Jumatatu, 29 Oktoba 2018
Jumamosi, 27 Oktoba 2018
DHAMIRA YA SERIKALI YA KUWA NA CHUO KIKUU CHA KILIMO BUTIAMA IKO PALEPALE
Waziri wa Elimu, Sayansi na
Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amesema dhamira ya Serikali ya kumuenzi baba
wa Taifa Mwalimu Jullius K. Nyerere kwa kuwa na Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi
na Teknolojia, (MJUNAT) iko palepale.
Waziri Ndalichako ametoa kauli
hiyo akiwa Wilayani Butiama mkoani Mara mara baada ya kutembelea Chuo
hicho kwa lengo la kukagua miundombinu yake, pamoja na kuzungumza na watumishi
wanaofanya kazi chuoni hapo.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.
Joyce Ndalichako akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Mara Adam Malima wakitoka nje mara
baada ya kukagua bwalo la chakula katika Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi
na Teknolojia cha Mwalimu Nyerere.
Akizungumza na Watumishi wa Chuo
hicho pamoja na viongozi wa Mkoa na wale wa Wilaya ya Musoma na Butiama amesema
hivi sasa Serikali iko katika hatua za mwisho za makabidhiano ya miundombinu hiyo kutoka
kwa aliyekuwa mmiliki wa majengo hayo Nimrod Mkono.
Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu Moshi
Kabengwe na Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia CPA (T) Rose
Waniha wakifuatilia jambo wakati wa kikao cha Waziri kwenye Chuo Kikuu cha
Kilimo, Sayansi na Teknolojia cha Mwalimu Nyerere kilichopo Wilayani BUTIAMA
mkoani Mara.
Waziri Ndalichako amesema lengo la
kuwa na Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi na Teknolojia ni kumuenzi baba wa Taifa
kwa kutambua mchango wake katika suala la kilimo na kuwa suala hili pia
limeanzishwa kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi.
“Mchakato huu ulianza mwaka 2016
na kuwa hapo awali majengo haya yalikuwa yanamilikiwa na Nimrod Mkono, hivyo
Serikali haiwezi kujenga au kuboresha bila kuwa na maandishi ya kisheria ya
umiliki halali. Napenda kueleza kuwa makabidhiano yako katika hatua za mwisho
ili Serikali iweze kuendelea na taratibu nyingine” alisema Ndalichako.
Waziri Wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako
akipokelewa na Watumishi katika Chuo Kikuu cha Kilimo, Sayansi na Teknolojia
cha Mwalimu Nyerere, kilichopo Butiama, Mkoani Mara.
Ijumaa, 26 Oktoba 2018
SERIKALI YAAHIDI KUTOA MILIONI 700 KUBORESHA SHULE ALIYOSOMA BABA WA TAIFA MWALIMU NYERERE
Serikali imeahidi kutoa kiasi cha
Shilingi Milioni 700 kwa ajili ya kujenga na kukarabati Miundombinu mbalimbali
katika shule ya msingi Mwisenge aliyosoma Baba wa Taifa Mwalimu Jullius K.
Nyerere iliyopo manispaa ya Musoma mkoani Mara.
Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa
Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako mara baada ya kutii
maelekezo yaliyotolewa na Rais John Magufuli ya kuitembelea shule hiyo na kufanya
tathmini kwa lengo la kuikarabati ili iendane na hadhi ya Baba
wa Taifa.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako
akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Mara Adam Malima wakiwa wamekaa kwenye dawati
alilokuwa anatumia Baba wa Taifa Mwalimu Jullius Nyerere wakati akisoma katika shule
ya Msingi Mwisenge iliyopo manispaa ya Musoma, Mkoani Mara.
Waziri Ndalichako amesema,
kipaumbele cha Serikali ya awamu ya Tano ni Elimu, hivyo amemwelekeza Mkuu wa
mkoa huo Adam Malima kuhakikisha kuwa fedha ambazo zitaelekezwa katika shule
hiyo basi zisimamiwe ili zifanye kazi iliyokusiduwa na si kutumika vinginevyo.
“Rais John Magufuli akiwa katika
ziara zake alifika na kuona kuwa shule hii inahitaji kuboreshwa hivyo
alinielekeza nifike na kufanya tathmini kwa lengo la kuboresha Miundombinu ya
Shule hii, sasa Mkuu wa mkoa mimi na wewe tuhakikishe uboreshaji unafanyika
tena kwa kiwango kitakachoendana na hadhi ya Baba wa Taifa letu,” alisisitiza
Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu na Mkuu wa mkoa wa Mara
wakiwa nje ya bweni alilokuwa analala Baba wa Taifa Mwalimu Jullius K. Nyerere
katika shule ya msingi aliyokuwa anasoma ya Mwisenge iliyopo manispaa ya Musoma.
Waziri Ndalichako amesema fedha
hizo zitatumika kujenga mabweni mawili mapya, vyumba vitano vya madarasa,
kukarabati Nyumba za walimu na kuboresha Miundombinu ya maji.
Kwa upande wake Mkuu wa mkoa huo
Adam Malima ameahidi kusimamia fedha zitakazotolewa kwa ajili ya kuboresha
Miundombinu katika shule hiyo na kuwa shule hiyo itakuwa mfano na pia
kumbukumbu nzuri kwa Taifa.
Waziri Ndalichako pamoja na
viongozi mbalimbali wa mkoa huo pia wametembelea Shule ya sekondari ya Ufundi
Musoma, Shule ya sekondari Mara na Chuo Kikuu Cha kilimo na Teknolojia cha
Mwalimu Nyerere kilichopo Wilayani Butiama kwa lengo la kukagua hali ya
Miundombinu katika Taasisi hizo.
Darasa ambalo Baba wa Taifa Mwalimu Jullius K.
Nyerere alilitumia kwa ajili ya kusoma kuanzia mwaka 1934 - 1936, shule hiyo
ipo kwenye manispaa ya Musoma mkoani Mara.
Alhamisi, 25 Oktoba 2018
SERIKALI YAAHIDI KUENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA YA WATU WENYE ULEMAVU
Waziri wa
Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri zote
nchini kuhakikisha wanatenga asilimia 2 ya bajeti zao kwa ajili ya
kuhudumia watu wenye ulemavu na kuwa suala hilo lipo kisheria.
Waziri
Ndalichako ametoa kauli hiyo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Fimbo Nyeupe
duniani ambayo Kitaifa hapa nchini yamefanyikia Mkoani Mwanza.
Waziri
wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisalimiana na
Mkurugenzi Msaidizi wa idara ya Elimu
Maalumu wa Wizara hiyo Adamson Shimbatano aliyeshika Fimbo Nyeupe wakati wa
Maadhimisho ya Siku ya Fimbo Nyeupe duniani ambayo kitaifa yamefanyikia mkoani
Mwanza.
Ndalichako
amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe. Rais John Magufuli
imeendelea kuboresha mazingira ya watu wenye ulemavu ikiwa ni pamoja na
kutoa ajira na kuwa katika ajira za mwaka jana walimu 70 wasioona
waliajiriwa.
“Niwahakikishie
Watanzania kuwa Rais John Magufuli ni kiongozi anaejali sana watu wenye ulemavu
ndiyo maana wapo viongozi wenye ulemavu aliowateua kushika nafasi mbalimbali za
uongozi katika Serikali yake wakiwemo Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi, Mabalozi,
na wengine ili wamsaidie katika kutekeleza majukumu ya kuliletea Taifa
Maendeleo,” alisema Ndalichako.
Waziri
Ndalichako pia amewataka Wazazi kuacha tabia ya kuwaficha watoto wasioona na
badala yake wahakikishe watoto wote waliofika umri wa kwenda Shule
wanaandikishwa kwa kuwa hivi sasa Elimu msingi inatolewa bila malipo na kuwa
ulemavu siyo kikwazo cha Maendeleo.
Waziri
wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akipokea msaada wa Fimbo
Nyeupe kutoka kwa mmoja Wafanyabiashara mkoani Mwanza, ili fimbo hizo zigaiwe
kwa watu wasioona walioshiriki maadhimisho hayo mkoani Mwanza.
Akizungumza
katika Maadhimisho hayo Mwenyekiti wa Shirikisho la watu wenye ulemavu nchini
Tanzania Benedict Louis amempongeza na kumshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa
uongozi wake wa kutambua jitihada na uwezo wa watu wenye ulemavu na hivyo
kuwateua wenye ulemavu kushika nafasi mbalimbali.
Louis ameeleza kuwa Siku
ya Fimbo Nyeupe ni muhimu kwa kuwa inatoa fursa kwa wasioona kutathmini
jitihada zinazofanywa na serikali katika kuleta ustawi kwa watu wenye ulemavu
na kuwa Fimbo hiyo ni nyenzo muhimu ambayo inamsaidia asiyeona
kutambua vikwazo vilivyo mbele yake.
Kauli mbiu
ya mwaka huu katika maadhimisho hayo ni “ Mafunzo ya TEHAMA kwa wasioona ni
nyenzo Shirikishi ya uchumi wa Viwanda.”
Watu
wasioona wakicheza mziki pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof.
Joyce Ndalichako wakati wa maadhimisho ya siku ya Fimbo Nyeupe ambayo kitaifa yamefanyikia
mkoani Mwanza na kauli mbiu katika maadhimisho hayo ni mafunzo ya TEHAMA kwa
wasioona ni nyenzo shirikishi ya uchumi wa Viwanda.
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA
TEKNOLOJIA
MAJINA
YA WATANZANIA WALIOPATA UFADHILI WA MASOMO JAMHURI YA ALGERIA MWAKA WA MASOMO
2018 – 2019
Wizara ya Elimu, Sayansi na
Teknolojia inawapongeza wanafunzi wote waliopata fursa za ufadhili wa masomo
kutoka Serikali ya Jamhuri ya Algeria kwa mwaka wa masomo 2018/2019. Wanufaika wote mnatakiwa kuzingatia maelekezo
muhimu ili kufanikisha safari yenu ya kwenda masomoni.
Maelekezo
Muhimu
Wanafunzi wote wanatakiwa
kukamilisha maandalizi ya safari kwenda masomoni nchini Algeria kwa kufanya mambo
yafuatayo:
(i)
Kila mwanafunzi anatakiwa kuwasilisha “passport”
yaani hati ya kusafiria ubalozi wa Algeria kwa ajili ya VISA.
(ii)
Kulipa USD 50 kwa ajili ya VISA. Ada ya VISA italipwa ubalozi wa Algeria.
(iii)
Awe na picha passport size 3 zenye kivuli
cheupe.
(iv)
Tarehe ya safari ni kati ya tarehe 5 –
11/11/2018.
NB: Iwapo mnufaika atakuwa
na changamoto awasiliane na Mratibu Bwana L. Malili Na. ya simu ni
0715 150047.
NA
|
NAMBA YA USAJILI
|
JINA LA
MWANAFUNZI
|
JINA LA CHUO
|
PROGRAMMU
|
1
|
8TZA4703
|
Kassim
Adila Ally
|
University
of Science and Technology in Oran
|
Science
and Technology
|
2
|
8TZA4701
|
Oscar
Gomba
|
University
of Constantine 1
|
Natural
Science and life
|
3
|
8TZA4626
|
Mkumbo
Nakembetwa John
|
University
of Setf 1
|
Natural
Science and Life
|
4
|
8TZA4375
|
Faru
Suhayrnan R George
|
University
of Science and Technology in Blida 1
|
Science
and Technology Science
|
5
|
8TZA4126
|
Masige
Goodluck Stephano
|
University
of Constantine 1
|
English
|
6
|
8TZA4118
|
Ngwenya
Alfonce Simon
|
University
Sidi Bel Abbes
|
English
|
7
|
8TZA4132
|
Malekela
Yonathani Frank
|
University
of Constantine 1
|
Veterinary
Science
|
8
|
8TZA4175
|
Mohamed
Ali Mlenge
|
University
of Tlemcen
|
Science
and Technology
|
9
|
8TZA4182
|
Mwakikuti
Ezra George
|
University
of Blida 1
|
Veterinary
Science
|
10
|
8TZA4165
|
Malemo
Francisca Masatu
|
University
of Science and Technology in Oran
|
Hydraulic
|
11
|
8TZA4172
|
Kabyazi
Edibily Egbert
|
University
of Bejaia
|
Economic
Science Management and Trade
|
12
|
8TZA4039
|
Hussein
Mariam Ismail
|
University
of Constantine 1
|
English
|
13
|
8TZA4122
|
Meza
Ismail Omary
|
University
of Oran 2
|
English
|
Imetolewa na:
Katibu Mkuu,
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia,
25/10/2018
Jumanne, 23 Oktoba 2018
UFAFANUZI WATOLEWA KUHUSU WANAFUNZI KUJIUNGA UDSM
ALIYOYAZUNGUMZA NAIBU MAKAMU MKUU WA CHUO KIKUU CHA DAR ES
SALAAM PROF. BONAVENTURE RUTINWA KATIKA KIPINDI CHA JAMBO TANZANIA LEO TBC.
1. Wale wote waliiomba Chuo Kikuu
Cha Dar es Salaam (UDSM) wakafutiwa udahili kwa sababu ya kuwa wengi zaidi
(over capacity) wamerudishwa wote bila masharti yoyote.
2. Prof. Rutinwa ameeleza kuwa wale
walioko Dar es Salaam waendelee kuchukua barua zao za udahili (admission
letter) kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na wale walioko mbali na Dar es
Salaam watazipokea barua zao kuanzia tarehe 27/10/2018 watakapofika kwa
usaili.
3. Wataalamu wa mifumo ya
kompyuta wanaandaa utaratibu ili waliodahiliwa wapokee barua zao kwenye akaunti
zao za udahili.
4. Wanafunzi ambao wamekosa code
au wameshindwa kuingiza codes UDSM au vyuo vingine watapewa utaratibu wa kwenda
chuo wanachokitaka.
5. Kutakua na dirisha la wale
waliokosa nafasi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa sababu ya Program hizo
kujaa wapate nafasi ya kuomba tena.
6.Serikali imeendelea kuboresha
Miundombinu katika Chuo hicho ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya vyumba
vya madarasa na maabara kwa hali ya juu na ya viwango kwa ajili ya kuhudumia
wanafunzi ambao chuo hicho inataka kuwadahili.
7. Serikali pia inaendelea
kukiwezesha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuongeza idadi ya Wahadhiri wabobevu
ili kukidhi uhitaji.
8. Leo ilikuwa ni siku ya mwisho
kufunga udahili lakini mara baada ya kufanya kikao na Mhe. Waziri wa Elimu,
Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako alielekeza kuongezwa kwa siku hizo
ili kutoa fursa zaidi kwa wanafunzi.
9. Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
kinamshukuru sana Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce
Ndalichako kwa kusaidia kutatua changamoto iliyokuwepo katika udahili kwa
UDSM.
Jumatatu, 22 Oktoba 2018
WAZIRI NDALICHAKO AWATAKATA WAHASIBU WA WIZARA ANAYOINGOZA KUACHA “WIZI WA KISHAMBA”
Waziri wa Elimu, Sayansi na
Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amesema kuwa kuna baadhi ya wahasibu wa
Wizara hiyo na Taasisi zake ambao wamekuwa wakitumia vibaya nafasi zao kwa
kughushi nyaraka mbalimbali wakati wa kufunga mahesabu kwa lengo la kujipatia fedha
ambazo si halali yao.
Waziri Ndalichako ametoa kauli
hiyo jijini Dar es Salaam wakati akifungua mafunzo ya siku tano ya uandaaji wa
hesabu za Fedha za Serikali kwa wahasibu wa Wizara hiyo na Taasisi zake.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako
akizungumza na Wahasibu wa Wizara hiyo na taasisi zake wakati akifungua mafunzo
ya uandaaji wa hesabu za fedha za serikali jijini Dar es Salaam, ambapo Waziri
amesisitiza suala la uadilifu, uzalendo na kuwataka wahasibu kuacha kushughushi
nyaraka kwa lengo la kujipatia fedha ambazo siyo halali yao.
Waziri Ndalichako amesema
Wahasibu wa Wizara lazima wawe mfano katika kuonesha nidhamu kwa kuwa Wizara ya
Elimu, Sayansi na Teknolojia ndiyo Wizara mama kwani kada zote
zinafundishwa na walimu ambao msingi wao ni Wizara hiyo hiyo anayoiongoza.
Waziri Ndalichako ameeleza kuwa kuna
dalili kuwa kuna baadhi ya wahasibu katika Wizara hiyo wanachezea fedha za
Umma, hivyo amewaeleza Wahasibu hao kuwa hivi sasa kuna ukaguzi
unaendelea kwenye Wizara hiyo na matokeo ya ripoti hiyo yatakapokamilika umma
utajulishwa.
“Kuna misemo kuwa eti mbuzi anakula
kwa urefu wa kamba yake, sasa kamba inakatika, tuwe makini na kanuni za kazi,
Fedha za serikali katika awamu hii ya Tano ni sumu, nyaraka nyingi ambazo
zimekuwa zikitumika kwenye kufunga hesabu ni za kughushi, majina yamekuwa
yakijirudia katika semina ambazo zimekuwa zikifanyika, saini tofauti jambo
linaloashiria kuwa kuna wahasibu wanachezea fedha za serikali na huo ni wizi wa
kishamba, amesisitiza Waziri Ndalichako.
Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Elimu CPA (T) Rose Waniha akizungumza
na wahasibu wakati wa mafunzo ya uandaaji wa fedha za serikali mkoani dar es
salaam
Waziri huyo ameeleza kuwa zipo
pia baadhi ya Taasisi za Wizara hiyo zinapokusanya fedha za ada hawaziingizi
kwenye mfuko wa serikali.
Hivyo ameielekeza Wizara hiyo na
Taasisi zake zote kuhakikisha kuwa hadi itapofika Novemba moja mwaka huu ziwe
zimejiunga na mfumo wa serikali wa malipo ya kielektroniki (GePG- Government e
- payment Gateway Systeam) ili kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato ya
serikali.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako
akizungumza na Mhasibu Mkuu wa Wizara hiyo CPA(T) Rose Waniha wakati wa
ufunguzi wa mafunzo ya uandaaji wa hesabu za Fedha za Serikali, mafunzo hayo ya
siku Tano yameanza leo na yatakamilika oktoba 26, 2018
Kwa upande wake Mhasibu Mkuu wa
Wizara hiyo CPA (T) Rose Waniha amesema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea
uwezo wahasibu kuwa na uelewa wa pamoja wa namna bora ya uandaaji wa
hesabu za fedha za serikali.
Mafunzo hayo ya siku Tano yaliyoanza
leo yatahitimishwa oktoba 26, 2018.
Baadhi ya wahasibu wakifuatilia hotuba ya
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako wakati wa
ufunguzi wa mafunzo ya uandaaji wa hesabu za Fedha za serikali, mafunzo
yanayofanyika jijini Dar es salam.
Jisajili kwenye:
Machapisho (Atom)