Ijumaa, 14 Februari 2020

UKWELI KUHUSU VYUO VYA MAENDELEO YA WANANCHI (FDCs)

WAZIRI NDALICHAKO ATAKA USIMAMIZI THABITI WA MIRADI YA ELIMU

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako ametoa rai kwa watendaji wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kusimamia vizuri fedha za  miradi ya Elimu inayotelekezwa katika maeneo yao ili  ikamilike kwa wakati na ubora.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza wakati wa uzinduzi wa Jengo la  Utawala la Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam
Waziri Ndalichako ametoa rai hiyo Jijini Dar es Salaam wakati akizinduzia Jengo la Utawala la Chuo Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE) lililokarabatiwa na kuongeza ukubwa ambapo amesema Serikali imekuwa ikitoa fedha nyingi za Miradi lakini haikamiliki kutokana na usimamizi mbovu hivyo kutaka watendaji hao kusimamia miradi ipasavyo.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizindua Jengo la Utawala la Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam
Amesema Serikali ya Awamu ya Tano imefanya kazi kubwa sana katika kuboresha mazingira ya utoaji elimu  na kwamba kukamilika kwa mradi wa upanuzi wa Jengo la Utawala la Chuo Kishiriki cha DUCE ni sehemu tu ya mambo mengi ambayo Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli na serikali yake imefanya.
Baadhi ya Wanajumuiya ya Chuo Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako wakati wa uzinduzi wa Jengo la Utawala la Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam
Profesa Ndalichako aliongeza kuwa wakati Serikali ikiendelea na maboresho hayo, taasisi za elimu ya juu zinatakiwa kuendelea  kutekeleza wajibu wao ipasavyo ambao  ni kutoa taaluma, kufanya tafiti pamoja na kutoa huduma na ushauri kwa jamii.

“Vyuo Vikuu vimekuwa vikijikita katika utoaji wa taaluma wakati mwingine vinakuwa vikisahau jukumu la kufanya tafiti na ndio maana tunaona idadi ya machapisho imekuwa ikipungua mwaka hadi mwaka. Niwaambie tunapokuwa tunafanyiwa tathmini ya upangaji wa madaraja ya vyuo, sehemu ambayo mara nyingi imekuwa ikituangusha ni sehemu ya tafiti, kwa hiyo nitumie nafasi hii kuzikumbusha Taasisi za elimu ya juu kuendelea kufanya tafiti na tafiti zenyewe ziwe ni zile zinazotoa mchango moja kwa moja katika maendeleo ya nchi,” amesema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanajumuiya wa Chuo Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam mara baada ya  kuzindua Jengo la utawala la chuo hicho,  jijini Dar es Salaam
Katika hatua nyingine Profesa Ndalichako ametoa wito kwa Vyuo vya Elimu ya Juu nchini kutumia vema mapato yao ya ndani yanayotokana na huduma wanazotoa  kama za ushauri na tafiti kwa maendeleo ya Vyuo ikiwa ni pamoja na  kutenga sehemu ya Mapato hayo ndani kugharamia masomo ya watumishi.

“Nakipongeza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kuweza kutumia fedha kutoka kwenye mapato  ya ndani kutoa ufadhili wa masomo kwa watanzania wenye ufaulu wa kiwango cha Juu. Huu ni mchango mkubwa kwa Taifa letu kwani unatoa fursa kwa watanzania ambao wamefaulu vizuri lakini kutokana na sababu mbalimbali wasingeweza kunufaika na mikopo itolewayo na Bodi ya Mikopo,” alisema Waziri Ndalichako.
 
Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Kishiriki cha Dar es Salaam ambae pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi ya DUCE Profesa William Anangisye amemuahidi Waziri Ndalichako kuendelea kusimamia vizuri matumizi ya fedha za Miradi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha jengo lililozinduliwa leo linatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kuwa chachu ya maendeleo ya Chuo hicho.

“Mhe. Waziri nakuahidi kuwa majengo haya yatatunzwa vizuri na kutoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa majukumu ya chuo,” amesema Prof. Anangisye.

Naye Kaimu Rasi wa Chuo Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE), Prof. Stephen Maluka ameishukuru Serikali kwa namna inavyoendelea kuboresha mazingira ya utoaji elimu kwa Taasisi za elimu ya Juu ambapo amesema katika Chuo hicho upanuzi wa Jengo la utawala umeondoa changamoto iliyokuwepo ya ukosefu wa ofisi za watumishi huku akiiomba Serikali kuwapatia fedha kwa ajili ya kusomesha wataalamu wao.

Jumatano, 12 Februari 2020

UFUNGUZI WA MAFUNZO YA MAAFISA BAJETI WA WIZARA NA WA OFISI ZA UTHIBITI UBORA WA SHULE KANDA

Serikali imeweka kipaumbele katika kuwajengea uwezo watendaji wake ili kutimiza majukumu yao kwa ufanisi ikiwa ni pamoja na kuongeza nidhamu katika matumizi ya fedha na usimamizi fanisi wa mali za serikali.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Maafisa Bajeti wa Wizara nawa Ofisi za Uthibiti Ubora wa Shule Kanda mkoani Morogoro
Hayo yamesemwa Mkoani Morogoro na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa Ufunguzi wa Mafunzo ya Maafisa Bajeti wa Wizara na wa Ofisi za Uthibiti Ubora wa Shule Kanda yenye lengo la kuboresha utendaji kazi hususani katika maandalizi ya Bajeti.

Kiongozi huyo amesema utoaji wa mafunzo haya utasaidia kutoa maarifa mapya na stadi zaidi katika utekelezaji wa majukumu ikiwa ni Pamoja na  kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utendaji kazi.

Mkurugenzi wa Idara ya Uthibiti Ubora wa Shule kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Mwl Euphrasia Buchuma akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya Maafisa Bajetu wa Wizara na wa Ofisi za Uthibiti Ubora wa Shule Kanda Mkoani Morogoro

“Mkurugenzi wa Uthibiti Ubora wa shule amenieleza kuwa kulikuwa na changamoto katika uaandaji wa bajeti kwa kuwa haikuwa na uhalisia, natambua mwenye kujua hali halisi kwenye ofisi ya uthibiti ubora ni yule ambaye yuko katika ofisi husika za kanda na wilaya na kwa kuwa  wataalamu wa bajeti wameona kuna mapungufu ndiyo maana tumeitisha mafunzo haya ili katika kupanga bajeti iwe na uhalisia,”alisema Naibu Waziri Ole Nasha
Mwezeshaji kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Pendo Sianga akiwapitisha wajumbe kwenye utaratibu wa kuandaa bajeti wakati wa mafunzo ya bajeti mkoani Morogoro

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ole Nasha amesema Serikali katika kipindi cha miaka minne ya Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano imeweka mkazo katika kuimarisha Uthibiti Ubora wa Shule kwa kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wathibiti Ubora na kuweka mazingira sahihi ya ufanyaji kazi.

Ametaja maboresho yaliyofanyika katika eneo hilo kuwa ni pamoja na  ununuzi wa magari 45 ya wathibiti ubora wa Shule kwa wilaya ambazo hazikuwa na magari Pamoja na Kujenga Ofisi 100 za Wathibiti na kuziwekea samani na vitendea kazi. Aidha Serikali pia imenunua pikipiki 2,894 za Maafisa elimu Kata ili kuimarisha usimamizi wa  shule, pamoja na kuwapatia mafunzo ya kiutendaji wathibiti Ubora wa shule 1,276.
Baadhi ya Washiriki wa mafunzo ya Bajeti Mkoani Morogoro wakifuatilia hotuba ya Ufunguzi ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha
Maboresho mengine ni Kuongeza idadi ya Maafisa Uthibiti Ubora wa shule 400 ngazi ya Wilaya na Kanda pamoja na kuanzisha ofisi mpya 5 za Uthibiti Ubora wa shule katika wilaya mpya za Songwe, Kigamboni, Ubungo, Chalinze na Ushetu ili kurahisisha utoaji huduma za uthibiti Ubora huku serikali ikijipanga kununua magari mengine mapya 65 kwa ajili ya idara hiyo.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Uthibiti Ubora wa Shule Mwl. Euphrasia Buchuma amesema mafunzo haya yanafanyika kutokana na changamoto ambazo zimekuwa zikibainika katika bajeti zinazoandaliwa ikiwa ni pamoja na kueleweshana taratibu za matumizi ya fedha kulingana na vifungu vilivyowekwa.
 
Mafunzo ya kuwajengea uwezo maafisa bajeti wa Wizara na wa Ofisi za Uthibiti Ubora wa shule za Kanda yameanza leo Februari 12, 2020 na yana jumla ya washiriki 70 kutoka Ofisi hizo na Wizara ya Elimu Makao makuu.

KONGAMANO LA KIMATAIFA LA KUUNGANISHA WANATAALUMA NA WADAU WA SEKTA YA U...

WIZARA YAKABIDHI VIFAA VYA TEHAMA NA VITABU KWA VYUO VYA UALIMU VYA SERIKALI 35 KWA AJILI YA KUFUNDISHIA NA KUJIFUNZIA

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekabidhi vifaa vya TEHAMA na vitabu  kwa vyuo vya ualimu vya serikali 35 kwa ajili ya  kufundishia na kujifunzia.




Akikabidhi vifaa hivyo kwa mkuu wa Chuo cha Ualimu Patandi  jijini Arusha Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard  Akwilapo  amewataka wakuu wa vyuo hivyo kuhakikisha vifaa hivyo vinatunzwa na vinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

"Vifaa tunavyovikabidhi leo ni vya gharama kubwa sana wito wangu kwa wakuu wa vyuo wote kuhakikisha wanavitunza vifaa hivi ili viweze tumika kwa muda mrefu na kuwanufaisha hata wanachuo watakaojiunga kwa miaka mingine" amesisitiza Katibu Mkuu.

Amesema pamoja na  kukabidhi vifaa hivyo na kutoa mafunzo kwa wakufunzi wa vyuo vya ualimu lengo kubwa ni kuimarisha na kuboresha mafunzo yanayotolewa kwa walimu tarajali ili wanapomaliza mafunzo yao wawe na mbinu bora
 za ufundishaji ambazo zitasaidia kuinua ubora wa elimu katika shule za msingi na sekondari

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Ave Maria Semakafu amesema utoaji wa vifaa hivyo ni juhudi za  makusudi zinazofanywa na wizara katika kutekeleza azma ya  kuboresha elimu nchini.

Kansela Mkuu, Ushirikiano na Maendeleo kutoka Canada Gwen Waimsley amesema nchi yake itaendelea kusaidia katika kuhakikisha walimu tarajali wanapata mafunzo bora ambayo yataleta tija katika ufundishaji na ujifunzaji katika shule za msingi na sekondari.

Gwen amesema nchi ya Canada inaamini kuwa walimu wanapoandaliwa katika mazingira mazuri ya kupatiwa mafunzo zoezi zima la utoaji elimu katika hatua zote linakuwa limefanikiwa.

Naye Mkuu wa Chuo cha Ualimu Patandi.....  ameishukuru serikali kwa  kufanya mabadiliko makubwa katika vyuo vya ualimu vya serikali ambavyo vimekuwa na mabadiliko ya miundombinu na kupatiwa vifaa vingi vya kufundishia na kujifunzia

Mkuu wa chuo huyo amesema kama watendaji walioaminiwa katika kusimamia vyuo hivyo wana wajibu wa kusimamia vyuo hivyo na kufanya kazi kwa bidii ili kufikia malengo yaliyowekwa kwani mazingira yamekuwa rafiki kwa utendaji na ufundishaji.

Vifaa vilivyokabidhiwa katika vyuo hivyo ni pamoja na kompyuta mpakato 43, kompyuta za mezani 780, mashine za kudurufu 74 vitabu vya masomo ya kufundishia na vitabu vya kitaaluma  26,470 , projectors na vifaa vya kufundishia elimu maalumu.

Jumanne, 11 Februari 2020

Kongamano la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya Utalii na Ukarimu

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiongea wakati wa kufunga Kongamano la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya utaliina ukarimu liliofanyika Jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amesema taasisi za mafunzo na wadau wa sekta ya utalii wanahitajika kufanya kazi kwa pamoja ili kutatua changamto zilizopo ikiwemo nguvu kazi yenye weledi na ufanisi wa kutosha  katika tasnia hiyo.

Naibu Waziri Ole Nasha ameyasema hayo Jijini Dar es Salaam wakati wa kufunga Kongamano la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya Utalii na Ukarimu ambapo amesema ushindani katika soko ni mkubwa hivyo kunahitajika maandalizi mazuri ya rasilimali watu ili kuweza kushindana katika soko la dunia.



Mmoja wa washiriki wa   Kongamano la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya utalii akipokea cheti cha ushiriki kutoka kwa Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa kufunga kongamano hilo Jijini Dar es Salaam.

Amesema Utalii ni moja ya Sekta inayolipatia  Taifa  fedha za kigeni akitolea mfano mwaka jana 2019 nchi ilipata fedha za kigeni dola  milioni 2.4 kutokana na utalii hivyo kukiwa na nguvu kazi yenye weledi na ufanisi wa kutosha nchi itaneemeka kupitia utalii.

“Hakika tunahitaji kuandaa vizuri rasilimali watu, nchi jirani zimepiga hatua kwenye kuvutia watalii sio kwamba wana vivutio vingi kuliko sisi ni kutokana na  pamoja na mambo mengine kuwa na nguvu kazi yenye weledi ndio maana kama Taifa tunawekeza katika kutayarisha vijana ili kuwa na nguvu kazi yenye weledi katika sekta ya utalii," amesema Naibu Waziri Ole Nasha.
Mmoja wa washiriki wa kongamano  la Kimataifa la kuunganisha wanataaluma na wadau wa sekta ya utalii  na Ukarimu Zera Mwanga kutoka Chuo cha Taifa cha Utalii cha Jijini Dar es Salaam akionesha cheti cha ushiriki mara baada ya kukabidhiwa.
Kiongozi huyo aliongeza kuwa kwa sasa Taifa letu linatoa kipaumbele katika kuimarisha viwanda ili kuleta mabadiliko ya kiuchumi ikiwa ni pamoja na kuandaa nguvu kazi, hivyo ni vizuri kukawa na mfumo wa mafunzo pacha kati ya Taasisi za mafunzo na wamiliki wa viwanda.

“Ninawiwa kusema kuwa kongamano hili limekuja kwa wakati muafaka sana na Wizara yangu itayachukua kwa uzito mapendekezo yote yaliyotolewa ukizingatia kuwa kuimarisha muunganiko kati ya wanatasnia na wanataaluma ni moja ya vipaumbele katika wizara yangu ili kuhakikisha tunazalisha wahitimu bora wanaokidhi mahitaji ya soko,” aliongeza Naibu Waziri Ole Nasha. 

Naibu Waziri Ole Nasha amekipongeza chuo cha Taifa cha Utalii na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kuandaa mkutano wa kuwaunganisha wakufunzi na watoe huduma hiyo walio katika biashara ya Utalii kwani kwa pamoja wanaweza kutatua changamoto zilizopo.

Naye Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Utalii, Dkt. Shogo Mlozi amesema kwa kushirikiana na vyuo vingine vinavyotoa mafunzo ya utalii wataendelea kuimarisha mpango wa utoaji mafunzo  kwa kufanya kazi karibu na watoa huduma ili kupata nguvu kazi yenye weledi na ujuzi. 
Baadhi washiriki wa kongamano  la Kimataifa la kuunganisha wanataalumana wadau wa sekta ya Utalii na Ukarimu wakifuatlia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimi, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa kufunga kongamano hilo jijini Dar es Salaam
Kwa upande wake mshiriki wa kongamano hilo kutoka VETA makao makuu,  Happiness Salema amesema ni vizuri kukawa na makongamano ya aina hii kwa kuwa yanawaleta pamoja watoa mafunzo na wamiliki wa viwanda, jambo ambalo linasaidia kuona changamoto zilizopo na kuweka mkakati kwani nchi zilizoendelea zinatumia mfumo huu katika kutoa mafunzo.

"Soko la hotelia na utalii liwe tayari kupokea mfumo wa mafunzo pacha hali kadhalika kuwa tayari kutoa nafasi kwa ajili ya walimu kupata ujuzi kwani kwa kufanya hivyo nchi itakuwa ya kwanza kuongoza kwenye sekta ya utalii na ukarimu," amesema Salema.

Kongamano la kimataifa la kuunganisha sekta ya Utalii na Ukarimu katika nchi zinazoendelea limefanyika kwa siku mbili Jijini Dar es Salaam na limewakutanisha  wadau  na wanataaluma katika sekta ya Utalii na Ukarimu kutoka nchi zinazoendelea.

WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA KUJENGA KUJENGA BWALO KATIKA SHULE YA MRISHO GAMBO ILIYOPO MKOANI ARUSHA



Akizungumza mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa shule hiyo, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo  amesema Wizara itajenga bwalo la chakula ili kuwezesha wanafunzi wa shule hiyo kuwa na sehemu nzuri na salama ya kupatia chakula watakapokuwa wakiishi katika mabweni yatakayojengwa na wizara.

"Nimeambiwa wanafunzi wa shule hii wanatoka maeneo ya mbali, Wizara ilishaahidi kujenga mabweni mawili sasa tutajenga na bwalo," amesema Dkt. Akwilapo.

 Aidha, Dkt. Akwilapo amesema  serikali ina wajibu wa kuhakikisha wanafunzi wanasoma  katika
 mazingira salama na yenye miundombinu salama.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo amesema shule hiyo imejengwa baada ya kupokea maombi kutoka kwa  wakazi wa Olasite baada shule yao kuzidiwa na wingi wa wanafunzi.

"Baada ya kupokea maombi kutoka kwa wakazi wa hapa  na kuona kweli kuna shida katika shule hii ya Olasite ndipo tukaanza kutafuta wadau mbalimbali ambao walijitokeza na kusaidia uanzishwaji wa ujenzi wa shule hiyo," amesema Gambo.

Mkuu wa shule hiyo, Fedelis Michael amesema mazingira ya wanafunzi kusoma mbali sana na shule ni changamoto kwao kwani njiani wanakutana na mambo mengi ambayo yanaweza kuwasababishia kushindwa kusoma vizuri.

Jumatatu, 10 Februari 2020

CANADA YATOA ZAIDI YA BILIONI 90 KWA AJILI YA KUBORESHA ELIMU YA UALIMU

Serikali ya Canada imetoa zaidi ya bilioni 90 kwa Tanzania zitakazotumika kuboresha elimu ya ualimu nchini.

Hayo yamesemwa Jijini Arusha na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo  wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kupitia na kutathmini utekelezaji wa Mradi wa Kuendeleza Elimu nchini (TESP) ambapo amesema mradi huo pia umewezesha kuinua kiwango cha ubora wa elimu katika shule za msingi na sekondari kwa kuzalisha rasilimali watu yenye ubora.
.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akizungumza na wadau wa Elimu ya Ualimu (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kupitia na kutathimini Mradi wa Kuendeleza Elimu ya Ualimu (TESP) Jijini Arusha
Dkt. Akwilapo amesema Canada kupitia TESP imetoa fedha hizo ambazo zimetumika katika kuvijenga upya baadhi ya vyuo vya ualimu, kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia  pamoja na kutoa mafunzo kazini kwa  walimu.

Kansela Mkuu, Ushirikiano na Maendeleo kutoka Canada Gwen Walmsely akizungumza na wadau wa Elimu ya Ualimu jijini Arusha
Kiongozi huyo amesema kuwa Ushirikiano wa Tanzania na Canada unalenga kuongeza uwezo wa vyuo vya ualimu kufundisha walimu waliobobea watakaofundisha vizuri katika shule mbalimbali.

“Tunatoa shukrani nyingi sana kwa serikali ya Canada na Kitengo chao cha Global Affairs ambacho kinasimamia mradi huu, mafanikio makubwa yamepatikana kupitia mradi huu na matokeo yameshaanza kuonekana," amesisitiza Katibu Mkuu Akwilapo.

Dkt. Akwilapo amesema mafanikio  ya mradi huo yameanza kuonekana ambapo walimu wameongeza uwezo katika ufundishaji na matumizi ya TEHAMA katika kufundisha.

Kansela Mkuu, Ushirikiano na Maendeleo ​kutoka Canada Gwen Walmsley amesema kuwa Canada itaendelea kutoa fedha zaidi katika kuboresha sekta ya elimu nchini na mradi huo ni moja kati ya juhudi wanazozifanya katika kuunga mkono serikali ya Tanzania katika jitihada za  kuboresha elimu.

Gwen ameipongeza Tanzania kwa kufanya Sekta ya Elimu kipaumbele ili  kuhakikisha watoto wote wanapata elimu, suala ambalo limewezesha zaidi ya watoto milioni 10.6 kujiunga na elimu ya msingi na sekondari

Mratibu wa Mradi wa kuendeleza Elimu​ ya Ualimu TESP kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Ignas Chonya amesema kuwa mradi huo umewawezesha walimu kuboresha mbinu za ufundishaji kupitia Tehama ambapo vyuo 35 vya ualimu vimeanganishwa na mfumo huo na wanatarajia kuunganishwa na mkongo wa Taifa.

Jumamosi, 8 Februari 2020

MKUTANO WA WATUMISHI WA WIZARA WALIOKO MAKAO MAKUU


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo amesema utumishi wa umma una sheria, kanuni, taratibu, maadili na miiko ya kiutendaji ambayo kila mtumishi anapaswa kuielewa na kuzingatia katika utendaji kazi.
 
Katibu Mkuu Akwilapo amesema hayo wakati wa Mkutano  wa Wafanyakazi wa kutathmini utendaji wa Wizara katika kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba 2019 ambapo amesema ni vizuri kila mtumishi akazingatia taratibu hizo ili kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Amesema pamoja na kuzingatia sheria hizo ni vizuri tukafanya kazi kwa kushirikiana na kuelekezana ili kupata matokeo chanya katika utekelezaji wa majukumu.

Kiongozi huyo amepongeza watumishi wa Wizara hiyo kwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo ili kufikia malengo makubwa ya Wizara ambayo ni kutoa Elimu bora nchini.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. AveMaria Semakafu amesema ni vizuri watumishi wakaendeleza kasi liyopo sasa ya utendaji huku wakizingatia utendaji wenye viwango ili sekta ya Elimu iendelee kufanya vizuri.

Akizungumza kwa niaba ya Watumishi wa Wizara Bwana Nicholaus Moshi ameupongeza Uongozi wa Wizara kwa namna unavyoweka mazingira wezeshi ya utoaji Elimu kwa  kujenga na kukarabati miundombinu ya elimu, kununua vifaa vya kufundishia na kujifunzia, kuhakikisha uwepo wa vitendea kazi pamoja na ujenzi wa ofisi zikiwemo za Wathibiti Ubora wa shule na ukarabati na upanuzi wa  Vyuo  ya Ualimu.

Alhamisi, 6 Februari 2020

SERIKALI KUJENGA SHULE ZA WANAFUNZI WENYE MAHITAJI MAALUM KILA MKOA

Serikali imesema itaendelea na mpango mkakati wa kutekeleza elimu bila malipo pamoja na kutoa vipaumbele kwa watu wenye ulemavu kupata elimu iliyo bora.

Hayo yameelezwa jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu wakati wa ufungaji wa mafunzo ya TEHAMA na Teknolojia Saidizi kwa wakufunzi na walimu wa Sekondari wenye mahitaji maalum.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akiongea wakati wa ufungaji wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi kwa Wakufunzi na Walimu wa Sekondari wenye mahitaji maalumu jijini Dar es Salaam.
Dk. Semakafu amesema  serikali imejipanga kuhakikisha walimu  na wanafunzi wanapata elimu ya Tehama, elimu jumuishi sambamba na kujenga shule zao maalum katika kila mkoa ambapo kwa sasa wameanza na mkoa wa Katavi.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akitoa maelekezo kwa mmoja wa washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi OUT, jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo awali ilielezwa kuwa tayari serikali imetumia kiasi cha shilingi bilioni 5.9 kwa ajili ya kununua na kusambaza vifaa maalum vya kielimu saidizi katika shule za msingi na sekondari zinazopokea wanafunzi wenye mahitaji maalum nchini.

“Hii kazi pia si ndogo, napenda kwa namna ya kipekee kabisa kutumia nafasi hii kuushukuru Uongozi wa Chuo Kikuu Huria kwa kukubali kuendesha mafunzo haya hapa chuoni na kutoa wawezeshaji, vifaa pamoja na miundombinu mingine kwa ajili ya kufanikisha mafunzo haya muhimu,’’ amesema Dk. Semakafu.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi akiwa katika mafunzo yaliyofanyika Chuo Kikuu Huria jijini Dar es Salaam.  Kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu.
Aliongeza kuwa mafunzo waliyoyapata ni muhimu kwani yatawasaidia katika matumizi ya TEHAMA kwenye  ufundishaji na ujifunzaji, kutafuta rejea mbalimbali za kielektroniki kwenye mitandao na kutumia teknolojia saidizi zinazowezesha matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.

Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo, Mwalimu wa shule ya sekondari ya Binti Mussa iliyopo Kiwalani jijini Dar es Salaam, Anna Mbogo alisema wanaishukuru kwa  dhati  Wizara ya Elimu kwa kuona umuhimu wa kutoa  mafunzo kwa walimu wenye mahitaji maalum.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya Tehama na Teknolojia Saidizi kwa Wakufunzi na Walimu wa sekondari wenye mahitaji maalumu wakifuatilia hotuba ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu (hayupo pichani)  wakati wa kufunga mafunzo hayo jijini Dar es Salaam.
“Mafunzo haya  yalilenga kutujengea uwezo sisi walimu kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia ya sasa, pia tunaushukuru uongozi wa OUT chini ya serikali ya awamu ya tano kuonesha bayana nia ya kuwasaidia walimu wenye mahitaji maalum na kuwathamini watu wenye ulemavu kwa kuajiri watu wenye ulemavu,’’ amesema Mwalimu Anna.

MAKISATU 2020 KUENDELEA KUIBUA WABUNIFU

Serikali imesema inatambua umuhimu na mchango wa ubunifu na teknolojia katika kurahisisha na kuongeza ufanisi  katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma kuhusu kuanza kwa Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) 2020, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amesema  mashindano hayo ni moja ya mikakati ya Serikali ya kuibua, kutambua na kuendeleza ubunifu na ugunduzi unaofanywa na watanzania.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Mkutano mara baada ya kuzungumza na Waandishi wa habari jijini Dodoma.  Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Leonard Akwilapo na kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Sylvia Lupembe.

"Lengo kubwa la MAKISATU pamoja na kukuza na kusaidia kubiasharisha, yanatoa fursa kwa wabunifu na wagunduzi wa teknolojia mbalimbali kujitangaza na kutangaza kwa wadau ubunifu unaozalishwa," amesisitiza Ole Nasha.
Mwakilishi wa Benki ya CRDB, Prosper Nambaya akizungumza wakati wa Mkutano wa Waandishi wa habari kuzungumzia kuanza kwa mashindano ya MAKISATU, 2020 jijini Dodoma.
Ole Nasha amesema MAKISATU inawalenga wabunifu kutoka makundi ya shule za msingi, sekondari, vyuo vya ufundi stadi, vyuo vya kati, vyuo vikuu, Taasisi za utafiti na Mfumo usio rasmi.

Baadhi ya washiriki waliohudhuria Mkutano wa kuzungumzia kuanza kwa Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknonojia na Ubunifu (MAKISATU) 2020 jijini Dodoma, wakimsikiza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani) wakati akizungumza na Waandishi wa habari.

Aliongeza kuwa kupitia MAKISATU 2019 Serikali imewaibua na kuwatambua wabunifu wachanga zaidi ya 415 huku wabunifu 60 mahiri wakiendelezwa ili ubunifu wao ufikie hatua ya kubiasharishwa.


Kiongozi huyo ametoa wito kwa watanzania wenye ubunifu mbalimbali kushiriki katika mashindani hayo na amewashukuru Benki ya CRDB kwa kukubali kufadhili mashindano hayo.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Wateja Wakubwa kutoka CRDB, Prosper Nambaya amesema Benki hiyo imeamua kuwa na ushirikiano endelevu na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili kusaidia kukuza ubunifu unaozalishwa nchini kutokana na kuwepo kwa watu wengi wenye mawazo ya kibunifu yanayopaswa kuendelezwa.