Jumapili, Novemba 3, 2019
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza orodha ya awamu ya tatu yenye jumla ya wanafunzi wa mwaka kwanza 4,785 waliopata mikopo yenye thamani ya TZS 14.3 bilioni na hivyo kufanya jumla ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza waliopata mikopo yenye thamani ya TZS 162.86 bilioni hadi sasa kufikia 46,838.
Orodha ya kwanza ilitolewa Oktoba 17 mwaka huu na ilikuwa na wanafunzi wa mwaka wa kwanza 30,675 waliopata mikopo yennye thamani ya TZS 113.5 bilioni. Orodha ya pili ilitolewa Oktoba 26 mwaka huu ikiwa na wanafunzi wa mwaka wa kwanza 11,378 waliopangiwa mikopo yenye thamani ya TZS 35.06 bilioni.
Taarifa iliyotolewa leo (Jumapili, Novemba 3, 2019) na Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru imeeleza kuwa wanafunzi waliopata mikopo katika awamu ya tatu wanaweza kupata taarifa zao kupitia akaunti walizotumia kuomba mkopo maarufu kama SIPA – Student’s Individual Permanent Account.
Pamoja na SIPA, Badru amesema majina yote ya waombaji waliofanikiwa kupangiwa mikopo katika awamu hii ya pili yanapatikana katika mtandao wa HESLB wa uombaji mkopo (https://olas.heslb.go.tz) na tovuti ya Bodi (www.heslb.go.tz).
“Awamu hii ya tatu inajumuisha wanafunzi wahitaji ambao wamekamilisha taratibu za udahili pamoja na kukamilisha marekebisho ya maombi yao yaliyokuwa na dosari … tutaendelea kufanyia kazi maombi yanayorekebishwa na wale wenye sifa watapangiwa,” amesema Badru.
Kuhusu taratibu za malipo kwa wanafunzi, Badru amesema fedha za wanafunzi waliopata mikopo zimeshapelekwa vyuoni na vyuo vimeleekezwa kuhakikisha fedha zinawafikia wanafunzi walengwa mara wanapofika na kukamilisha taratibu za usajili.
“Serikali imeshatupatia TZS 125 bilioni ambazo tulikuwa tunazihitaji kwa ajili ya malipo ya robo ya kwanza ya Oktoba hadi Disemba mwaka huu na sisi tumeshatuma vyuoni na maafisa wetu wameanza kwenda vyuoni ili kukutana na wanafunzi na kutatua changamoto iwapo zitajitokeza,” amesema Badru.
Badru amesema katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga TZS 450 bilioni kwa ajili ya jumla ya wanafunzi 128,285. Kati yao, wanafunzi 83,285 ni wenye mikopo wanaoendelea na masomo ya mwaka wa pili, tatu na kuendelea.
Bodi inapenda kuwasihi waombaji wa mikopo kuwa watulivu wakati mchakato wa upangaji wa mikopo kwa wanafunzi wenye sifa kwa awamu inayofuata ukiendelea.
Mwisho.
Jumatatu, 4 Novemba 2019
Ijumaa, 1 Novemba 2019
SERIKALI KUIMARISHA MICHEZO KATIKA VYUO VYA UALIMU
Serikali ya Awamu ya Tano
imeweka kipaumbele katika kuimarisha michezo kama eneo muhimu la mtaala wa
mafunzo ya ualimu kutokana na ukweli kwamba michezo inaimarisha stadi za
kujifunza, nidhamu na ni ajira pia.
Hayo yamesemwa Mkoani Mtwara
na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha wakati wa
kufunga Mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania
Bara (UMISAVUTA).
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akitoa kombe la ushindi wa mpira wa miguu kwa wachezaji wa Kanda ya Ziwa wakati wa ufungaji wa mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa ya Vyuo vya Ualimu UMISAVUTA yaliyomalizika mkoani Mtwara.
Amesema pamoja na kuwepo kwa
mchepuo wa michezo katika baadhi ya vyuo vya Ualimu ni vizuri vyuo hivyo
kupitia Ofisi ya Kamishna wa Elimu wakaweka mikakati ya kuhakikisha kuwa
ufundishaji na ujifunzaji wa michezo na Sanaa unalenga kuwawezesha vijana
kufanya vizuri katika eneo hilo kwa maendeleo yao na Taifa.
Ametaja vyuo ambavyo kwa
sasa vinatoa mchepuo wa michezo kuwa ni Chuo cha Ualimu Tarime, Butiama,
Butiama Mtwara Kawaida na Ilonga na kwamba Wizara itahakikisha kuwa michezo
inaimarishwa katika vyuo vyote vya ualimu nchini.
Naibu Waziri Ole Nasha amevitaka
vyuo vya ualimu kuhakikisha vinaendeleza michezo chuoni kutoka na faida
zitokanazo na michezo ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wahitimu wa mafunzo ya ualimu wanapata
mafunzo ambayo wakihitimu wanakwenda kuwa walimu mahiri wa michezo katika shule
za msingi na sekondari ambapo ndipo wanamichezo na wasanii wanaandaliwa.
“Nimefarijika kuona mashindano
ya michezo na Sanaa kwa vyuo vya ualimu imerudi tena baada ya kutokuwepo kwa
miaka 20 iliyopita hatuna budi kuwekeza katika michezo kwa sababu ni fursa za kuweza
kusaidia kukua kiuchumi. Nchi nyingi duniani michezo imekuwa sehemu kubwa ya kusaidia
kukua kiuchumi,” alisema Naibu Waziri Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akisalimiana na wachezaji kabla ya kuanza mechi ya fainali wakati wa ufungaji wa Mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania Bara yaliyofanyika Mkoani Mtwara.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu
wa Mkoa wa Mtwara ambae pia ni Afisa Elimu Mkoa Germina Mng’aho amesema
kufanyika kwa michezo hiyo ni utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi
ambayo inataka kuwepo kwa mashindano ya michezo kwa shule na vyuo ili kuwezesha
kuinua vipaji ambavyo vitaleta mafanikio katika michezo ya kitaifa na kimataifa.
Nae Kaimu Mkurugenzi Msaidizi
Seksheni ya Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
Agusta Lupokela amesema anaishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kutambua
faida zinazopatikana katika michezo ikiwemo stadi za kujifunza na kuamua
kurejesha mashindano ya michezo kwenye Vyuo vya Ualimu.
Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Seksheni ya Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na TeknolojiaAgusta Lupokela akikabidhi kikombe kwa mwakilishi wa Kanda ya Kaskazini ambao ni washindi wa mbio wakati wa kufunga mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu, UMISAVUTA mkoani Mtwara
Akitoa taarifa ya mashindano
hayo kwa Naibu Waziri Mwenyekiti wa
UMISAVUTA Taifa Agustine Sahili amesema kuwa michezo hiyo imeendeshwa kulingna
na taratibu za michezo na matokeo yameamuliwa kwa weledi na haki katika kupata
washindi.
Sahili ameiomba Wizara kuimarisha kozi ya michezo na fani mbalimbali
za ndani katika vyuo vya ualimu ili wataalamu waweze kupatikana shuleni ambako
ndiko chimbuko halisi la vipaji linapatikana lakini pia kuwajengea uwezo
wasimamizi na waamuzi wa michezo kwa kuendesha kozi fupi na ndefu kwa
kushirikiana na Wizara ya Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Pia ameiomba Wizara kuongeza
wakufunzi wa michezo na Sanaa vyuoni kwani kwa sasa vyuo vingi havina wakufunzi
wa aina hiyo hali inayodunisha uendeshaji wa michezo na ukuzaji wa vipaji kwa
vijana chuoni ambapo pia inasababisha shule za msingi na sekondari kukosa
walimu mahiri katika michezo na Sanaa.
Wanamichezo wakipita mbele ya mgeni rasmi (hayupo pichani) wakati wa kufunga mashindano ya Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ulimu yaliyofanyika Mkoani Mtwara.
Nae Mshiriki wa Mashindano
ya Michezo na Sanaa Albert Thomas kutoka Kanda ya Ziwa ameishukuru Serikali kwa
kurejesha mashindano ya UMISAVUTA kwani inasaidia kujenga afya na akili lakini pia inasaidia kuwa na uelewa wa
masula ya michezo na kutoa elimu ya michezo kwa wanafunzi ambao watakwenda
kuwafundisha baada ya kumaliza masomo.
Ameiomba Serikali kuendeleza vipaji vya wanamichezo wanaoshindana katika
mashindano ya ngazi ya shule na vyuo na kuonekana washindi ili vipaji hivyo visiishie
kwenye ngazi ya kitaifa bali katika ngazi ya kimataifa.
Ufungaji wa mashindano ya
Kitaifa ya Michezo na Sanaa kwa vyuo vya ualimu yaliyoanza Oktoba 25, 2019 na
kuhitimishwa Oktoba 31, 2019 yamepambwa na mechi kati ya Kanda ya ziwa na kanda
ya kusini ambapo kanda ya ziwa wameibuka kidedea baada ya kuwafunga kanda ya
kusini goli moja kwa sifuri.
Kanda ya Ziwa wakifurahia kupata vikombe vya ushindi katika michezo mbalimbali ambayo wameshindania katika mashindano ya kitaifa ya michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania Bara yaliyofanyika Mkoani Mtwara.
Jumapili, 27 Oktoba 2019
WIZARA YA ELIMU YAPONGEZWA KWA KUREJESHA MASHINDANO YA UMISAVUTA
Serikali imeipongeza Wizara
ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kutekeleza agizo la kurudisha mashindano ya
Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu (UMISAVUTA) huku ikiitaka kuhakikisha kuwa
michezo na Sanaa vinapewa kipaumbele katika mipango endelevu ya Wizara.
Pongezi hizo zimetolewa
Mkoani Mtwara. na Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo Dkt. Harrison
Mwakyembe kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
Kassim Mjaliwa wakati wa ufunguzi wa mashindano ya UMISAVUTA.
Mgeni rasmi Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akipiga mpira kuashiria uzinduzi rasmi wa
mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini katika viwanja vya
Nangwada Sijaona mkoani Mtwara.
Dkt. Mwakyembe amesema eneo
la michezo na Sanaa ni sehemu muhimu katika makuuzi ya watoto kwani yanajenga
na kuimarisha afya ya mwanadamu lakini pia yanaimarisha mahusiano baina ya
raia.
“Kwa sasa nchi imeonesha
mafanikio makubwa katika michezo hivyo ili Taifa lipate wataalamu na vipaji
sahihi katika michezo na Sanaa hatuna budi kuanza ngazi za awali za elimu, “alisema
Dkt. Mwakyembe.
Kwa upande wake Katibu Mkuu
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. leonard Akwilapo amesema Wizara
imejipanga vyema katika kuendeleza michezo ili kuongeza furaha kwa wananchi wa
Tanzania kwa kuziona timu zinashiriki na kushinda mashindano makubwa ya
kimataifa.
“Kama Wizara tunasema muda
wa kushiriki sasa umetosha tunataka kuwa washindani na mashindano haya ni
sehemu ya maandalizi ya kutekeleza azma hiyo,” alisema Katibu mkuu Akwilapo.
Mgeni rasmi Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akisalimiana
na washiriki wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu
nchini wakati wa ufunguzi wa mashindano hayo mkoani Mtwara.
Katibu Mkuu Akwilapo alisema
kupitia mashindano haya washiriki wataongeza ujuzi katika michezo na kuwa walimu ambao
wataimarisha michezo wakati watakapokuwa kazini huku wengine wakiendeleza
vipaji vyao na kuwa hazina ya Taifa kwa siku za usoni.
Michezo inayoshindaniwa ni
pamoja na mpira wa Pete, mpira wa miguu, wavu kikapu, riadha, mashindano ya
uchoraji, Sanaa za maonesho, ngoma pamoja na kwaya. Mingine ni pamoja na ile ya
kutengeneza zana za kufundishia na kujifunzia kwa lengo la kumjengea mwalimu
umahiri wa kuandaa na kutumia zana nzuri za kufundishia.
Baadhi ya Walimu Tarajali wakiingia katika uwanja wa Nangwanda mkoani Mtwara
wakati wa ufunguzi wa mashindano ya michezo na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini
mapema hii leo mkoani Mtwara.
Nae Kaimu Mkurugenzi
Msaidizi kutoka Seksheni ya Mafunzo ya Ualimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi
na Teknolojia Agusta Lupokela amesema mashindano hayo yaliyoanza Oktoba 25,
2019 yanatarajiwa kuhitimishwa Oktoba 31, 2019 na yameshirikisha Kanda saba
ambazo ni Kanda ya Kati, Kusini, Mashariki, Magharibi, Kanda ya Ziwa, Kaskazini
na Kusini ambazo zimeundwa kulingana na vyuo vya ualimu.
Juni 10, 2019 katika Viwanja
vya Nagwanda Sijaona mkoani Mtwara wakati Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania anafungua mashindano ya UMISSETA na UMITASHUMTA alitoa agizo kwa
Wizara ya Elimu kuhakikisha kuwa mashindano ya michezo na Sanaa kwa Vyuo vya
Ualimu yanarejeshwa.
Baadhi ya Walimu Tarajali wakiandamana kuelekea katika
uwanja wa Nangwanda mkoani Mtwara wakati wa ufunguzi wa mashindano ya michezo
na sanaa kwa vyuo vya ualimu nchini mapema hii leo mkoani Mtwara.
Ijumaa, 18 Oktoba 2019
Alhamisi, 17 Oktoba 2019
WAZIRI NDALICHAKO ATAKA MKUU WA SHULE KASANGEZI KUHAMISHWA
Waziri wa Elimu, Sayansi na
Teknolojia Prof Joyce Ndalichako ametilia shaka matumizi ya fedha za serikali
zaidi ya shilingi milioni mia tano zilizotolewa kwa ajili ya ujenzi na
ukarabati wa shule ya sekondari Kasangezi iliyopo wilayani Kasulu mkoani
Kigoma.
Akizungumza mara baada ya
kukagua utekelezaji wa mradi huo waziri Ndalichako amesema shule hiyo imepatiwa
zaidi ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya madarasa 4,
mabweni 4 yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 80 katika kila moja, matundu ya
vyoo 10, bwalo pamoja na ukarabati wa maabara.
Ndalichako amesema kazi iliyofanyika haiendani na fedha
iliyotolewa kutokana na miundombinu hiyo kujengwa chini ya Kiwango.
“Milango ya madarasa na hata
ya mabweni mmetengeneza kwa mbao laini tofauti na BOQ pamoja na kuwa laini ina
uwazi hii nataka itolewe, tazama sakafu imeshaharibika hapa hata mwaka
haujaisha mabweni mliambiwa ya watu themanini mmejenga ya watu sitini"
Waziri
wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akiangalia mlango wa
darasa ambao umetengenezwa kwa mbao laini kinyume cha taratibu katika shule ya
sekondari Kasangezi
Kufuatia hali hiyo ndalichako
ameagiza kuwa ujenzi wa mabweni urudiwe kwa kuzingatia BoQ na ameaguza ujenzi
huo uwe umekamilika ifikapo desemba.
"Nitakuja mwenyewe
mwezi wa kwanza kukagua kama hayo yatakuwa hayajatekelezwa mengine yatafuata,”
amesema waziri Ndalichako.
Aidha waziri Ndalichako
amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya
Kasulu Mhandisi Godfrey Kasekenya kumuondoa
mara moja shuleni hapo mkuu wa shule hiyo kwa kushindwa kusimamia vizuri kazi hiyo na hivyo kuisababishia
hasara serikali.
“Kwanza ujenzi wa mara ya
kwanza hata matofali hukununua ulichukua kwenye benki ya wananchi na tayari
nilikuwa nimeleta fedha sasa kwanini hukujiongeza hata ukarekebisha ofisi ya
Mkuu wa Shule ambayo iko katika hali isiyoridhisha vitu vingine ni kudhalilisha
Serikali, Mkurugenzi muahamishe huyu katika shule hii,” alisema waziri
Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na
Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako akikagua maendeleo ya ujenzi wa moja ya bweni katika shule ya
sekondari Kasangezi iliyoko Halmashauri ya wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma.
Waziri Ndalichako pia
ameitaka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na
Rushwa (TAKUKURU) wilayani Kasulu
kufuatilia muenendo wa upatikanaji wa madawati miamoja themanini
yaliyonunuliwa katika mradi huo kama yametimia na yamenunuliwa kwa kufuata
utaratibu.
Kwa upande wake Mkuu wa
Wilaya ya Kasulu Kanali Saimon Anange amekiri kuwepo uzembe katika kusimamia
miradi hiyo na kumuhakikishia waziri Ndalichako kuwa ofisi yake itafanyia kazi
maelekezo yote aliyoyatoa katika ziara hiyo.
Waziri wa Elimu Sayansi na
Teknolijia Prof. Joyce Ndalichako yupo mkoani Kigoma Kwa ziara ya Kikazi
akikagua miradi ya elimu inatekelezwa kupitia fedha za Programu ya lipa kwa
matokeo EP4R.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akikagua mlago wa darasa ambao umetumia mbao laini tofauti na maelekezo katika shule ya sekondari Kasangezi.
Jisajili kwenye:
Machapisho (Atom)