Ijumaa, 12 Aprili 2019

PROF. MDOE AZUNGUMZIA UTEKELEZAJI WA KUANZISHWA VITUO VYA TEKNOLOJIA


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. James Mdoe leo amefungua Kikao Kazi cha kupitia na kutoa maoni yatakayowezesha kuboresha rasimu ya Mwongozo na Mpango wa Utekelezaji wa kuanzisha vituo vya Teknolojia nchini.

Akizungumza na washiriki wa kikao hicho mkoani Dodoma Prof. Mdoe ameainisha kuwa Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano, unalenga katika kujenga uchumi wa viwanda ili kuchochea mageuzi ya uchumi na maendeleo ya watu.
Naibu Katibu Mkuu Prof. James Mdoe akizungumza na washiriki (hawapo pichani) katika kikao Cha kujadili rasimu ya mwongozo wa kitaifa wa kuanzisha na kuendeleza vituo vya Teknolojia na ubunifu. Kikao hicho kimefanyikia mkoani Dodoma.
Amesema Mpango huo, umebainisha umuhimu wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu katika maendeleo ya nchi na Uendelezaji wa Teknolojia na Ubunifu kuwa unakabiliwa na changamoto ya kuwepo kwa vituo mahiri vya kuzilea, kuziendeleza au kuhawilisha teknolojia na bunifu ili kuzigeuza na kuwa fursa za kiuchumi.
Baadhi ya washiriki wakifuatilia Hotuba ya mgeni rasmi wakati wa kikao cha kujadili rasimu ya Mwongozo wa kitaifa wa kuanzisha na kuendeleza vituo vya Teknolojia na ubunifu.
Prof. Mdoe amesema vituo vya kuendeleza teknolojia na ubunifu ni nyezo muhimu katika maendeleo ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu na huchochea kuwepo kwa tija katika kuleta maendeleo ya jamii na nchi kwa ujumla.

“Uwepo wa vituo hivyo hujenga mazingira wezeshi kwa Taasisi za utafiti na maendeleo kwa kutoa huduma za kulea, kuendeleza na kuhawilisha  teknolojia kwa makampuni madogo na ya kati (SMEs).  Aidha, vituo hivi vina umuhimu wa kutoa ufumbuzi wa kisayansi, na kiteknolojia katika kutatua changamoto zinazoikabili jamii,” alisisitiza Prof. Mdoe.

Washiriki wa kikao cha kujadili rasimu ya mwongozo wa kitaifa wa kuanzisha na kuendeleza vituo vya Teknolojia na ubunifu wakiwa katika picha ya pamoja na mgeni rasmi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu Prof. Maulilio Kipanyula ameeleza kuwa umuhimu wa vituo hivyo ni kuimarisha matumizi chanya ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kama vile Teknolojia za kuendeleza viwanda.

Naibu Katibu Mkuu Prof.James Mdoe aliyekaa katikati akisoma hotuba yake wakati akifungua mkutano wa wadau wa kujadili rasimu ya mwongozo wa kitaifa wa kuanzisha na kuendeleza vituo vya Teknolojia na Ubunifu kikao ambacho kinafanyika mkoani Dodoma.

Kikao kazi hicho cha siku moja kimehudhuriwa na washiriki kutoka Wizara mbalimbali, Taasisi zinazojishughulisha na masuala ya utafiti, na Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Washiriki wa kikao wakipiga makofi ikiwa ni ishara ya kumpongeza mgeni rasmi kwa hotuba nzuri aliyoitoa wakati akifungua mkutano wa wadau wa kujadili Rasimu ya Mwongozo wa kuanzisha vituo vya teknolojia.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni