Jumamosi, 2 Machi 2019

WAZIRI NDALICHAKO ATAKA WANAWAKE KUSHIKAMANA NA KUSAIDIA MAKUNDI YA WATU WASIOJIWEZA


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako amewataka wanawake kuwa mstari wa mbele katika kusaidia makundi ya watu wasiojiweza hasa watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

Prof Ndalichako ametoa wito huo mkoani Kigoma wakati akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya siku ya maombi ya dunia ya umoja wa wanawake  wa kikristo  Tanzania  CCT na kusema kuwa wanawake  wakiamua wana uwezo mkubwa wa kubadili maisha katika jamii.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akizungumza wakati wa kilele cha maadhimisho ya siku ya maombi ya dunia kwa wanawake mkoani Kigoma. Amewataka wanawake kuwa mstari wa mbele kuyasaidia makundi ya watu wasiojiweza na hasa watoto wanaoishi katika mazingira magumu ili wapate haki zao za msingi hususan elimu.

Amesema wanawake ndio walezi wa watoto kuanzia ngazi za familia akiwafananisha na walimu kwani wao wana jukumu la kulea na kufundisha watoto wote.

“Wanawake wenzangu tukumbushane msemo ambao Mama Salma Kikwete ambae ni mke wa Rais Mstaafu wa awamu ya Nne Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amewahi kusema kuwa mtoto wa mwenzio ni wa kwako hivyo tuwasaidie watoto yatima, wa mitaani na wale wanaoishi katika mazingira magumu ili waweze kutimiza ndoto zao hasa za  kupata elimu,” alisisitiza Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako (aliyepo katikati) akicheza na moja ya kwaya iliyotumbuiza wakati wa kilele cha maadhimisho ya siku ya maombi ya dunia kwa wanawake katika Kanisa la Anglikan lililopo mkoani Kigoma.

Pia, Waziri Ndalichako amewataka wanawake nchini kudumisha mshikamano miongoni mwao na kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Mhe. Rais Dkt. John Magufuli kwa vitendo kwa kuhakikisha wanafanya shughuli mbalimbali za uzalishaji mali kwa lengo la kujipatia kipato.

Akiwa mkoani humo waziri Ndalichako pia aliwatembelea wagonjwa ambao wamelazwa katika hospitali ya rufaa ya  Kigoma Maweni na kutoa misaada mbalimbali kwa wagonjwa hao.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiwajulia hali baadhi ya wagonjwa waliolazwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Kigoma Maweni. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni