Jumanne, 24 Aprili 2018

NAIBU WAZIRI OLE NASHA AFUNGA MKUTANO WA BARAZA LA WAFANYAKAZI


·        ASISITIZA UWAJIBIKAJI MAHALI PA KAZI


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amewataka Wafanyakazi wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa kufuata kanuni, taratibu  ikiwa ni pamoja na kuwa na ushirikiano miongoni mwao ili kufikia malengo yaliyowekwa na Serikali.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. William Ole Nasha akizungumza na wajumbe wa Mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Mkutano huo wa siku mbili umehitimishwa leo  Mkoani Morogoro.

Naibu Waziri huyo ametoa kauli hiyo wakati akifunga mkutano wa 25 wa baraza la wafanyakazi ambapo amesisitiza kuwa mkutano huo upo kisheria na kuwa unasaidia kuainisha haki za Wafanyakazi pamoja na Wajibu wao katika utumishi wa Umma.
Viongozi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wakiwa wameshikana mikono kuonesha umoja wao wakati wa  kufunga Mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika mkoani Morogoro.

Mheshimiwa Ole Nasha amewataka Wafanyakazi hao kuhakikisha Elimu inayotolewa hapa nchini inakuwa bora kwa kuwa Elimu ndiyo msingi pekee wa kufikia Uchumi wa viwanda.
Wajumbe wa Mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara  wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia wakati wa kufunga Mkutano wa baraza la Wafanyakazi mkoani Mkoani Morogoro.

Pia amewataka makatibu wakuu wa Wizara hiyo kushughulikia kikamilifu maazimio yote yalifikiwa katika mkutano huo wa siku mbili wa baraza la Wafanyakazi kabla ya kufanyika kwa mkutano mwingine wa baraza hilo unaotarajiwa kufanyika mapema Oktoba mwaka huu.


Kauli mbiu ya mkutano wa baraza hilo inasema: “Elimu Jumuishi, Sayansi na Teknolojia ni msingi wa Maendeleo, Endelevu ya Uchumi wa viwanda Tanzania.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. James Mdoe akizungumza na wajumbe wa mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (hawapo pichani), wakati wa kufunga mkutano huo uliofanyika Mkoani Morogoro amabye amesisitiza kuwa jukumu la Wizara hiyo ni kuweka viwango vya ubora vya Elimu.

Jumatatu, 23 Aprili 2018

BARAZA LA WAFANYAKAZI WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA WAKUTANA MKOANI MOROGORO


·         WAJADILIANA NAMNA YA KUFIKIA UCHUMI WA VIWANDA

Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Clifford Tandari ameishauri Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kusomesha vijana wengi katika fani ya ufundi ili kupata wataalamu watakaofanya kazi katika viwanda ili kuendana na sera ya serikali ya awamu ya Tano ya kuwa na uchumi wa Kati na wa viwanda ifikapo mwaka 2015.

Tandari amesema hayo Mkoani Morogoro wakati akifungua Mkutano wa 25 wa Baraza la wafanyakazi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na kusisitiza kuwa Serikali inayoongozwa na Rais John Pombe Magufuli imeweka misingi imara itakayowezesha kila Mtanzania kupata Elimu bora na yenye tija kwa Taifa ili kufikia malengo ya Taifa.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Clifford Tandari akizungumza na wajumbe wa Mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mkoani Morogoro. 

Akizungumza na baraza hilo la Wafanyakazi Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo amesema kufanyika kwa baraza hilo ni matokeo ya utekelezaji wa Sera ya kuwashirikisha wafanyakazi katika uongozi wa pamoja mahali pa kazi na kuwa mkutano huo pia utapitia na kujadili utekelezaji wa bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mwaka 2017/18 na mwelekeo wa bajeti ya mwaka 2018/19.


kwa upande wake Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo Gerald Mweli amesema Baraza hilo ndio chombo cha juu kabisa cha sheria ya majadiliano kazini kinachojumuisha wafanyakazi wote kujadiliana kwa pamoja mafanikio, changamoto na kuweka mipango ya namna ya kutatua changamoto zinazowakabili.
Viongozi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wakiwa wameshikana mikono kuonesha umoja wao wakati wa Mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo.

Mkutano huo wa siku mbili ulioanza leo utakamalizika kesho ukiwa na kauli mbiu inayosema “Elimu Jumuishi, Sayansi na Teknolojia ni Msingi wa maendeleo Endelevu ya Uchumi wa Viwanda Tanzania".

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo akizungumza na wajumbe wa mkutano wa 25 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (hawapo pichani), ambapo amesisitiza suala la Umoja, Upendo na ushirikiano mahali pa kazi. (hawapo pichani)

Jumamosi, 21 Aprili 2018

KIBAHA SEKONDARI KINARA WA INSHA, SHULE NYINGINE ZATAKIWA KUJIFUNZA KUTOKA KWAO


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu amezitaka Shule za Sekondari nchini ambazo zimekuwa zikishindwa katika mashindano ya insha za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za kusini mwa Afrika SADC kujifunza kupitia shule ambazo zimekuwa zikifanya vizuri.

Dkt. Semakafu ameyasema hayo mjini Dodoma wa wakati hafla ya kuwazawadia washindi wa insha hizo kwa mwaka 2017 ambapo amesema ni vema kukawa na  utaratibu wa kuzikutanisha shule hizo mara moja kwa mwaka ili kujadiliana mbinu mbalimbali zitakazowawezesha kufanya vizuri katika mashindano hayo.

Semakafu amesema ushindi huu ni dhahiri kuwa Elimu  inayotolewa nchini  ni Elimu bora na diyo maana wanafunzi wa kitanzania wameweza kushinda tuzo na kuongoza  katika ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Nchi za kusini mwa Afrika.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu akimkabidhi zawadi ya fedha mshindi wa Jumla wa Insha za Jumuiya ya Afrika Mashariki Michael Msafiri kutoka Shule ya Sekondari Kibaha iliyopo Mkoni Pwani.

Afisa Elimu Mkuu wa sekretaieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki James Otieno kauli aliunga mkono  kauli hiyo kwa kusema kuwa Elimu nchini Tanzania ni bora kwa Nchi za ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwasababu wanafunzi kutoka Tanzania wamekuwa wakifanya vizuri katika mashindano hayo.


Kwa upande wake Mwanafunzi bora wa mashindano ya insha hizo kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) Michael Msafiri kutoka Shule ya Sekondari Kibaha ndiye atakuwa mwakilishi wa washindi wote katika Mkutano Mkuu wa Wakuu wa nchi za Jumuiya hiyo utakaofanyika baadae mwaka huu mkoani Arusha.

Kaimu Mratibu wa mashindano hayo Salum Salum kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia amesema mshindano haya huanza mara baada ya kikao cha wakuu wa Nchi wanachama kutoa azimio la mwaka na kwamba mada zinazoshindanishwa huzingatia makubaliano ya wakuu wa nchi.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu akikabidhi zawadi kwa mwanafunzi Anord Matungwa kutoka shule ya Sekondari Kagemu mkoani Kagera aliyeshinda kutoka kundi la shule zenye mazingira magumu.

Jumatano, 18 Aprili 2018

WAZIRI NDALICHAKO AZINDUA JENGO LA GHOROFA 10 DIT • AITAKA TAASISI HIYO KUTUNZA MIUNDOMBINU

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako leo amezindua Jengo la kufundishia la ghorofa 10 katika Taasisi ya Teknolojia  Dar es salaam- DIT – Teaching Tower Complex.

Akizungumza mara baada ya kutembelea na kukagua jengo hilo amesema kuzinduliwa kwa jengo hilo kutasaidia kuongeza udahili wa wanafunzi kwa kuwa jengo hilo linauwezo wa kuchukua wanafunzi zaidia ya Mia Tisa kwa mara moja.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako azindua Jengo la ghorofa 10 DIT na ameitaka Taasisi hiyo kutunza miundombinu kwa kuwa imejengwa kwa gharama kubwa na fedha zilizotumika ni za ndani.

Ndalichako amesema kuwa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuondoa upungufu wa kero ya Miundombinu iliyokuwa inaikabili DIT kwa muda mrefu ambapo jengo hilo limeigharimu Serikali zaidi ya Bilioni Tisa ambazo ni fedha za ndani.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akizungumza  na watendaji pamoja na wanafunzi wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam(hawapo pichani) wakati wa kuzindua  Jengo la kufundishia la ghorofa 10.

Kwa upande wake Mkuu wa chuo cha DIT Profesa Preskedis Ndomba ameishukuru Serikali kwa uwekezaji huo  uliofanywa na Serikali ambapo amemhakikishia Waziri wa Elimu kuwa  watailinda miundombinu hiyo ili iweze kutumika kwa muda mrefu kwa lengo la kuongeza tija ya kuwepo kwa wataalamu wa fani mbalimbali hapa nchini


Baadhi ya Watumishi wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam –DIT -wakisikiliza kwa makini hotuba ya Prof Joyce Ndalichako wakati wa kuzindua Jengo la kufundishia la ghorofa 10

Jumanne, 17 Aprili 2018


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA


Anuani ya simu “ELIMU”
Simu: 026  296 35 33
Baruapepe:info@moe.go.tz
Tovuti: www.moe.go.tz



Chuo cha Masomo ya  Biashara na Sheria,
Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Jengo Na. 10,
S. L. P. 10,
40479 DODOMA.           




Tarehe: 17 Aprili, 2018
TAARIFA KWA UMMA
KUHUSU UFANISI KATIKA USIMAMIZI WA UREJESHAJI WA MIKOPO NA UKUSANYAJI WA MADENI NA MIKOPO YA WANAFUNZI WA ELIMU YA JUU

A.    UTANGULIZI
Ndugu Waandishi wa Habari, napenda kutumia nafasi hii kuishukuru kwa dhati Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa kufanya ukaguzi huu ambao umeainisha mafanikio na changamoto mbalimbali zilizopo katika Usimamizi na urejeshwaji wa Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu. Pia namshukuru CAG kwa kuibua changamoto ya kuchelewa kwa mradi wa ujenzi katika Chuo cha Ualimu Ndala pamoja na ushauri wake na mapendekezo kwa ujumla aliyoyatoa yenye lengo la kuhakikisha ufanisi katika usimamizi na matumizi ya fedha za umma kwa Wizara na Taasisi zote zilizo chini ya Wizara yangu, unaimarika.

Jumatatu, 16 Aprili 2018

SERIKALI YAAHIDI KUTATUA CHANGAMOTO KWA WANAFUNZI WENYE UZIWI


Waziri wa Elimu, Sayasni na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amekihakikishia Chama cha walimu Viziwi kuwa Serikali iko tayari kusikiliza na kujua changamoto zinazowakabili wanafunzi wenye uziwi ili hatua madhubuti ziweze kuchukuliwa.

Waziri Ndalichako amesema hayo leo mkoani Dodoma alipokutana na kufanya mazungumzo na walimu wenye Uziwi ambapo amewaeleza kuwa hajafurahishwa na matokeo ya kidato cha Nne ya shule ya Sekondari Njombe na kubainisha kuwa ni vyema changamoto zikaainishwa ili hatua ziweze kuchukuliwa.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako  akisalimiana na Mkurugenzi wa Chama cha Walimu wenye uziwi Tanzania Karim Bakari.

Kwa upande wake mratibu wa chama hicho cha Walimu Viziwi Francis Mbisso ameiomba Serikali kutoa semina kwa walimu wanaofundisha wanafunzi Viziwi ili  walimu waweze kuelewa saikolojia ya wanafunzi pale wanapowafundisha, lakini pia kuwe  na wigo mpana  wa mafunzo ya ufundi kwa wanafunzi hao  badala ya kuwalazimisha kusoma masomo ya darasani.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akutana na kufanya mazungumzo na Chama cha Walimu wenye Uziwi Tanzania. Mazungumzo hayo yanalenga kutataua changamoto zinazowakabili wanafunzi wenye uziwi.

Mbisso ameshauri kuwepo kwa mtaala wa lugha ya alama pekee utakaowasiadi wanafunzi wenye uziwi kuelewa kwa uarahisi masomo yao wanapokuwa darasani ikiwa ni pamoja na kuongeza muda ya kipindi darasani ukilinganisha na muda wanaotumia wanafunzi wa kawaida.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Ave Maria Semakafu akisalimiana na Mwalimu Theresia Nkwera mwenye uziwi, ambaye alishiriki majadiliano ya pamoja yenye lengo la kutatua changamoto zinazowakabili wanafunzi wenye uziwi.

Jumatatu, 9 Aprili 2018

UJENZI CHUO CHA UFUNDI NA MAFUNZO YA UFUNDI STADI CHA MKOA WA KAGERA KUANZA OKTOBA 2018


Mkuu wa Wilaya ya Bukoba Deodutus Kinawiro amesema tayari Serikali imekamilisha ujenzi wa Miundombinu muhimu ya barabara na umeme katika Kijiji cha Burugo ambapo Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi stadi cha Mkoa wa Kagera kinatarajiwa kujengwa.

Kinawiro amesema hivi sasa Mkoa upo katika kukamilisha miundombinu ya maji  na kuwa tayari suala hilo limewekwa kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2018/19.
Mwakilishi wa Kampuni ya ujenzi ya Kichina (CHINA QIYUAN ENGINEERING CORPORATION) Yang Tao akiwapitisha Watendaji wa Mkoa wa Kagera katika Michoro ambayo wameiandaa kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi cha Mkoa wa Kagera.


Kukamilika kwa Miundombinu hiyo kunatoa fursa ya kuanza kwa ujenzi wa chuo hicho ambapo Ujumbe wa timu ya Wataalam kutoka Kampuni ya ujenzi ya Kichina (CHINA QIYUAN ENGINEERING CORPORATION) inayotarajiwa kusimamia ujenzi wa Chuo hicho umetembelea eneo hilo ambapo umekiri kuridhishwa na hatua hizo ambazo serikali imezitekeleza.


Kwa upande wake Meneja Mkuu Msaidizi wa Kampuni hiyo Fang Kefeng amesema uwepo wa barabara, umeme na maji katika eneo la mradi utawawezesha kutekeleza ujenzi bila kikwazo  na kuwa tayari wameandaa michoro kwa ajili ya ujenzi wa chuo hicho na kwamba mradi utaanza mara baada Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kuridhia michoro iliyoandaliwa kwa ajili ya Chuo hicho. 
Kaimu Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Mhandisi Enock Kayani akifafanua jambo kwa timu ya Wataalam kutoka Kampuni ya Kichina ya Ujenzi (CHINA QIYUAN ENGINEERING CORPORATION) wakati walipotembelea eneo la Mradi  katika Kijiji cha Burugo  Halmashauri ya Wilaya Bukoba Mkoani Kagera.

Kaimu Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhandisi Enock Kayani amesema Mradi huo unatarajiwa kuanza mwezi Oktoba Mwaka huu mara baada ya Kampuni hiyo kufanya maboresho yaliyotolewa na Wizara katika michoro yao na kwamba mradi mzima utagharimu fedha za Kitanzania takribani bilioni 22 na utafanyika kwa awamu mbili.
Ujumbe wa Timu ya Wataalam kutoka Kampuni ya Ujenzi ya Kichina ilipotembelea  shule ya Sekondari ya wavulana Ihungo inayojengwa upya na Serikali mara baada ya kuharibiwa vibaya na tetemekeo la ardhi lililotokea Septemba 10, 2016. Kampuni hiyo ilitembelea shule hiyo kwa lengo la kujifunza  na kuona aina ya ujenzi wa Miundombinu inayotekelezwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.