Jumamosi, 9 Machi 2019

WIZARA YA ELIMU YAGAWA KOMPYUTA 300 KWA VYUO VYA ELIMU VYA UMMA


Kiasi Cha Shilingi bilioni 1.2 kimetumika  kununulia vifaa vya TEHAMA kwa ajili ya vyuo vya ualimu vya umma  18, kwa  lengo la   kuimarisha ujifunzaji na ufundishaji katika vyuo hivyo ili  kuzalisha walimu bora  na wanaoendana na ulimwengu wa Teknolojia.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Mkuu Profesa James Mdoe kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia wakati wa halfa ya utoaji vifaa mbalimbali vya TEHAMA zikiwemo Kompyuta 300, UPS 300 na Projector 100 kwa ajili  vyuo hivyo vya Ualimu.

Kaimu Katibu Mkuu Prof. James Mdoe akigawa vifaa vya Tehama kwa Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Umma nchini kwa lengo la kuboresha elimu ya Ualimu, hafla hiyo imefanyikia mkoani Dodoma.

Katika hotuba yake, Profesa Mdoe amesema serikali ya Tanzania inawashukuru  washiriki wa maendeleo ambao ni serikali ya CANADA kwa kufadhili mradi wa kuendeleza na kuboresha Elimu ya Ualimu  (TESP ) kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Profesa Mdoe pia amewaasa Wakuu wa Vyuo kutumia vifaa hivyo kwa malengo yaliyo kusudiwa na ametoa onyo kwa Wakuu wa vyuo wote wanauhujumu jitihada za serikali za kuboresha miundombinu ya vyuo vya Ualimu kuacha mara moja tabia hiyo na kuwataka watumishi wote  kutanguliza maslahi ya Taifa ikiwa ni pamoja na kuacha kufanya kazi kwa mazoea.

 
Vifaa mbalimbali vya Tehama zikiwemo Kompyuta, UPS na Projector kwa ajili ya kugawiwa kwenye Vyuo vya Ualimu vya umma 18.

“Nipende kuwasihi watumishi wote wa Wizara ya Elimu na hasa Idara ya manunuzi   kuzingatia Sheria, Taratibu na Kanuni  wakati wa kutekeleza majukumu."

Vyuo vya Ualimu vya Umma ambavyo vimepata vifaa hivyo ni pamoja na Dawaka, Ilonga, Mandaka, Mhonda, Murutunguru, Mamire, Ndala, Singachini, Shinyanga na Vikindu.

Kaimu Katibu Mkuu Prof. James Mdoe akizungumza na watumishi wa Wizara (hawapo) pichani wakati wa hafla ya kugawa vifaa vya Tehema mkoani Dodoma.


Vyuo vingine ni Patandi, Tarime, Mpuguso, Sumbawanga, Mpwapwa, Tukuyu , Morogoro na Korogwe.




Kwa upande wake Mwenyekiti wa Wakuu wa Vyuo vya Ualimu nchini Augustino Sahili ameiomba serikali kuharakisha kukamilisha mpango wa kuunganisha vyuo vyote vya Ualimu vya umma na Mkongo wa Taifa.
Baadhi ya Wakuu wa Vyuo vya Ualimu wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi ambaye ni Kaimu Katibu Mkuu Profesa James Mdoe (hayupo pichani) wakati wa ugawaji wa vifaa vya Tehama kwa Vyuo vya Ualimu. Hafla hiyo imefanyikia mkoani Dodoma.

Alhamisi, 7 Machi 2019

WAZIRI NDALICHAKO ASEMA SAYANSI NA TEKNOLOJIA NI MUHIMU KATIKA UKUAJI WA UCHUMI


Serikali imewataka  wabunifu nchini kujikita katika  kuangalia shughuli za ambazo zinafanyika katika mazingira yao na wabuni jinsi ya kuzirahisisha kwa kutumia Sayansi na kiteknolojia ili kuchangia katika ukuaji wa uchumi nchini.
Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Ilboru Maximillian Masesa akitoa maelezo kwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako  juu ya kifaa cha kubaini wanafunzi ambao wanatumia simu shuleni alichobuni.

Kauli hiyo ya serikali imetolewa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako katika kilele cha Mashindano ya kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu mjini Dodoma. Waziri Ndalichako  pia aliongeza kuwa eneo la Sayansi na Teknolojia ni muhimu kwa taifa na likitumika vyema litasaidia  kuongeza uzalishaji na Kurahisisha utekelezaji wa mambo mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

“Kwa muda mrefu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekuwa ikisimamia zaidi Elimu kuliko masuala ya Sayansi na ubunifu hivyo ni vyema wabunifu waendelee kujitokeza  zaidi na wajikitike katika  ikubuni mbinu za kurahisisha mifumo ya shughuli mbalimbali za kijamii  ikiwemo Kilimo, ufugaji na njia bora za upatikanaji wa maji”, alisema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiangalia ubunifu wa injini ya Ndege  uliofanywa na Emmanuel Chibula kutoka Musoma, Mkoani Mara wakati wa kilele cha mashindano ya kitaifa ya sayansi, teknolojia na Ubunifu yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Mkuu Profesa James Mdoe amesema  lengo  la Mashindano hayo yaliyohusisha wabunifu kutoka  ngazi mbali za Elimu ni kuibua ubunifu, umahiri, kuchochea ugunduzi kwa lengo la kukuza matumizi ya Sayansi na Teknolojia katika maendeleo.
Wanafunzi mbalimbali wa Shule za Msingi na baadhi ya Wananchi wakifuatilia Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu yaliyofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere.

Mashindano hayo  yalifunguliwa rasmi na Naibu Waziri Mhe. William Ole Nasha Machi 5, 2019 na leo yamefikia kilele ambapo washindi mbalimbali walipata zawadi za fedha na kutunukiwa vyeti.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na washiriki mbalimbali hawapo pichani wakati wa kufunga mashindano ya kitaifa ya kitaifa ya sayansi, teknolojia na Ubunifu yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Kauli mbiu ya mashindano hayo kwa mwaka huu ni " kukuza ujuzi na ubunifu kwa uchumi wa viwanda".
Wanafunzi wa Chuo cha Usafirishaji nchini NIT wabuni gari lisilotumia injini, na badala yake linatumia umeme kuendesha mifumo yake. Pichani Waziri akiwa kwenye gari hilo akipewa maelezo ya namna gari hilo linavyofanya kazi.

OLE NASHA AMUAGIZA KATIBU MKUU WIZARA YA ELIMU KUFUATILIA UKARABATI SHULE YA SEKONDARI KIBAHA


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amemuagiza Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dkt. Leornald Akwilapo kufika katika shule ya Sekondari Kibaha kujionea jinsi kazi ya ukarabati ilivyo chini ya kiwango ili achukue hatua zinazostahili.

Naibu Waziri Ole Nasha ametoa agizo hilo alipofanya ziara katika shule ya sekondari Kibaha kukagua maendeleo ya utekelezaji wa miradi ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu katika shule hiyo.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua maendeleo ya ujenzi wa mabweni mawili katika shule ya Sekondari Kwala iliyopo katika Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani yanayojengwa na wizara kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) 
Kiongozi huyo amesema hajaridhishwa kazi  inavyoendelea kwani hailingani na fedha ambayo tayari imeshalipwa na serikali tangu mwaka juzi walipokabidhiwa. Kazi  hii ya ya ukarabati wa jingo la bweni na jingo la maabara ya fizikia katika shule hiyo inayotekelezwa na Wakala wa Majengo Nchini (TBA).

“Wakala huyu alipaswa kuwa amekamilisha ukarabati na ujenzi wa miundombinu jumla 31 katika shule hii, lakini mpaka sasa amekarabati majengo mawili tu na ukiyaangalia  yako chini ya viwango huku akiwa ametumia zaidi ya kiasi cha shilingi milioni 400,” Amesema Ole Nasha.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akikagua vifaa vya ujenzi wa mabweni katika shule ya Sekondari Kwala iliyopo katika Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani baada ya kutoridhishwa na taarifa ya ujenzi iliyotolewa kwake na Mkuu wa shule hiyo kuhusu vifaa vilivyotumika katika mradi huo.
Katika hatua nyingine Naibu Waziri amewapongeza wanafunzi wa Shule ya Sekondari Kibaha kwa kufanya vizuri katika mitihani ya kitaifa bila kujali changamoto walizonazo za miundombinu ya mabweni, madarasa pamoja na vyoo.

“Wanafunzi hawa wanachukua mchepuo wa sayansi wanahitaji kujiongezea maarifa sasa nimeambiwa shule hii ina kompyuta nne tu hivyo namuagiza Katibu Mkuu alete kompyuta 50 shuleni hapa ziweze kuwasaidia wanafunzi” alisisitiza Naibu Waziri

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akijadiliana na baadhi ya walimu na wajenzi katika shule ya sekondari ya Kwala ambapo wizara inatekeleza mradi wa ujenzi wa mabweni mawili kwa ajili ya wanafunzi wa shule hiyo.
Kwa upande wake Kaka Mkuu wa Shule hiyo Jonas Baraka amemweleza Naibu Waziri kuwa wamekuwa wakikutana na changamoto nyingi za miundombinu kwani hata ile iliyokarabatiwa kwani vyoo havipitishi maji, ubovu wa vitasa vya milango pamoja na ukosefu wa maji katika baadhi ya maeneo ya shule.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza na wazazi, wanafunzi, walimu pamoja na wanakijiji wa Kwala mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa mabweni mawili katika shule ya Sekondari Kwala na kuwata wanakijiji hao kuchangia katika mradi huo ili ukamilike mapema.
Katika hatua nyingine Naibu Waziri ameonyeshwa kutoridhishwa na matumizi ya zaidi ya shilingili milioni mia moja na hamsini ziliotolewa na serikali kwa ajili ya ujenzi wa mabweni mawili katika sekondari ya Kwala na kumuagiza Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Asumpter Mshama kutuma vyombo vya ulinzi na usalama kwenda kukagua mchakato mzima uliotumika katika ujenzi wa mabweni mawili ya shule hiyo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akitembelea maeneo mbalimbali ya shule ya sekondari Kibaha akiwa ameambatana na Mbunge wa Kibaha Mjini Mhe. Silyvestry Koka na wanafunzi wa shule hiyo.
Naibu Waziri Ole Nasha yupo katika ziara ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa miradi ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya shule inayofadhiliwa na Wizara ya Elimu kupitia Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R) katika Mkoa wa Pwani katika wilaya za Kibaha, Kisarawe na Rufiji.