Jumatano, 18 Oktoba 2017

Waziri Ndalichako azindua ufadhili wa wanafunzi unaotolewa na Barclays


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amewataka wanafunzi kutumia mitandao ya kijamii kwa ajili ya kupata taarifa zitakazowasaidia kutekeleza fursa mbalimbali za kujiletea Maendeleo.
Waziri Ndalichako ameyasema hayo leo  wakati wa uzinduzi wa Twende kazi na Balozi mwanafunzi unaohusu ufadhili wa masomo kwa wanafunzi  23 wa shahada ya kwanza ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam na kusisitiza kuwa taasisi nyingine ziige mfano huo wa Barclays wa kufadhili wanafunzi.

Pia Barclays imewasaidia vijana 32 Kati ya 200 kuwatafutia ofisi ili kufanya kazi kwa vitendo kwa ajili ya kuwajengea uwezo wa kuwa tayari kwa kazi.

Uzinduzi huo pia umehudhuriwa na Mkurugenzi wa Elimu ya Juu, Profesa Sylivia Temu.



Ijumaa, 13 Oktoba 2017

Waziri: Ndalichako: Shule ya nyasi zitabaki kuwa historia

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako leo amekagua na kufungua ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule ya msingi kilole, Matondoro,  na Kilimani na kuweka jiwe la msingi bweni la wasichana katika shule ya Sekondari Semkiwa  Wilayani Korogwe Mkoani Tanga.

Akizungumza Mara baada ya kukagua utekelezaji wa miradi hiyo Waziri Ndalichako amesema  suala la nchi kuwa na shule au vyumba vya madarasa vya nyasi litabaki kuwa historia kwa kuwa serikali ya awamu ya Tano inahitaji wanafunzi wapate Elimu bora inayoenda sambamba na uboreshaji wa miundombinu na hicho ndicho kinachofanyika hivi sasa.

Akizindua bweni moja la wasichana katika shule ya Sekondari Semkiwa waziri Ndalichako ameahidi kutoa kiasi cha shilingi milioni kumi kwa ajili ya kununulia vitanda na magodoro ili bweni hilo lianze  kutumika mara moja.

Pia amewataka watanzania kwa ujumla kuendelea kumuunga mkono Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli kwa namna anavyojitoa  katika kuwatumikia Wananchi wanyonge kwa lengo la kuliletea Taifa Maendeleo.

Ujenzi wa vyumba hivyo vya madarasa,na  vyoo umetekelezwa  na Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia kupitia mradi wa Lipa kulingana na matokeo, (EP4R).




TANGAZO


Jumatano, 11 Oktoba 2017

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa Dkt. Hussein Mwinyi wampokea Mtukufu Agha Khan


Mtukufu Aga khan muda mfupi Mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa jijini Dar es Salama na amepokelewa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako pamoja na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa Dkt. Hussein Mwinyi.



Mtukufu Aga Khan akikagua gwaride lililoandaliwa kwa ajili yake muda mfupi  baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa jijini Dar es salaam.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolonia Profesa Joyce Ndalichako, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa Dkt. Hussein Mwinyi wakiwa katika picha ya pamoja  na Mtukufu Aga Khan ambaye amewasili leo.




Jumanne, 10 Oktoba 2017

Mradi wa TEHAMA wazinduliwa Mkoani Pwani


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo amezindua mradi wenye thamani ya  zaidi ya shilingi bilioni 4 wa ujifunzaji na ufundiashaji wa TEHAMA kwa shule za Sekondari.
Akizindua mradi huo mkoani Pwani hii leo Dkt. Akwilapo amsema Serikali inahitaji kuona mradi huu unakuwa  endelevu na usiishie katika mkoa wa Pwani pekee bali usambae kwa nchi nzima.
Pia amewataka waratibu wa mradi huo - gesci -  kuhakikisha mpango huu unafanikiwa kwa kushirikisha  wadau wote wa Elimu ili mradi  ufanikiwe.
Dkt. Akwilapo amesema TEHAMA ni nyenzo muhimu katika ulimwengu wa mawasiliano, na kwa sasa ndiyo nyenzo kuu ya utoaji na usambazaji wa taarifa kwa umma.
Katibu Mkuu Akwilapo amewataka wale wote wenye miradi au mipango ya namna hiyo wawasiliane na wizara ili miradi yao iweze kuratibiwa na  kutekelezwa kwa taratibu za Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Mradi huo unatekelezwa katika baadhi ya nchi za Afrika ikiwemo Tanzania, Kenya, na Cotedvoire





Jumatatu, 9 Oktoba 2017

VIONGOZI WA WIZARA YA ELIMU,SAYANSI NA TEKNOLOJIA WAAHIDI KUFANYA KAZI KWA USHIRIKIANO


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema kuwa kitendo cha Rais  John Magufuli kumbakisha kwenye Wizara hiyo ni sawa na kumchagua upya,  hivyo ameahidi kufanya kazi kwa bidii.

Waziri Ndalichako amesema hayo wakati akimkaribisha Naibu waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha ambaye ameapishwa leo kuitumikia Wizara  hiyo.
 
Wakati akizungunza na Watumishi wa Wizara hiyo Naibu Waziri  Ole Nasha amesema  katika utumishi wake anaamini katika mambo manne ambayo ni uadilifu na uaminifu,  kufanya kazi kwa bidii, ubunifu na ushirikiano ili kutimiza malengo ya Kitaifa.

 Ole Nasha amesema hayo muda mfupi baada ya kupokelwa na watumishi wa Wizara hiyo huku akiahidi kutoa ushirikiano katika kuendeleza Sekta ya Elimu.




Alhamisi, 5 Oktoba 2017

Waziri Ndalichako azindua Bodi ya Wakurugenzi HESLB na Baraza la TET

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknnolojia Prof. Joyce Ndalichako amelitaka  Baraza la Taasisi ya Elimu Tanzania na Bodi ya wakurugenzi ya Bodi ya mikopo ya Wanafunzi  wa elimu ya juu kufanya kazi kwa kufuata kanuni, sheria na taratibu za kazi.

Waziri Ndalichako ameyasema hayo leo jijini Dar es salaam wakati wa uzinduzi wa bodi hizo ambapo amezitaka pia kuhakiksha zinarudisha hadhi ya Taasisi  za serikali wanazozisimamia katika kutoa huduma kwa wananchi kwa kuweka miongozo ya utendaji kazi na kuhakikisha wanaisimamia miongozo hiyo ili kuleta ufanisi katika kazi.

Ndalichako amezitaka bodi hizo kuhakikisha zinatembea katika ahadi za Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Joseph Magufuli za kuhakikisha zinawasaidia wanyonge kupata Elimu bora.

Waziri Ndalichacho amelitaka Baraza la Taasisi ya Elimu Tanzania kuhakikisha vitabu vyote vyenye makosa vinarekebishwa na kwamba bodi ijiridhishe na mfumo na utaratibu utakaotumika katika kuvirekebisha vitabu hivyo.

Baraza hili ambalo litahudumu kwa miaka mine (4) kuanzaia septemba 2017 hadi septemba 2021 limetakiwa pia kusimamia Kitengo cha Mawasiliano kwa Umma vizuri kwa sababu kumekuwa na upotoshaji kuhusiana na Taasisi lakini pia amewataka kuhakikisha kunakuwa na vipindi vya kuelimisha namna Taasisi inavyotekeleza majukumu yake. 


Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Taasisi ya Elimu Tanzania Profesa Bernadetta Kilian amesema atahakikisha Taasisi inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria na kwamba maelekezo yote yaliyotolewa yatafanyiwa kazi ili kukidhi matarajio ya watanzania.