Maji.
Namna ya kulipa kwa kutumia mfumo wa kieletroniki (Government e-Payment Gateway);
1.   Malipo yanaweza kufanywa kwa njia ya kibenki kwa kufuata hatua zifuatazo;
a)     Unapopata kumbukumbu ya malipo (Control Number);
b)     Tembelea Tawi lolote la Benki ya CRDB, NMB na NBC;
c)      Baada ya kuwasili kwenye benki, mpe mtoa huduma wa dirishani namba kumbukumbu ili kukamilisha mchakato wa malipo yako.

2.    Malipo yanaweza pia kufanywa kwa njia ya mtandao wa simu za mikononi (M-pesa, Tigo Pesa na Airtel Money) kwa kufuata hatua zifuatazo;
a)     Kupitia simu yako, piga *150*00#, au *150*01# au *150*60#;
(Kupata M- pesa, Tigo Pesa na Airtel Money);
b)     Chagua ‘Lipia malipo (Pay-Bills)’;
c)      Chagua ‘Malipo ya Serikali’;
d)    Chagua ‘Ingiza namba ya malipo’ na uingize namba ya kumbukumbu ya malipo (Control Number);
e)     Weka kiasi cha fedha unachotaka kulipa;
f)      Thibitisha muamala wako kwa kuingiza neno au namba yako ya siri; na
g)     Hifadhi ujumbe wa simu uliopokea kama ushahidi wa malipo endapo utahitajika kuonyesha kwa kituo husika.

Imetolewa na;

Dkt. Leonard D. Akwilapo
KATIBU MKUU
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni