Jumatatu, 8 Aprili 2019

NORWAY NA TANZANIA KUENDELEA KUSHIRIKIANA KATIKA SEKTA YA ELIMU


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Norway nchini Tanzania Elisabeth Jacobsen mjini Dodoma ambapo pamoja na mambo mengine wamezungumzia kuendeleza ushirikiano katika sekta ya elimu kati ya nchi hizo mbili.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akifanya mazungumzo na Balozi wa Norway Elisabeth Jacobsen kuhusu Sekta ya Elimu.

Waziri Ndalichako ameishukuru serikali ya Norway kwa kuendelea kufadhili sekta ya elimu kupitia Mfuko wa Global Partnership for Education (GPE ) na amemuhakikishia Balozi Jacobsen kuwa fedha zote zinazotolewa na kupitia mpango huo zitatumika kama ilivyokusudiwa.

Waziri Ndalichako amevitaja vipaumbele vya ufadhili huo kuwa ni masuala ya uthibiti ubora wa shule, ununuzi wa  vitabu na kutoa  mafunzo kwa walimu walio kazini.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na Balozi wa Norway Elisabeth Jacobsen pamoja na viongozi wengine Mjini Dodoma

Kwa upande wake Balozi wa Norway nchini Tanzania, Elisabeth Jacobsen, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa kupiga hatua kubwa katika elimu na kueleza kuwa wanaridhishwa na utekelezaji wa mradi wa uanzishaji Kituo cha kufuatilia Hewa ya Ukaa katika  Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA).

Kituo hicho kinafadhiliwa na Serikali ya Nchi ya Norway kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiagana na Balozi wa Norway Elisabeth Jacobsen

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni