Jumatano, 10 Julai 2019

SERIKALI YA AWAMU YA TANO YAANDIKA HISTORIA KWA KUFANYA UWEKEZAJI MKUBWA KWENYE SEKTA YA ELIMU


Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli imeandika historia kwa kufanya uwekezaji mkubwa kwenye Sekta ya Elimu kwa lengo la kutimiza azma yake ya kupata nguvu kazi iliyo mahiri katika sekta mbalimbali za ufundi itakayofanya kazi katika viwanda ili kufikia uchumi wa kati na wa viwanda ifikapo 2025.

Hayo yameelezwa Jijini Mwanza na Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia William ole Nasha alipofanya ziara katika Wilaya za Sengerema, Kwimba na Misungwi kukagua miradi ya maendeleo ya ujenzi wa ofisi mpya za Uthibiti ubora wa shule wilaya  na ukarabati wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDC) unaoendelea katika wilaya hizo.

Ole Nasha alisema pamoja na mambo mengine mengi ambayo serikali imetekeleza katika Sekta ya Elimu katika mwaka wa fedha 2019/20 Serikali imetenga fedha kiasi cha sh bilioni 40 kwa ajili ya ujenzi wa Vyuo vipya 25 vya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) vya Wilaya lakini pia kuna vyuo 5 vya mkoa vinaendelea kujengwa ili kuwezesha vijana wa kitanzania kusomea elimu ya ufundi itakayowawezesha kujiajiri.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua ujenzi wa majengo ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Karumo kilichopo Wilaya ya Sengerema Mkaoni Mwanza. 

Pia alisema Serikali inajenga na kukarabati vyuo 55 vya Maendeleo ya Wananchi (FDC) ili kuboresha miundombinu ya vyuo hivyo itakayotoa fursa kwa vijana wengi kujifunza na kupata elimu ya ufundi itakayowawezesha kufanya kazi za uzalishaji katika maeneo yao lakini pia watakuwa chachu ya maendeleo ambayo ndio Serikali inahitaji.



“Katika moja ya eneo ambalo Mhe. Rais Magufuli ameelekeza nguvu nyingi katika kipindi cha utawala wake ni kuboresha elimu na sababu ni rahisi  huwezi kusema unajenga nchi ili kufikia uchumi wa kati unaotegemea uchumi wa viwanda kama huna nguvu kazi iliyoelimika,”alisema Naibu Waziri Ole Nasha

Alisema kwa sasa ukitembea nchi nzima utaona ujenzi na ukarabati unaoendelea katika vyuo, shule za msingi na sekondari hii yote ni mkakati wa Serikali wa kuboresha elimu katika gazi zote za za elimu nchini.

“Mwaka uliopita pekee wizara ya Elimu, Saynsi na Teknolojia kupitia Programu ya EP4R imekarabati na kujenga miundombinu mipya kwenye shule zaidi ya 500 ambapo zaidi ya sh bilioni 90 zimetumika na hapa nazungumzia kile kinachotekelezwa na Wizara ya Elimu pekee na sio TAMISEMI. Hii inaakisi uwekezaji mkubwa ambao umefanyika kwenye sekta ya elimu,” alisema Naibu Waziri Ole Nasha.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua miundombinu ya vyoo katika moja ya bweni la wanafunzi katika Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Karumo Jijini Mwanza.


Alisema haya yote yanatokana na ukweli kwamba elimu ndio msingi mkubwa wa kuleta mabadiliko yanayotakiwa katika nchi yetu na ndio maana serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa katika sekta ya elimu.

“Utaona uwekezaji huu haufanyiki tu kwenye kujenga tunaweka vifaa vya kufundishia na kujifunzia. Katika vyuo ambavyo vinashughulika na ufundi wa Kati Serikali imeendelea kupeleka vifaa kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji,” aliongeza Naibu Waziri Ole Nasha

Pia alisema kwa miaka mitatu  mfululizo Serikali imeajiri takribani walimu wapya  elfu 18, na kwamba katika mwaka huu wa fedha serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuajiri walimu wengine wapya lengo ni kuwa na uwiano mzuri kati ya mwalimu na mwanafunzi.

Alitaja eneo lingine ambalo fedha nyingi za umma zinaelekezwa ni ugharamiaji wa Elimu bila malipo ambapo kila mwezi Serikali hutoa zaidi ya bilioni 20 kugharamikia elimu kuanzia elimu ya awali hadi kidato cha nne. Alisema lengo ni kumwezesha mtoto wa kitanzani mwenye umri wa kuanza shule aweze kusoma bila kisingizio cha kukosa ada.
Muonekano wa sasa wa moja ya Jengo la Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Karumo lililojengwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia mradi wa ESPJ. Chuo hicho kipo Kata ya Karumo Wilaya ya Sengerema Jijini Mwanza

Naibu Waziri Ole Nasha alisema kwa upande wa Elimu ya Juu Serikali imepanua wigo wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu ambapo katika mwaka huu inategemea wanafunzi wapya elfu 45 huku fedha za mikopo zikiongezeka kutoka shilingi bilioni 427 za mwaka jana hadi kufikia 450 mwaka huu.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ole Nasha amezitaka Halmashauri za Kwimba, Sengerema na Misungwi kusimamia vizuri fedha zinazokuja katika maeneo yao kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili iweze kukamilika kwa wakati na matokeo yaakisi thamani ya fedha zilizotolewa

 “Mhe. Rais katika jambo ambalo anasisitiza kila siku ni matumizi sahihi ya fedha za miradi ukiona fedha zinakuja fahamu ni kwa sababu serikali imetumia nguvu kubwa katika kukusanya kodi na kuzitafuta fedha hizo zisimamieni vizuri’’alisema Naibu Waziri Ole Nasha.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Juma Sweda, Mkuu wa wilaya ya Kwimba Senyi Nganga na yule wa Sengerema Emmanuel Kipoyo wameahidi kuendelea kusimamia ipasavyo fedha za miradi ya maendeleo zinazoletwa katika Wilaya zao ili ziweze kutimiza lengo na matokeo yaakisi gharama ya fedha zilizotolewa ikiwa ni pamoja na kusimamia elimu ipasavyo katika Wilaya hizo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua majengo ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Sengerema kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema Jijini Mwanza ambacho kimepatiwa fedha na Wizara kwa ajili ya kufanyiwa ukarabati.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni