Jumatatu, 1 Aprili 2019

WAZIRI WA ELIMU AZINDUA UKUMBI WA KISASA WA MIHADHARA CHUO CHA KUMBUKUMBU YA MWALIMU NYERERE


Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amezindua ukumbi wa mihadhara wa kisasa katika Chuo Cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere uliojengwa mapato ya ndani ya Chuo hicho.

Akizundua ukumbi huo wa Mihadhara kigamboni jijini Dar es salaam Waziri Ndalichako amepongeza Bodi ya Utawala na Uongozi wa Chuo hicho kwa kusimamia vema matumizi ya fedha zinazotokana na Mapato ya ndani na kutumia kutekeleza miradi yenye tija kwa Chuo na Taifa kama ilivyofanyika katika ujenzi wa Ukumbi huo na pia amewataka uongozi kusimamia Dira na Dhima ya uanzishwaji wake kwa kujikita katika kutoa mafunzo ya Uongozi, Utawala na Maadili.

Waziri Ndalichako amewapongeza Watendaji wa Chuo kwa kusimamia kwa karibu utekelezaji wa Mradi huo hadi kufikia hatua ya kukamilisha japo kwa kuchelewa kwa karibu miezi tisa.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikata utepe kuashiria  uzinduzi wa Ukumbi mpya wa Mihadhara uliyojengwa katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Kampasi ya Kivukoni uliojengwa kwa kutumia mapato ya ndani ya Chuo hicho.

“ nimefurahishwa na kazi hii nzuri iliyofanyika hapa, kwakweli ni jengo zuri lenye ubora wa hali ya juu na ambalo litawafanya wanafunzi kuongeza ari ya kujifunza na ninategemea kuona jengo hili likituzwa vizuri ili litumike kwa miaka mingi likiwa na ubora uleule”. Amesisitiza Ndalichako

Aidha Ndalichako amezitaka Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kuthamini na kutumia vizuri mapato yake ya ndani kwa ajili ya kutekeleza mipango na Miradi mbalimbali ya Maendeleo katika taasisi hizo ili kuleta maendeleo ya haraka badala ya kuzitumia fedha hizo kwa matumizi mengine yasiyo na tija.

Wakati huo amewataka Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) ambao ni wakandarasi  wa ujenzi wa Ukumbi huo kukamilisha miradi mingine iliyo chini ya Wizara ya Elimu ikiwemo ukarabati wa shule Kongwe mfano Kibaha Sekondari, Shule ya Sekondari ya Wasichana Songea pamoja na ujenzi wa Hosteli na miundombinu mingine katika Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili Kampasi ya Mloganzila.

 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akimpongeza Mwenyekiti wa Bodi ya Utawala wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyereer Stepen Wasira wakati wa uzinduzi wa Ukumbi wa Mihadhara uliyojengwa katika Chuo hicho.



Nae Mwenyekiti wa Bodi ya Utawala ya Chuo hicho Stephen Wasira, amesema Chuo hicho kimejipanga kuhahakisha kinatoa elimu bora na wahitimu walio bora wenye weledi hasa katika eneo la uongozi na utawala ili kuenzi fikra na maono ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alieanzisha chuo hicho Mwaka 1961 kwa lengo la kuandaa viongozi na watawala.

Awali, Mkuu wa Chuo Prof. Shadrack Mwakalila akitoa taarifa ya mradi amesema jengo hilo limegharimu zaidi ya Shilingi za Tanzania Bilioni 1.1  na kwamba lina uwezo wa kuchukua wanafunzi 330 kwa wakati mmoja. Ameongeza kuwa pamoja na ukumbi wa Mihadhara jengo hilo lina ofisi nane za wahadhiri na mifumo ya kisasa ya sauti.
 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisalimiana na Bibi Thabita Siwale Waziri wa kwanza wa Elimu mwanamke Tanzania ambae pia alipitia mafunzo katika Chuo hicho aliyehudhuria hafla ya uzinduzi wa Ukumbi wa Mihadhara uliyojengwa katika Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni