Ijumaa, 3 Agosti 2018

SERIKALI KUONGEZA RASLIMALI WATU WENYE UJUZI STAHIKI KATIKA UCHUMI WA VIWANDA

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amesema nchi inahitaji rasilimali watu yenye ufahamu na ujuzi stahiki katika kujenga uchumi wa viwanda.

Akizungumza katika ufunguzi wa kongamano na maonesho ya Wahandisi wanawake wa Taasisi ya Wahandisi Jijini Dar es Salaam Ndalichako amesema Wizara yake imeweka mikakati mbalimbali ili kuhakikisha nchi inakuwa na rasilimali watu ya kutosha, wenye ujuzi utakaowawezesha kuchangia maendeleo ya Taifa.
 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wa washiriki wa Kongamano na Maonesho ya Wahandisi Wanawake wa Taasisi ya Wahandisi iliyofanyika Jijini Dar es Salaam. Amesisitiza Wahandisi hao kuweka katika vitendo tafiti zao ili kuwasaidia wananchi katika kutatua changamoto.


“Tunao mradi wa Mkakati wa Kukuza Staadi za Kazi (ESPJ unaotekeleza Mkakati wa Kujenga Ufahamu na Ujuzi katika maeneo muhimu ya kiuchumi kwa Taifa, miongoni mwa maeneo hayo ni kilimo na uongezaji wa thamani ya mazao ya kilimo; viwanda, usafirishaji, Tehama, nishati, ujenzi na maeneo ya utalii na huduma ambayo uhandisi una mchago mkubwa.” Amesisitiza Ndalichako

Aametoa wito kwa wahandisi hao kuhakikisha wanafanya jitihada zaidi ya kutafuta njia za kuendeleza matokeo ya tafiti wanazofanya na kuziweka katika vitendo ili ziweze kuchangia ipasavyo ukuaji wa sekta ya viwanda nchini. 
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akitoa zawadi kwa Mhandisi Mama Kinasha ambaye ni miongoni wa wahandisi wa wa kwanza kusajiliwa na Taasisi ya Waandisi wakati wa ufunguzi wa Kongamano na Maonesho ya Wahandisi Wanawake wa Taasisi ya Wahandisi iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

Kwa upande wake Kaimu Msajili wa Wahandisi Patrick Balozi amesema katika kufanikisha azma ya kuwa na  uchumi wa viwanda ni muhimu kama Taifa kuongeza idadi ya Udahili kwa wanaunzi wa fani za uhandisi ikiwa ni pamoja na kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia yatakayowavutia wanafunzi kupenda masomo ya sayansi

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisikiliza maelezo kutoka kwa mmoja wa washiriki wa maonesho ya ubunifu katika toa ufunguzi wa Kongamano na Maonesho ya Wahandisi Wanawake wa Taasisi ya Wahandisi iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.

WAZIRI NDALICHAKO AWATAKA WALIMU KUHAMASISHA WANAFUNZI KUSHIRIKI MAONESHO YA UBUNIFU


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako amewataka walimu wa shule za Sekondari kuwahamisha na kuwasaidia wanafunzi kuandaa bunifu zao  ili waweze kushiriki katika maonesho  mbalimbali ya sayansi, teknolojia na ubunifu yanayofanyika nchini.

Akizungumza katika sherehe za utoaji wa zawadi kwa washindi wabunifu walioshiriki katika Monesho ya nane ya taasisi ya Wanasayansi Chipukizi (YST) Jijini Dar es Salaam Waziri Ndalichako amesema ushiriki wa wanafunzi katika maonesho hayo utawasaidia kuinua vipaji vyao na kupenda masomo ya sayansi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikabidhi zawadi kwa washindi wa maonesho ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kutoka Shule ya Sekondari Msalato. Waziri Ndalichako  amewahimiza wanafunzi nchini kushiriki katika maonesho mbalimbali ya namna hiyo ili kukuza vipaji vyao.

Ndalichako amesema anatambua kuwa maonesho hayo yamesaidia mamia ya wanafunzi wa shule za sekondari nchini kuonyesha bunifu zao ambazo zimewawezesha  kuendelea kutafuta  maarifa ya kisayansi yatakayosaidia nchi kufikia  uchumi wa viwanda.

Waziri Ndalichako amesema Wizara yake kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia COSTECH) itaendelea kushirikiana na taasisi hiyo kuangalia namna bora ya kuinua vipaji na kuboresha tatifi zinazofanywa na wanafunzi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akimpongeza mmoja wa washindi wa kwanza wa bunifu zilizoonyesho katika maonesho ya Sayansi , Teknolojia na Ubunifu kutoka Shule ya Sekondari Msalato.

Katika kipindi cha miaka 7 iliyopita, Taasisi hiyo imeweesha zaidi wanafunzi elfu tano (5,000) kushiriki katika maonesho ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu pamoja na kutoa mafunzo kwa walimu zaidi ya 1000 wa shule za sekondari ya namna ya kusaidia na kuboresha tafiti zinazofanywa na wanafunzi.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akishangilia na kufurahia pamoja na wanafunzi walioshinda zawadi mbalimbali katika maonesho ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu yaliyoshirikisha shule mbalimbali nchini.


Alhamisi, 2 Agosti 2018

NDALICHAKO: ANDAENI WANAFUNZI WENYE UJUZI NA UMAHIRI


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.  Joyce Ndalichako amekiagiza Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kuhakikisha kinaandaa wanafunzi mahiri na wenye ujuzi utakaowawezesha kuchangia katika uchumi wa Taifa.

Ndalichako ametoa agizo hilo wakati wa uzinduzi wa hosteli ya wanafunzi, uliofanyika katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akizungumza na watendaji pamoja na wanafunzi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (hawapo pichani) wakati wa kuzindua  hosteli ya wanafunzi yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 720 kwa mara moja.

 Amesema kwa kufanya hivyo mtakuwa mnatekeleza Dira ya Elimu ambayo inataka Taifa kuwa na Mtanzania aliyeelimika na mwenye maarifa, stadi, umahiri, uwezo na mitazamo chanya ili kuweza kuchangia katika maendeleo ya Taifa.

 Waziri Ndalichako ameupongeza uongozi wa chuo hicho kwa kuingiza masomo ya uongozi, maadili na uzalendo katika mitaala ya ngazi zote za kitaaluma kwa kuwa ni muhimu katika kuwajengea vijana uzalendo, moyo wa kujituma na kulipenda Taifa.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akizindua hosteli katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere na kuwataka wanafunzi wa Chuo hicho kutunza miundombinu hiyo ili iweze kuwasaidia wanafunzi wengine watakaojiunga na Chuo hicho.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo Profesa Shadrack Mwakalila amesema hosteli hiyo ni ya ghorofa 5 na ina uwezo kuchukua wanafunzi 720 kwa mara moja hivyo kupunguza tatizo la malazi ya wanafunzi katika chuo hicho.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akikagua baadhi ya miundombinu katika hosteli mpya aliyoizindua katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere. 

Jumatatu, 30 Julai 2018

WATHIBITI UBORA WA SHULE NCHINI WAPATIWA MAFUNZO YA MFUMO MPYA WA UKAGUZI WA SHULE


Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeanza kutoa mafunzo kwa wathibiti ubora wa shule kote nchini ya namna ya kutekeleza mfumo mpya wa Uthibiti Ubora wa Elimu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Jijini Dodoma Mthibiti Mkuu wa Shule kutoka Wizara hiyo Euphrasia Buchuma amesema mfumo huo unaondoa mfumo ambao wathibiti ubora wamekuwa wakitazamwa kama polisi pindi wanapofika shuleni na kuwa watu ambao wanatakiwa kutoa msaada katika shule.

Buchuma amesema mfumo huo mpya unashirikisha jamii nzima ya shule Viongozi wote, Wazazi, Kamati za Shule, Bodi ya shule na walimu ambao wanapaswa kufahamu Mthibiti Ubora wa Shule anapoingia katika Shule anafanya nini katika shule hiyo na taarifa za ukaguzi ni lazima ziwafikie viongozi wote wenye mamlaka na kutoa maamuzi.

Amesema kwa kuwa mfumo huu ni shirikishi unaleta uwazi zaidi na kuondoa usiri ambao ulikuwapo katika mfumo uliokuwa ukitumika zamani katika kukagua shule ambao uliitaji usiri kuanzia unapokagua shule uandikaji wa ripoti na hata uwasilishaji wa taarifa ya ukaguzi.

Mthibiti Mkuu wa Shule kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Euphrasia Buchuma akiongea na Wathibiti Ubora wa Shule wakati wa ufunguzi wa mafunzo eelekezi ya namna ya kutumia mfumo mpya wa ukaguzi wa Shule Jijini Dodoma.

Amewataka wathibiti ubora wa shule kushiriki mafunzo hayo kikamilifu kwa kuwa wana dhamana kubwa ya Elimu na kwamba kila mmoja kwa nafasi yake atambue wajibu wake, abadili mtizamo, afanye kazi kwani kunahitajika mabadiliko makubwa katika kuhakikisha Elimu ya nchi hii inatolewa kama inavyopaswa kutolewa.

“Tumekuwa tukinyooshewa vidole sana kwamba hatufanyi kazi na ni kwa sababu matokeo yanaonekana kama hatupo kumbe tupo, hatuonekani katika utendaji kazi na ndio maana kila panapotokea tatizo tunaonekana hatupo na hatufanyi kazi tubadilike tufanye kazi kwa moyo, bidii na weledi,” alisisitiza Buchuma
Baadhi ya Wathibiti Ubora wa Shule wakifuatilia hotuba ya Mthibiti Mkuu wa Shule kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Euphrasia Buchuma wakati wa ufunguzi wa mafunzo elekeze kwa Wathibiti Ubora wa Shule ya nama ya kutumia mfumo mpya wa ukaguzi wa Shule.
                                    
Katika hatua nyngine Buchuma amewataka wathibiti ubora wa shule mara baada ya mafunzo hayo kukamilika, wahakikishe wanakagua Shule zote za Sekondari ambazo ni Kongwe kwani zinaonesha kutofanya vizuri katika miaka ya hivi karibuni.

“leo ukienda katika shule nyingi ukiukwaji wa sheria za Shule ni mkubwa lakini na sisi tupo na hatusemi tunasema hatuhusiki, kimsingi sisi ndio wasimamia Sera, Miongozo, taratibu na kanuni zote za uendeshaji wa shule kuanzia ngazi ya Shule za Awali, Msingi, Sekondari na Vyuo vya Ualimuhivyo tukafanye kazi,” aliongeza Buchuma

Mafunzo elekezi ya namna ya kufanya ukaguzi kwa mfumo mpya wa uthibiti ubora wa Shule yanafanyika kwa siku nne kuanzia Julai 30, mwaka huu nchi nzima.

Jumamosi, 21 Julai 2018

OLE NASHA AZITAKA TAASISI ZA ELIMU YA JUU KUZINGATIA UBORA WA MAFUNZO WANAYAYOTOA


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha  amezitaka Taasisi za Elimu ya Juu kuzingatia suala la ubora wa mafunzo wanayoyatoa katika programu zao ili kupata wahitimu wenye ujuzi unaotakiwa kwenye uchumi wa viwanda.

Naibu Waziri Ole Nasha amesema hayo Jijini Dar es Salaam wakati wa kufunga   Maonesho ya 13 ya Elimu ya Juu ambapo amesema Serikali ina mategemeo makubwa ya kupata rasilimali watu bora itakayofanya kazi katika viwanda hivyo suala la ubora wa mafunzo linahitaji kupewa kipaumbele.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha akizungumza na wanashiriki (Hawapo pichani) katika maonesho ya kumi na tatu ya Elimu ya Juu wakati wa kufunga wa maonesho hayo katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es alaam.

“Tunataka mzalishe wahitimu wanaoonekana wamepata Elimu bora na si bora Elimu ambao wataweza kufanya kazi kulingana na mahitaji na matarajio ya taifa letu lakini pia watakaokidhi vigezo na matarajio ya wadau mbalimbali,” Alisisitiza Naibu Waziri Ole Nasha.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha akisikiliza ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali ya elimu  kutoka kwa mmoja wa washiriki wa maonesho ya kumi na tatu ya Elimu ya Juu yanayofanyika jijini Dar es Salaam.

Alisema wizara yake itaendelea kusimamia na kufuatilia kwa karibu zaidi suala la ubora wa Elimu katika ngazi zote na kuzitaka Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU) na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) kuhakikisha inafuatiali vyuo kwa karibu ili kuhakikisha wanafuata miongozo iliyopo na kwamba Serikali haitavumilia taasisi au mtu yeyote anayejaribu kukiuka miongozo hiyo kwa sababu yoyote ile.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha akikabidhi cheti cha ushiriki kwa mmoja wa wadau wa Elimu ya Juu walioshiriki maonesho ya kumi na tatu ya Elimu ya Juu yanayofanyika jijini Dar es Salaam.
Maonesho ya Elimu ya Juu yamehitimishwa leo na yalikuwa na kauli mbiu ELIMU YA JUU BORA KWA MAPINDUZI YA VIWANDA


Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe Prof. Lughano Kusiluka akijadiliana masula mbalimbali kuhusu Elimu na baadhi ya washiriki wa maonesho ya Elimu Juu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia yaliyofanyika jijini Dar es Salaam 

Alhamisi, 19 Julai 2018

WIZARA YA ELIMU YAKABIDHI MAGARI 47 KWA WADHIBITI UBORA WA SHULE


Wathibiti Ubora wa Shule nchini wametakiwa kufanya ufuatiliaji wa karibu wa taaluma shuleni kwani matokeo bora ya ujifunzaji yanahitaji usimamizi na tathmini ya mara kwa mara.

Hayo yameelezwa leo mkoani Dodoma na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako wakati wa hafla ya kukabidhi magari 45 kwa Wathibiti Ubora wa Shule wa Kanda na Wilaya na magari 2 kwa ajili ya Baraza la Mitihani Tanzania.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza wakati wa hafla ya ugawaji magari kwa Wathibiti Ubora wa Shule Kanda na Wilaya, pamoja na Baraza la Mitihani la Tanzania. Amesisitiza matumizi bora ya magari hayo ili yaweze kutimiza lengo lililokusudiwa.

Waziri Ndalichako amesema lengo la Taifa ni kuwa na watu walioelimika,  mahiri na wabunifu katika  kuelekea uchumi wa viwanda ifikapo 2025, hivyo ili kufikia malengo hayo  usimamizi wa karibu na tathmini ya mara kwa mara inahitajika.

Waziri Ndalichako amewasisitiza Wathibiti Ubora wa Shule kuhakikisha wanafanya  ufuatiliaji wa karibu wa kitaaluma ikiwa ni pamoja na kuhakikisha  walimu wanafika  shuleni  kwa  wakati  wanaingia  kwenye  vipindi  na wanafundisha.

 “Nataka nione mnasimamia kwa karibu taaluma na nataka  kuona  mabadiliko makubwa katika shule zetu za   Serikali  kuanzia  upande  wa  nidhamu na  taaluma ili mabadiliko yaweze kujitokeza  kwenye Shule zetu,  na tuone shule zetu  zinafanya vizuri katika matokeo ya Taifa ya kidato  cha  Nne,’’ alisisitiza Prof. Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akikata utepe kama ishara ya uzinduzi wa magari ambayo ameyagawa kwa Wathibiti Ubora wa Shule ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao ipasavyo.


Profesa Ndalichako ametaka magari hayo kutotumika katika malengo yasiyokusudiwa badala yake yatumike tu kwa ufuatiliaji wa taaluma shuleni.

“Haya ni magari kwa ajili ya ufuatiliaji wa Elimu, ninaagiza magari haya yasitumike kwa matumizi mengine yoyote tofauti na masuala ya Elimu, naomba hili likazingatiwe sana na yeyote atakayekikuka hatua za kinidhamu  zitachukuliwa,”alisisitiza Waziri Ndalichako.



Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akikagua moja ya gari lililonunuliwa na Wizara kama nyenzo na kitendea kazi kwa Wathibiti Ubora wa  Shule.



Pia Waziri Ndalichako amewataka Wakuu   wa  Shule  kuendelea  kusimamia  nidhamu  na kutowaonea huruma  wanafunzi wanaokiuka taratibu za Shule  kwani Serikali haitakuwa  na huruma na watendaji pale mambo yatakapokuwa hayaendi vizuri. 

“Angalieni  Mkuu wa Shule ya Sekondari Jangwani ameng’oka  kwa  hiyo  Serikali haitakuwa na huruma nanyi  pale mtakapowalea wanafunzi wenye 
utovu wa nidhamu Shuleni, wanafunzi hawatakiwi kuwa na simu shuleni  lakini bado wanafunzi wameendelea kuwa na simu, hakikisheni mnasimamia maadili na nidhamu za wanafunzi kwa mujibu wa taratibu zinavyoelekeza.

Mapema mwanzoni mwa Mwezi Julai Wizara iligawa pikipiki 2,894  kwa  ajili ya Waratibu Elimu kata ikiwa ni muendelezo wa kutatua changamoto ya usafiri kwaWathibiti Ubora ili wazeze kufikia shule zote na kufuatilia  hali  ya ufundishaji shuleni.
Baadhi ya Magari ambayo Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imenunua kwa ajili ya Wathibiti Ubora wa Shule Kanda na Wilaya pamoja na Baraza la Mitihani  Tanzania

Jumatano, 18 Julai 2018

NDALICHAKO AZITAKA TAASISI ZA ELIMU YA JUU ZENYE MAPUNGUFU ZIJIREKEBISHE


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amezitaka Taasisi za Elimu ya Juu nchini ambazo matokeo ya uhakiki yalibainisha kuwa na mapungufu kurekebishe kasoro hizo kama walivyoelekezwa na Mamlaka husika.

Waziri Ndalichako ametoa  agizo hilo Leo Jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi   wa Maonesho ya kumi na tatu ya Elimu ya Juu ambapo amesema taasisi hizo zisipofanya hivyo basi hatua stahiki zitachukuliwa, ikiwa ni pamoja na kufutiwa usajili.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wadau wa Elimu ya Juu (hawapo pichani) ambao wanashiriki katika maonesho ya kumi na tatu ya Elimu ya Juu wakati wa ufunguzi wa maonesho hayo yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es alaam ambapo amezitaka Taasisi zote za Elimu nchini kuzingatia ubora wa Elimu wanayoitoa.

Waziri  Ndalichako pia amewaagiza Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU) na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) kuendelea kusimamia kwa karibu na kwa  umakini masuala yote yanayohusu ubora wa Elimu inayotolewa na Taasisi za Elimu ya Juu.

” Katika Awamu hii ya Tano watu wanaofanya kazi kwa mazoea hawana nafasi, lazima muwe wabunifu nampitie upya zana mnazotumia kuhakiki ubora wa vyuo. Haiwezekani kila siku tunasikia malalamiko kuhusu ubora wa wahitimu wakati TCU na NACTE mpo” amesisitiza Prof. Ndalichako.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Prof. James Mdoe wakisikiliza ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali ya elimu  kutoka kwa mmoja wa washiriki wa maonesho ya kumi na tatu ya Elimu ya Juu yanayofanyika jijini Dar es Salaam, ambapo washiriki hao wametakiwa kujitadhimini kuhusu utoaji wao wa Elimu ya Juu 

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo  Prof. James Mdoe amesema maonesho hayo ya Elimu ya Juu yatazisaidia Taasisi mbalimbali za Elimu kujitathmini na kupata mrejesho kutoka  kwa wadau namna  wanavyotekeleza majukumu yao.

Maonesho ya Taasisi za Ellimu ya Juu ambayo yatafanyika kwa siku nne yanalenga kutoa elimu kwa umma kuhusu fursa zinazopatikana kwenye Taasisi za Elimu ya  Juu,  kutoa nafasi kwa wananchi wanaotarajia kujiunga na Elimu ili elimu ya kujiridhisha na programu za masomo na huduma zinazotolewa.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Prof. James Mdoe akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa Tume ya Vyuo Vikuu ambao ni waandaaji wa maonesho ya kumi na tatu ya Elimu ya Juu yanayofanyika jijini Dar es Salaam.