Ijumaa, 14 Desemba 2018


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA

Anuani ya simu “ELIMU”
Simu: 026  296 35 33
Baruapepe:info@moe.go.tz
Tovuti: www.moe.go.tz



Chuo cha Masomo ya Biashara na Sheria,
Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Jengo Na. 10,
S.L.P. 10,
40479 DODOMA.

Tarehe: 10 Desemba, 2018.

WARAKA WA ELIMU NA. 2 WA MWAKA 2018
UTARATIBU WA KUKARIRI DARASA KWA WANAFUNZI WA SHULE ZA MSINGI NA SEKONDARI

Serikali imekuwa na utaratibu wa kupokea na kushughulikia maombi ya kukariri darasa kutoka kwa baadhi ya wazazi na walezi wa watoto wanaoshindwa kuendelea na masomo kwa sababu mbalimbali. Aidha, Shule Zisizo za Serikali zimekuwa zikiwakaririsha darasa wanafunzi wanaoshindwa kufikia viwango vya ufaulu vinavyopangwa na shule husika.

Kufuatia hali hiyo kumekuwepo na malalamiko kutoka kwa wazazi na walezi kutokana na kutoshirikishwa ipasavyo katika kufanya uamuzi wa mwanafunzi kukariri darasa. Kutokana na changamoto zinazojitokeza kwenye suala hili wizara inapenda kutoa maelekezo kama ifuatavyo:

1.0 Kukariri Darasa
Maombi ya Kukariri darasa kwa wanafunzi wa Shule za Msingi na Sekondari yatashughulikiwa kama ifuatavyo:
(a)                  Maombi ya Kukariri darasa la I, II na III yatashughulikiwa na Halmashauri husika ambapo darasa la IV, V na VI kwa Shule za Msingi na kidato cha 1, 2, 3, na 5 kwa shule za Sekondari yatashughulikiwa na Mkoa;
(b)         Maombi ya kukariri darasa la VII kwa shule za Msingi na Kidato cha 4 na 6 ambayo ni madarasa ya mitihani ya mwisho ya Kitaifa yataendelea kutumwa kwa Kamishna wa Elimu ili kupata kibali cha kukariri; na
(c)                  Mwanafunzi atakayeomba na kukubaliwa kukariri katika ngazi ya Elimu ya Msingi na Sekondari atapewa fursa ya kukariri mara moja. Endapo mamlaka inayohusika itaona umuhimu wa Mwanafunzi kukariri darasa  mara ya pili, ataweza kupewa fursa hiyo.

(d)         Utaratibu wa Maombi ya Kukariri Darasa
                                 i.        Mzazi wa mwanafunzi wa darasa la I, II na III anatakiwa kuandika barua ya maombi ya kukariri darasa kwa Mkurugenzi wa Halmashauri husika;
                               ii.       Mzazi wa mwanafunzi wa  darasa la IV, V na VI kwa shule za Msingi na Kidato cha 1, 2, 3, na 5 kwa shule za Sekondari anatakiwa kuandika barua kwa Katibu Tawala wa Mkoa;
                        iii.            Mzazi wa mwanafunzi wa darasa la VII kwa Shule za Msingi na Kidato cha 4 na 6 kwa shule za Sekondari anatakiwa kuandika barua kwa Kamishna wa Elimu kulingana na darasa husika;
                        iv.            Maombi yote yapitie kwa Mkuu wa Shule anayosoma mwanafunzi na Mkurugenzi wa Halmashauri husika, na
                           v.            Kila barua ya maombi ni lazima iwe na viambatisho vifuatavyo:
a.      Picha 2 za mwanafunzi aina ya pasipoti;
b.     Namba ya kuandikishwa shuleni; na
c.      Nyaraka zozote muhimu kulingana na sababu ya maombi                                        yanayowasilishwa.

2.0    Kukariri Darasa Wanafunzi Wanaoshindwa Kufikia Viwango vya Ufaulu Vilivyowekwa na Shule

Wizara inakumbusha kuwa wanafunzi waliofaulu mitihani ya upimaji inayofanywa kitaifa (Darasa la IV na Kidato cha 2) wanakuwa na sifa ya kumaliza ngazi ya elimu husika bila kukariri.

Hata hivyo, kwa makubaliano ya maandishi kati ya mzazi au mlezi na Mkuu wa shule ya Serikali au isiyo ya Serikali, mwanafunzi ataruhusiwa kukariri Darasa kwa kufuata utaratibu ulioainishwa hapo juu ambapo mzazi atakuwa ameridhia.

Waraka huu unafuta nyaraka zote zilizotangulia zilizokuwa zikitoa maelekezo kuhusu utaratibu wa kukariri darasa na utaanza kutumika Januari, 2019.



Dkt. Edicome C. Shirima
KAIMU KAMISHNA WA ELIMU

WAZIRI NDALICHAKO AAHIDI KUSHUGHULIKIA UCHAKAVU WA MIUNDOMBINU VYUO VYA VETA NCHINI


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Joyce Ndalichako ameahidi kushughulikia changamoto ya uchakavu wa miundombinu katika vyuo vya ufundi stadi vinavyomilikiwa na VETA ili vyuo hivyo viweze kutoa mafunzo bora yanayoendana na Teknolojia ya kisasa.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo wakati wa sherehe za mahafali ya 33 katika Chuo Cha VETA kilichopo katika Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro na kusisitiza kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na  Teknolojia ina jukumu la kuhakikisha Taasisi   zilizo chini yake zinakuwa  na mazingira bora  ya kazi , hivyo  iko tayari kupokea mchanganuo wa mahitaji ya vyuo vya ufundi stadi nchini ili vyuo hivyo viweze kufanyiwa kazi.

“Wizara ikiwezeshwa  vizuri ikafahamu mahitaji ya vyuo hivi vya Ufundi Stadi na kwa sababu ni kipaumbele cha serikali ya awamu ya Tano katika kuwezesha nchi kuwa na uchumi wa kati basi tuko tayari kupokea ushauri  wa wataalam ili tuweze kuhakikisha kuwa tunaimairisha mafunzo ya ufundi stadi kwa kiwango ambacho ndio kinahitajika na wataalam na wajiri pindi vijana wanaoomaliza mafunzo,” alisema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako  akisikiliza maelezo kutoka kwa mhitimu  wa fani ya kukaanga Mvuke kwenye  maonesho ya Mahafali ya 33 Chuoni hapo. Aliyesimama kulia kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu.

Waziri Ndalichako amesema kuwa  mfumo wa mafunzo kwa njia ya uanagenzi una manufaa siyo tu  kusaidia kuongeza udahili,  lakini pia mfumo huu unasaidia vijana kujifunza teknolojia mpya zilizopo viwandani, kusaidia vijana kupata ujuzi na uzoefu halisi unaohitajika mahala pa kazi katika fani husika na makampuni kuwa na uhakika wa nguvukazi yenye umahiri wa kiwango wanachokihitaji.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi - VETA- Dkt. Pancras Bujulu alisema kuwa baadhi ya vyuo vya VETA ni vikongwe mno na miundombinu yake imechakaa  na vinahitaji ukarabati.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako akitazama nyaraka za kampuni ya LES Inspection iliyoanzishwa na wahitimu wa VETA ambao wamefuzu na kupata leseni za kutoa ithibati ya kazi za uungaji vyuma kwa kiwango cha kimataifa wakati akitembelea maonesho ya mahafali ya 33 ya Chuo cha VETA katika manispaa ya Moshi.

Dkt. Bujulu alimweleza Waziri Ndalichako kuwa pamoja na uchakavu wa Miundombinu lakini pia  vifaa na mashine zinazotumika kwenye karakana kwa ajili ya kufundishia nazo  zimechakaa na zingine  zimepitwa na wakati kutokana na mabadiliko ya kiteknolojia hivyo hazifai kutumika kufundishia, vifaa vinavyohitajika ni vile vinavyoendan na Teknolojia.

Jumla  ya wahitimu 174 wa fani mbalimbali  wamehitimu mafunzo yao katika mahafali hayo ya 33 katika Chuo hicho Cha VETA, manispaa ya Moshi mkoani  Kilimanjaro.

NAIBU WAZIRI OLE NASHA ASHIRIKI UJENZI WA SHULE WILAYANI SAME


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe.William Ole Nasha ameshiriki shughuli za ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule ya msingi Ruvu iliyopo Wilayani Same Mkoani Kilimanjaro.

Mhe.Ole Nasha ameshiriki ujenzi huo na Wananchi wa Kijiji cha Ruvu Darajani wakati kukagua miradi ya inayotekelezwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknlojia katika Wilaya hiyo ambapo amewataka wananchi kuendeleza jitihada hizo ili kuweka  mazingira mazuri ya wanafunzi kusoma.
Naibu Waziri Wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akishiriki ‘Msaragambo’ wa Ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule ya msingi Ruvu iliyoko Kata ya Ruvu Darajani Wilayani Same Mkoani Kilimanjaro alipofanya ziara kukagua miradi ya elimu inayotekelezwa katika Wilaya hiyo.

Kufuatia jitihada hizo za Wananchi Naibu Waziri Ole Nasha amewaahidi wananchi kuwa Wizara itajenga  vyumba viwili vya madarasa, mabweni mawili na matundu ya vyoo ikiwa ni kuunga mkono juhudi ambazo wananchi wa kijiji cha Ruvu Darajani wameonesha lakini pia kuwezesha wanafunzi kutulia shuleni na kusoma.

“Serikali ikiona eneo ambalo wananchi wameanza na wana hamasa ya kujiletea maendeleo haiwezi kusita kuja kusaidia, Wilaya ya Same mmeonesha mfano kupitia utaratibu wenu wa kufanya kazi kwa umoja na ushirikiano hivyo Wizara itaunga mkono juhudi hizi kwa kuwajengea vyumba vya madarasa, mabweni na matundu ya vyoo,” alisema Naibu Waziri Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akitoa aelekezo katika eneo ambalo vyumba viwili vya madarasa vitajengwa katika Shule ya Msingi Ruvu Iliyoko katika Kata ya Ruvu Darajani Wilayani Same Mkoani Kilimanjaro.

Naibu Waziri huyo pia amewataka wananchi wa Kijiji cha Ruvu Darajani ambao wanajihusisha na shughuli za ufugaji kuacha kutumia watoto kuchunga mifugo badala yake kuhakikisha wanatumia fursa ya Elimu bure kuwaandikisha watoto wote waliofikia umri wa kwenda shule.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Same Rosemary Staki alimweleza Naibu Waziri wa Elimu kuwa changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa katika shule ya msingi Ruvu ambayo imetokana na ongezeko la Wanafunzi waliohamishiwa shule hiyo kutokana na shule walizokuwa wakisoma miundombinu yake kuathiriwa na mafuriko yaliyotokana na mvua za masika za mwaka huu.

Katika ziara hiyo Naibu Waizri Ole Nasha pia alitembelea shule ya Sekondari Makanya, Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same na Shule ya Sekondari Same ambapo ameridhishwa na ukarabati ulivyofanyika katika shule kongwe hiyo .
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua ukarabati wa miundombinu uliofanyika katika Shule ya Sekondari Same iliyoko Wilaya ya Same Mkoani Kilimanjaro. Ameridhishwa na namna ukarabati huo ulivyofanyika na kuwataka kutunza miundombinu hiyo ili iweze kutumika kwa muda mrefu.

SKAUTI WATAKIWA KUJENGA NA KULEA MAADILI MEMA KWA VIJANA


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amewataka viongozi wa Chama cha Skauti Tanzania kuwajenga na kuwalea vijana katika maadili mema ya kitanzania .

Waziri Ndalichako ametoa agizo hilo wakati wa hafla ya kumkabidhi Balozi Nicholas Kuhanga tuzo ya Elephant Award aliyotunukiwa na Chama cha Skauti Kanda ya Afrika iliyofanyika jiji Dar es Salaam ambapo amesema tuzo hiyo inatolewa ili Kutambua huduma iliyotukuka na mchango wa balozi huyo  katika maendeleo ya shughuli za Skauti barani Afrika.

“Ninawapongeza Viongozi wote wa Chama kwa kujenga na kulea maadili mema, na kwa juhudi zenu katika kupambana na mmomonyoko wa maadili ili kujenga taifa lenye wazalendo watakao iletea nchi maendeleo ya kweli” alisisitiza Waziri Ndalichako
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akimvisha nishani ya tuzo ya Elephant Award Balozi Nicholas Kuhanga aliyotunukiwa na Chama cha Skauti Kanda ya Afrika katika hafla ya kumkabidhi iliyofanyika jiji Dar es Salaam.

Waziri Ndalichako amesema Balozi Kuhanga ameiweka nchi katika kumbukumbu ya kihistoria katika ngazi ya Skauti Kanda ya Afrika kwa kuwa  tuzo aliyopata ina hadhi ya juu kuliko zote ndani ya Skauti Kanda ya Afrika, hivyo mchango wa Balozi Kuhanga ni wa kujivunia na ni mfano wa kuigwa, hasa kwa vijana ambao ni viongozi wa baadae.

Akizungumza katika hafla hiyo Kamishna Mtendaji wa chama hicho Eline Kitaly amesema Balozi Kuhanga amekuwa kiongozi wa mstari wa mbele katika shughuli za skauti, na hata alipostaafu kazi serikalini ameendelea kuwa kiongozi wa Skauti anayefundisha maadili mema kwa skauti pamoja na Viongozi waSkauti Tanzania.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akimpatia zawadi Balozi Nicholas Kuhanga iliyotolewa na Chama cha Skauti Tanzania wakati wakuadhimisha miaka 100 ya skauti nchi, zawadi hizo zimekabidhiwa leo jijini Dar es Salaam. 

Kwa upande wake Balozi Nicholas Kuhanga ameishukuru Serikali ya Tanzania  kwa kumpatia elimu iliiyomwezesha  kufanya kazi zake kwa umakini na pia aliwashukuru watumishi wa skauti kwa ushirikiano waliompa mpaka kufikia hatua ya kupata tuzo hiyo.

UINGEREZA NA CANADA KUENDELEA KUSAIDIA SEKTA YA ELIMU


Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Benki ya Dunia zimekubalina kuendelea kuimarisha programu za  Mpango wa Elimu kwa walioikosa (MEMKWA) na Mpango wa Elimu Jumuishi baada ya Kumaliza elimu msingi (IPPE), ili kuwezesha wanafunzi wanaokatisha masomo kabla ya kumaliza shule waweze kuendelea na masomo yao.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako wakati wa mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Afrika Mashariki na Kusini kutoka nchini Canada Mars Andre Fredette aliyeambatana na Balozi wa Canada nchini Tanzania Pamela O Donnell ambao wote kwa pamoja wamejadili masuala mbalimbali pamoja na nchi hiyo kuendelea kuisaidia Tanzania katika  Sekta ya Elimu.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo na Mkuu wa DFID Tanzania Beth Arthy aliyefika kwenye ofisi za Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia zilizopo jijini  Dar es Salaam kujadili masuala mbalimbali kuhusu sekta ya  Elimu
Waziri Ndalichako amesema nia ya serikali ni kuona kila mtoto wa kitanzania anayepaswa kupata elimu anaandikishwa na kubaki shule mpaka anapomaliza masomo yake ingawa kumekuwepo na Changamoto ya baadhi wa wanafunzi kukatisha masomo kutokana na sababu mbalimbali.

 “Ukitembea barabarani unakutana na watoto wadogo wakifanya biashara ndogondogo unapoongea nao wanakwambia wameacha shule ili kusaidia wazazi kufanya biashara hizo, wengine utawakuta wapo mashambani wanawasaidia wazazi kulima hivyo changamoto ya watoto kukatisha masomo ni kubwa, na ndiyo maana serikali inaona namna bora ya kuhakikisha wale wote wanaokatisha masomo wanajiendeleza”alisisitiza waziri Ndalichako

Waziri Ndalichako amesema programu ya MEMKWA inamwezesha mtoto ambaye hakwenda shule kabisa kusoma na kisha kufanya mtihani wa darasa la nne na baadaye anapofaulu huandikishwa katika  mfumo rasmi na kuendelea na masomo kama wanafunzi wengine wakati mfumo wa IPPF ni kwa ajili ya wanafunzi wanaokatisha masomo ya sekondari  unawawezesha kumaliza masomo hayo na kuendelea na elimu juu.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akijadiliana na Mkurugenzi Mkuu wa Afrika Mashariki na Kusini kutoka Canada Mars Andre Fredette aliyeambatana na Balozi wa Canada nchini Tanzania Pamela O Donnell ambao kwa pamoja wamejadiliana namna bora ya kuboresha elimu nchini Tanzania.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Afrika Mashariki na Kusini kutoka Canada Mars Andre Fredett amesema Canada inajivunia uhusiano wa muda mrefu uliopo katika ya Tanzania na Canada ambao umewezesha nchi kupata misaada mbalimbali ya kuendeleza sekta ya elimu ambayo imewezesha watoto wa kike na kiume kupata elimu bora pamoja na kutoa mafunzo kwa walimu.

Waziri wa Elimu pia amefanya mazungumzo na Balozi wa Finlanda nchi Pekka Hukka na Mkuu wa Dfid Tanzania Beth Arthy ambao wamezungumzia masuala mbalimbali ya namna bora ya kuboresha elimu nchini ikiwepo masuala ya kuongeza fursa za upatikanaji wa elimu bora kwa kila mtoto wa kitanzania.

SERIKALI YATOA MAELEKEZO UJENZI WA VETA SIMANJIRO


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia WilliamOle Nasha ameitaka Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara kuhakikisha inahusisha Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA katika ujenzi wa Chuo Cha VETA Wilayani humo ili miundombinu ya chuo hicho ijengwe kwa utaratibu na viwango vinavyohitajika.

Naibu Waziri Ole Nasha ametoa agizo hilo Mkoani Manyara wakati akikagua eneo ambalo Serikali ya Wilaya hiyo inategemea kujenga Chuo cha Veta kwa kushirikiana na Shirikala Maendeleo ya Hiari ECLAT.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Yefred Myenzi kuhusu namna walivyojipanga kujenga Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi cha Wilaya katika eneo la Mradi la Emboreet lililoko katika Wilaya hiyo.
Alisema ni vizuri Mamlaka husika zikahusishwa katika ujenzi wa Chuo hicho kuanzia hatua za awali na kumtaka Mkurugenzi wa kanda  hiyo na yule wa Mkoa kufika katika eneo la Emboreet ambako mradi utajengwa ili kuzungumza  na wananchi ili mradi utekelezwe kwa utaratibu  unaostahili.

“Mnataka kujenga chuo cha Ufundi ni wazo zuri lakini ni lazima kijengwe kwa utaratibu sio kiholela kwa sababu kumeanza kuibuka utitiri wa vyuo ambapo mtu anakuwa na jengo moja anakutana chuo, kuna viwango na masharti ambayo ni lazima yatimizwe kabla chuo kuruhusiwa kufanya kazi kwa hiyo na nyinyi fuateni taratibu hizo ili muweze kuanzisha chuo cha Ufundi,” alisisitiza Naibu Wazizri Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akitoa zawadi kwa mmoja wa wanafunzi wa shule ya msingi Kitwai A aliyefanya vizuri katika mitihani ya kuhitimu darasa la saba mwaka 2018. Shule ya Msingi Kitwai A imefaulisha wanafunzi 25 kati ya 28 waliofanya mtihani mwaka huu. 
Mheshimiwa Ole Nasha amesema Serikali ya Awamu ya Tanoimeweka mkazo mkubwa katika Elimu ya Ufundi kwa kuwa kuna vijana wengi wanaomaliza shule wanaishia kutokuwa na ajira kwa kuwa hawana maarifa yanayowasaidia kupata ajira hasa pale wanapokosa fursa ya kuendelea na elimu ya juu hivyo ujenzi wa vyuo vya ufundi vingi utasaidia kuwajengea vijana  uwezo wa kujiajiri.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Yefred Myenzi alisema wazo la kuanzisha  kwa Chuo hicho kutawawezesha vijana  kupata maarifa ya kujiajiri badala ya kusubiri kuajiriwa.

Naye Meneja Mradi ya ECLAT Bakiri Angalia alisema  pamoja na shirika hilo kushiriki ujenzi wa Chuo hicho  pia  imefadhili miradi ya Elimu yenye thamani ya  zaidi ya sh bilioni 3 katika Wilaya hiyo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiongea na wakazi wa Kata ya Kitwai A iliyoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara ambapo amewataka kuhakikisha wanawandikisha shule wanafunzi wote wenye umri wa kuanza shule bila kuwaacha nyumbani na kuwapangia majukumu mengine.

DKT. AKWILAPO: SEKTA YA ELIMU INA MAFANIKIO MAKUBWA KWA SASA


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo amesema Serikali ya awamu ya Tano ya inatambua mchango na juhudi zinazofanywa na shule zinazoendeshwa na makanisa hapa nchini (CSSC) ikiwa ni pamoja na baadhi ya shule kufanya vizuri katika matokeo ya mitihani na kutoa malezi bora kwa watoto.

Dkt. Akwilapo ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na Wakuu wa Shule za Sekondari za Makanisa na kueleza kuwa mafanikio ambayo yamepatikana katika sekta ya elimu hivi sasa ni makubwa ukilinganisha na wakati nchi inapata uhuru.
Wakuu wa shule za Sekondari za Makanisa  hapa nchini wakimsikiliza Katibu Mkuu (hayupo pichani) wakati akifungua mkutano wenye lengo la kujadili mafanikio na Changamoto katika shule wanazozisimamia.mkutano huo wa siku mbili unafanyika mkoani Dodoma.

Ameeleza kuwa  Wakati nchi inapata uhuru mwaka 1961 kulikuwa na  shule 3,238  lakini hadi kufikia mwaka 2018  zipo  shule za elimu ya  msingi 17,704 zilizosajiliwa , Elimu ya sekondari zilianza shule 41, lakini sasa kuna  shule  4,963 zilizosajiliwa   na kati ya hizi  shule  1,266   ni shule binafsi.

Vyuo vya ualimu navyo vimeongezeka kutoka vyuo 3 Lakini sasa kuna vyuo 138  na  kati ya hivyo   103 viko chini ya umiliki wa taasisi binafsi  ambapo  makanisa  wanamiliki  vyuo  15.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia akizungumza na Wakuu wa shule za Sekondari za Makanisa wakati akifungua mkutano huo na kueleza kuwa Sekta ya elimu imekuwa na mafanikio makubwa katika kipindi hiki cha serikali ya awamu ya Tano ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu mbalimbali katika sekta hiyo.

“Nawapongeza kwa kutoa huduma na kusimamia elimu, zipo baadhi ya shule zenu ni mfano  katika kufanya vizuri kwenye matokeo, shule za makanisa  pia zinatoa malezi bora kwa watoto kwa lengo la kuwa na viongozi bora na waadailifu wa Taifa la baadae, hii ni juhudi ya kuunga mkono serikali ya awamu ya Tano na serikali yenu inatambua hilo,”alisistiza Dkt. Akwilapo.

Kwa upande wake Mwalimu Petro Masatu ambaye ni Mkurugenzi wa huduma  za elimu CSSC alimweleza Katibu Mkuu baadhi ya changamoto walizonazo ikiwa ni pamoja na suala la upimaji wa watoto /wanafunzi kwa kuzingatia umahiri kutoka darasa moja kwenda jingine kuwa bado kuna utata kati ya shule zisizo za serikali, Wazazi na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kuchelewa kwa Sekula mpya kwa shule zisizo za serikali ili uwe mwongozo mzuri kwa mwaka 2019 pamoja na kuchelewa kwa sheria mpya ya elimu ambayo yote Katibu Mkuu ameahidi kuyafanyia kazi.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akisalimiana na baadhi ya viongozi wa CSSC muda mfupi baada ya kupokelewa na wenyeji wake katika mkutano wa Wakuu wa shule za sekondari za makanisa unaofanyika mkoani Dodoma.