Ijumaa, 4 Desemba 2015



JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI
 
Coat of arms of Tanzania.png

KATAZO LA KUONGEZA ADA KWA SHULE ZISIZO ZA SERIKALI KWA MWAKA WA MASOMO 2016
 
Waraka wa Elimu Na. 4 wa Mwaka 2008 uliweka viwango vya ada vinavyotozwa katika shule za Msingi na Sekondari za Serikali na zile zisizo za serikali. Ada iliyowekwa kwa shule za kutwa zisizo za serikali ni Tsh. 150,000/= na shule za bweni Tsh. 380,000/= kwa mwaka kwa kila mwanafunzi. Aidha waraka huo ulielekeza kwamba ongezeko lolote la ada lazima lipate kibali cha Kamishna wa Elimu kabla ya kuanza kutumika.  
Hata hivyo imegundulika kuna baadhi ya shule zisizo za serikali zimekuwa zikiongeza ada kila mwaka pasipo kupata kibali cha Kamishna wa Elimu. Utamaduni huu wa kuongeza ada kila ifikapo mwishoni mwa mwaka umekuwa ukisababisha usumbufu mkubwa kwa wazazi/walezi na hata baadhi yao kushindwa kuendelea kusomesha vijana wao katika baadhi ya shule.
Kwa tangazo hili wamiliki wote wa shule zisizo za serikali wanaagizwa kufanya yafuatayo:
1.      Kutokuongeza gharama za uendeshaji wa shule zikiwemo ada kwa mwaka wa masomo unaoanzia mwezi Januari mwaka 2016 mpaka watakapopata maelekezo kutoka kwa Kamishna wa Elimu; wale ambao tayari wameongeza gharama na ada kwa mwaka wa masomo wa 2016 bila kibali cha Kamishna wa Elimu, Wizara haitambui ongezeko hilo kwa kuwa ni batili na hivyo zimefutwa.
2.      Ada zote kwa shule zisizo za serikali zitabaki kama zilivyokuwa zimeidhinishwa na Kamishna wa Elimu.
3.      Kuwasilisha taarifa kwa Msajili wa Shule aliyepo Idara ya Ithibati ya Shule inayoeleza kiasi cha ada na gharama  kinachotozwa kwa sasa (kabla ya mwaka wa masomo 2016) na tarehe shule ilipopata kibali kutoka kwa Kamishna wa Elimu kutoza kiwango hicho cha ada.  Taarifa hiyo ifike ndani ya wiki mbili kuanzia tarehe ya tangazo hili.
Wathibiti ubora wa shule waliopo sehemu mbalimbali nchini wanaagizwa kulifuatilia suala hili kwa karibu ili kila shule itekeleze agizo hili na kutoa taarifa zilizoelekezwa katika tangazo hili. Hatua za kinidhamu zitachukuliwa kwa wamiliki ambao hawatatekeleza maagizo haya.  
Aidha Wizara iko katika hatua za mwisho za utafiti na kuandaa mfumo wa kielektroniki wa kutambua gharama za kumsomesha mwanafunzi katika elimumsingi (elimu ya awali, msingi na sekondari) na hivyo wadau mbalimbali watoe ushirikiano kwa timu za wataalamu wanaofanya kazi hii ili kusaidia katika kuukamilisha mfumo na hatimaye kuwa na ada elekezi katika maeneo mbalimbali.
 
     
IMETOLEWA NA KATIBU MKUU
 
 
 




 
 

Jumatatu, 9 Novemba 2015

USHAURI WANGU KWA SERIKALI JUU YA UBORESHAJI WA MIUNDOMBINU YA ELIMU.


Josias Charles.

Baada ya mchakato mzima wa Kampeni kukamilisha na hatimaye Serikali kuundwa na Chama cha Mapinduzi kupitia kwa aliyekua mgombea wake wa Urais Mh. Dkt. John Pombe Magufuli tunapaswa kuungana wote na kutoa mawazo yenye lengo la kujenga uchumi wa Nchi Yetu.

Kumekuwepo na tatizo sugu la ukosefu ama kuwa na miundombinu mibovu mbalimbali ya Elimu Kama Madarasa, Maktaba, Mabweni, Maabara, Madawati nk. Ukosefu wa miundombinu hii umekwamisha ama kudumaza utoaji wa Elimu nchini.

Binafsi napenda kuishauri Serikali ya awamu ya Tano kuwekeza katika kuimarisha Elimu ya ufundi (VETA) na kuweka sera madhubuti itakayowabana wahitimu wa vyuo vya ufundi kujitolea kama sehemu yao ya mafunzo lakini pia ikiwa kama sehemu ya Kujitolea kujenga Taifa.


Mitaala ya Elimu ya ufundi Kama itatolewa kwa kipindi cha miaka miwili basi mwaka mmoja utumike kwa mafunzo darasani na mwaka mmoja kwa mafunzo kwa vitendo yaani( FIELD). Wanachuo wote wa VETA hata kama watasoma bure lakini wakatakiwa kufanya field kwa mwaka mzima watakua wameshiriki kwa kiwango kikubwa katika Ujenzi wa Taifa letu.

Mfano wanafunzi 10,000 wakichukua mafunzo ya ufundi kwa mwaka kwa uwiano tuu wa mafundi uashi 5000 na mafundi seremala 5000 kisha baada ya masomo ya mwaka mmoja wakaenda field kwa Mwaka mmoja kujenga Shule, hospitali, vituo vya afya, kutengeneza samani za ofisi tutapunguza gharama kiasi gani?

Nchi Yetu tuna raslimali nyingi ikiwemo raslimali watu lakini hatujaweza kuiendeleza. Naomba tuwekeze katika  kuendeleza raslimali tulizo nazo kwa manufaa ya Taifa letu.

Baada ya kuhitimu mafunzo ya miaka miwili tunao uwezo wa kuwatengenezea ajira vijana hawa na kuwawezesha mitaji inayotokana na shughuri zao katika jamii kwa kujitolea kwa mwaka mzima.

Hebu fikiria Serikali inaagiza samani za ofisi kiasi gani kwa mwaka? Pesa kiasi gani inatumika? Vipi kama vijana waliohitimu VETA mafunzo ya miaka miwili tena kwa kujitolea kujenga Taifa kwa mwaka mzima wakisajiriwa na  kampuni na kupata soko la uhakika toka Serikali na kuachana na uagizwaji wa samani za kichina tutapunguza tatizo la ajira kwa kiwango gani?

Vipi kama vijana walio soma ufundi uashi na kujitolea kujenga Taifa kwa mwaka mzima  wakapewa mikataba ya kujenga nyumba kama za NHC na Majengo mengine mengi tutapunguza tatizo la ajira kwa kiwango gani?

Tuna amini Serikali ya awamu ya Tano ipo makini na inalenga kila MTU afanye kazi kutimiza kauli mbiu ya "HAPA KAZI TU"

Mawaziri, Wabunge, na viongozi wote wa Serikali onyesheni ubunifu kulifanya Taifa letu lisonge mbele.

Kwa Leo inatosha.

HapaKaziTu

Jumanne, 6 Oktoba 2015

WATAALAM WA ELIMU KUTOKA SWEDEN WAFANYA ZIARA YA KIKAZI NCHINI

 
Wataalam wa Elimu kutoka Sweden ambao ni Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Juu nchini humo wameanza ziara ya kikazi nchini  kwa lengo la kujifunza mfumo wa elimu katika ngazi zote, mipango ya maendeleo pamoja na mageuzi mbalimbali ya Elimu.
 
Wataalam hao ni Wakaguzi wawili toka Kitengo cha Elimu ya Juu (Cecilia George na Petra Nord); Wakaguzi wawili kutoka Kitengo cha Elimu ya Sekondari (Eva Neihoff na Isabelle Nilsson); na Mkaguzi mmoja toka katika Kitengo cha Elimu ya Ufundi (Stefan Lofkvist).
 
Ujumbe huo umekutana na kufanya mazungumzo na watumishi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi wakiongozwa na Kamishna wa  Elimu nchini Prof. Eustella Bhalalusesa aliyemwakilisha Katibu Mkuu. Mazungumzo yao yalijikita zaidi katika kubadilishana uzoefu kuhusu mifumo ya elimu inayotumika katika nchi hizo mbili.
 
Aidha, wataalam hao katika ziara yao iliyoanza tarehe 5 hadi 7 Oktoba, 2015  wanatembelea taasisi zilizo chini ya Wizara zikiwemo; Taasisi ya Elimu Tanzania, Baraza la Mitihani, Tume ya Vyuo Vikuu, Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mamlaka ya Elimu ya Ufundi Stadi.  Pia watatembelea shule mbili za sekondari zenye kidato cha tano na cha sita kwa lengo la kuanzisha uhusiano wa kirafiki na shule kama hizo nchini Sweden.









Alhamisi, 1 Oktoba 2015

MAMLAKA YA ELIMU TANZANIA YATOA MKOPO WA SHILINGI BILIONI 3 KWA TAASISI YA ELIMU TANZANIA


 Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) imeingia makubaliano na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) ya Mkopo wa Shilingi Bilioni tatu. Mkopo huu umetolewa na TEA ili kuiwezesha Taasisi ya Elimu Tanzania Kufanya utafiti wa kubaini mahitaji ya maboresho kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali wa elimu, Kuandaa mitaala na  mihtasari ya masomo ya Elimu ya Msingi na Kuandika vitabu vya kiada kwa Darasa la III hadi la VI ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014.

Mkataba huo umetiwa saini tarehe 30 Septemba, 2015 na Joel Laurent Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TEA na Dkt. Leonard Akwilapo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TET na kushuhudiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Prof. Sifuni Mchome ambapo Mkopo  huo ni nafuu unatarajiwa kulipwa katika kipindi cha  miaka 6.
Matokeo tarajiwa kutokana na Mkopo huo ni Pamoja na uwepo wa Mitaala inayoendana na wakati na inayokidhi mahitaji ya sekta na shirikishi, uwepo wa mihutasari ya masomo itakayosambazwa katika kila shule kama ilivyoainishwa katika mitaala na uwepo wa vitabu vya kiada kulingana na mtaala ili kuepusha kuwa na vitabu vinavyotofautiana.


Aidha, ufadhili huu unalenga kuiongezea Taasisi ya Elimu Tanzania kutekeleza majukumu yake kwa njia yenye tija na kuongeza mapato ya Taasisi na utakuwa ni chachu ya kuboresha mfumo wa upatikanji wa vitabu sahihi kulingana na mitaala nchi nzima kupitia TIE.





MKUTANO WA KUTATHMINI SEKTA YA ELIMU NCHINI WAFANYIKA


Mkutano wa kutathmini Sekta ya Elimu nchini kwa mwaka 2015 umefanyika jijini Dar es Salaam katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere kuanzia tarehe 28 hadi 30 Septemba, 2015 ambapo Wadau mbalimbali wa Elimu ikiwa ni pamoja na Serikali, Washirika wa Maendeleo na Taasisi Zisizokuwa za Serikali zinazojihusisha na Elimu walikutana na kujadiliana kuhusu mafanikio, changamoto na mikakati ya kuboresha elimu nchini.

 Mkutano huo ambao ulifanyika sambamba na Maonesho ya Matumizi ya TEHAMA katika Elimu ya Msingi ulifunguliwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Profesa Sifuni Mchome ambae aliwataka washiriki wa mkutano huo kujadili kwa kina namna bora ya kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika Sekta ya Elimu nchini.









Mkutano huo umefungwa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anaeshughulikia Elimu Mhe. Kassimu Majaliwa ambae alisema ushirikiano ulioko kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo unasaidia kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika kuimarisha mahudhurio ya shule, kugharamia Elimu  Msingi  kwa wanafunzi wote, kupatikana kwa walimu wa masomo ya Sayansi na Hisabati katika Elimu Msingi.




Jumatano, 23 Septemba 2015

Waziri Kawambwa afanya ziara AIMS – Tanzania


Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dkt. Shukuru Kawambwa mwishoni mwa wiki alitembelea Taasisi ya  African  Institute for  Mathematical  Sciences - Next Einstein Initiative (AIMS-NEI) kampasi ya Tanzania na kuzungumza na viongozi na wanafunzi wa Shahada ya Uzamili katika masomo ya  Hisabati na Sayansi kwa mwaka 2015/16. Taasisi ya AIMS hapa nchini imeanzisha kampasi yake Bagamoyo, mkoani Pwani ambapo hivi sasa inatumia kwa muda majengo ya Alpha Zulu Villa na baadaye itatumia majengo ya Old Boma na Datoo yaliyoko Bagamoyo mjini baada ya kufanyiwa ukarabati.
Wanafunzi 45 kutoka nchi mbalimbali za Afrika wamedahiliwa kuanza masomo katika taasisi ya AIMS – Tanzania kwa mwaka 2015/16 wakiwemo Watanzania 17 na wengine wanatoka nchi za Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Cameroon, DRC, Msumbiji, Nigeria, Zimbabwe, Afrika Kusini, Sudani na mmoja anatoka Uingereza.
Kuanza kwa mafunzo hayo ni jitihada za Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete kuhakikisha kuwa Taifa linakuwa na wataalam wa kutosha katika Nyanja za Hisabati na Sayansi. Mheshimiwa Rais alikutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa taasisi hiyo alipokuwa ziarani nchini Canada mwishoni mwa mwaka juzi.