Jumatano, 10 Julai 2019

BILIONI 40 KUJENGA VYUO VYA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI STADI KATIKA WILAYA 25


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amezindua Chuo cha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) cha Wilaya ya Urambo ambapo amesema serikali katika bajeti ya mwaka  huu imetenga jumla ya Shilingi bilioni 40  kwa ajili ya kujenga vyuo vipya  katika wilaya 25.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo mkoani Tabora wakati wa uzinduzi wa chuo hicho ambapo amesema ongezeko la vyuo vya ufundi nchini linasaidia kuongeza idadi ya wanafunzi wanaopata elimu ya ufundi ambao wanahitajika katika viwanda mbalimbali  vinavyoanzishwa nchini.

"Kadri tunavyoongeza vyuo hivi vya ufundi katika wilaya mbalimbali tunasogeza elimu  ya ufundi itolewayo na vyuo vya VETA karibu na wananchi ili kuwawezesha kupata ujuzi na stadi zinazohitajika katika kipindi hiki ambacho nchi yetu inalenga kujenga uchumi wa viwanda kuiwezesha kufikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025, " amesema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na viongozi  mbalimbali wa Serikali na  wananchi wa Mkoa wa Tabora (Hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa Chuo cha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA)

Amesema dira iliyowekwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli ya kujenga uchumi wa viwanda imekuwa chachu kwa wizara kuongeza kasi ya huduma ya mafunzo ya ufundi stadi ambapo mpaka sasa inakamilisha vyuo vya VETA katika Wilaya za Nkasi, Ileje, Newala na Muleba ambavyo vipo katika hatua za ukamilishaji.  Vyuo vingine vilivyo katika hatua ya ujenzi ni vya halmashauri ya Kasulu, Itilima, Ngorongoro, Chato, na Babati ambavyo vinatarajiwa kukamilika kabla ya kumaliza mwaka huu 2019.










 
Waziri Ndalichako amezitaja wilaya nyingine ambazo zitajengewa vyuo hivyo kuwa ni pamoja na Wilaya za Chunya, Kilindi, Korogwe, Ukerewe, Igunga, Pangani, Kishapu, Rufiji, Uyui, Kwimba, Bahi, Mafia, Longido, Mkinga, Uvinza, Ikungi, Iringa Vijijini, Lushoto, Mbarali, Monduli, Buhigwe, Ulanga, Masasi, Butiama na Chemba.

Aidha, Waziri Ndalichako amewashukuru Viongozi wa Mkoa wa Tabora, Halmashauri ya Wilaya ya Urambo, Mbunge wa Jimbo la Urambo, Mhe. Margreth Sitta na wananchi wote wa Wilaya hiyo kwa utayari wao wa kuhakikisha upatikanaji wa majengo na eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 45,000 kwa ajili ya Chuo cha VETA cha Urambo.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako pamoja na Viongozi wengine wakifurahia jambo mara baada ya kuzindua Chuo cha VETA cha wilaya ya Urambo Mkoani Tabora aliyevaa koti ni Mkuu wa Mkoa wa Tabora


Wakati huo huo Waziri Ndalichako ametumia nafasi hiyo kuagiza Uongozi wa VETA kukamilisha ujenzi unaoendelea wa vyuo vya VETA katika wilaya kwa wakati na ubora

Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanry, akizungumza katika uzinduzi huo, amewataka vijana wa wilaya ya Urambo kujiunga na chuo hicho ili kupata ujuzi na stadi zitakazowawezesha kufanya kazi katika miradi ya ujenzi ya kimkakati ya mkoa huo.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako, Mbunge wa Urambo Magreth Sit, Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanry pamoja na Viongozi wengine wakikata utepe kuashiria uzindua wa Chuo cha VETA cha wilaya ya Urambo Mkoani Tabora.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu, akitoa Maelezo  ya mradi huo amesema umehusisha ukarabati wa majengo, ununuzi wa samani za ofisi, vifaa na vitendea kazi vya ofisi , zana za kufundishia na  samani za mabweni ya wanafunzi umegharimu zaidi ya shlingi milioni 200.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako, akikagua baadhi ya vifaa vya kufundishia na kujifunzia vilivyonunuliwa kwa ajili ya Chuo cha VETA cha wilaya ya Urambo Mkoani Tabora.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni