Alhamisi, 25 Oktoba 2018

SERIKALI YAAHIDI KUENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA YA WATU WENYE ULEMAVU


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri zote nchini kuhakikisha wanatenga asilimia 2 ya bajeti zao kwa ajili ya kuhudumia watu wenye ulemavu na kuwa suala hilo lipo kisheria.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Fimbo Nyeupe duniani ambayo Kitaifa hapa nchini yamefanyikia Mkoani Mwanza.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisalimiana na Mkurugenzi Msaidizi wa idara ya           Elimu Maalumu wa Wizara hiyo Adamson Shimbatano aliyeshika Fimbo Nyeupe wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Fimbo Nyeupe duniani ambayo kitaifa yamefanyikia mkoani Mwanza.

Ndalichako amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe. Rais John Magufuli imeendelea  kuboresha mazingira ya watu wenye ulemavu ikiwa ni pamoja na kutoa ajira na kuwa katika ajira za mwaka jana  walimu 70 wasioona waliajiriwa.

“Niwahakikishie Watanzania kuwa Rais John Magufuli ni kiongozi anaejali sana watu wenye ulemavu ndiyo maana wapo viongozi wenye ulemavu aliowateua kushika nafasi mbalimbali za uongozi katika Serikali yake wakiwemo Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi, Mabalozi, na wengine ili wamsaidie katika kutekeleza majukumu ya kuliletea Taifa Maendeleo,” alisema Ndalichako.

Waziri Ndalichako pia amewataka Wazazi kuacha tabia ya kuwaficha watoto wasioona na badala yake wahakikishe watoto wote waliofika umri wa kwenda Shule wanaandikishwa kwa kuwa hivi sasa Elimu msingi inatolewa bila malipo na kuwa ulemavu siyo kikwazo cha Maendeleo.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akipokea msaada wa Fimbo Nyeupe kutoka kwa mmoja Wafanyabiashara mkoani Mwanza, ili fimbo hizo zigaiwe kwa watu wasioona walioshiriki maadhimisho hayo mkoani Mwanza.

Akizungumza katika Maadhimisho hayo Mwenyekiti wa Shirikisho la watu wenye ulemavu nchini Tanzania Benedict Louis amempongeza na kumshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa uongozi wake wa kutambua jitihada na uwezo wa watu wenye ulemavu na hivyo kuwateua wenye ulemavu kushika nafasi mbalimbali.

Louis ameeleza kuwa Siku ya Fimbo Nyeupe ni muhimu kwa kuwa inatoa fursa kwa wasioona kutathmini jitihada zinazofanywa na serikali katika kuleta ustawi kwa watu wenye ulemavu na kuwa Fimbo hiyo ni nyenzo muhimu ambayo inamsaidia asiyeona kutambua vikwazo vilivyo mbele yake.

Kauli mbiu  ya mwaka huu katika maadhimisho hayo ni “ Mafunzo ya TEHAMA kwa wasioona ni nyenzo Shirikishi ya uchumi wa Viwanda.”
Watu wasioona wakicheza mziki pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako wakati wa maadhimisho ya siku ya Fimbo Nyeupe ambayo kitaifa yamefanyikia mkoani Mwanza na kauli mbiu katika maadhimisho hayo ni mafunzo ya TEHAMA kwa wasioona ni nyenzo shirikishi ya uchumi wa Viwanda.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni