Jumatano, 22 Mei 2019

NDALICHAKO AVUTIWA NA WANAFUNZI WA SHULE YA DAR ES SALAAM INTERNATIONAL ACADEMY KWA UWEZO WA KUJIAMINI

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako ameupongeza Uongozi wa shule ya Dar es Salaam International Academy kwa kuwajengea uwezo na kuona umuhimu wa kuwafundisha na kuwapa nafasi wanafunzi kujifunza wenyewe.


Prof. Ndalichako ametoa pongezi hizo jijini Dar es Salaam aliposhiriki katika maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano katika shule hiyo ambapo amesema wanafunzi hao wamefundishwa kutafuta taarifa mbalimbali kutokana na mada walizopewa.

“Nimefurahi kuona wanafunzi wa darasa la tano wanaonesha ubunifu katika kuangalia matatizo ya jamii kwani hata mada walizoangalia zinaendana na hali halisi ya sasa ambayo serikali imekuwa ikiwekea msisitizo kama masuala ya jinsia, magonjwa ya homa ya ini na Ebola, dawa za kulevya pamoja na Teknolojia,” amesema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wanafunzi, walimu na wazazi (Hawapo Pichani) wa shule ya Dar es Salaam International Academy wakati wa maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano.
Waziri Ndalichako amesema katika kutafuta taarifa wanafunzi hao wameonyesha vipaji vya hali ya juu wakati wa kuandaa mada za maonyesho kwani wametumia mitandao pamoja na kuwahoji watu waliowaona muhimu kuwapatia taarifa zilizowawezesha kukamilisha mada zao kwa ajili ya maonyesho hayo.  

Aidha, Waziri Ndalichako ametoa wito kwa walimu kuwawezesha na kuwapa nafasi wanafunzi katika kuwa na ubunifu, kujiamini na kuweza kutafuta taarifa mbalimbali katika kujifunza kwani wanafunzi wa kitanzania wana uwezo wa kufanya mambo makubwa sana lakini wanakwama kutokana na kushindwa kujiamini na uoga wakati shuleni ni sehemu ambayo vipaji hivyo vinaweza kuendelezwa.

“Suala la kujiamini ni changamoto kubwa kwa watanzania wengi, wana uwezo, akili na vipaji lakini wanakuwa hawajiamini hili ni tatizo,  kwa hiyo tuendelee kuwa na maonyesho kama haya ambayo yatawajengea wanafunzi wetu uwezo, kujiamini, kuonyesha yale wanayoweza na kutoogopa kusema mbele za watu,” amesisitiza  Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na kusalimiana na walimu wa shule ya Dar es Salaam International Academy wakati wa maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano.
Aidha, Waziri Ndalichako amesema hata katika shule za serikali maonyesho kama hayo yanafanyika  katika ngazi ya shule za sekondari ambayo yanaanza katika ngazi ya shule, wilaya na kilele inakuwa katika ngazi ya Kitaifa hata hivyo wameahidi kuangalia namna ya kuanza kushirikisha wanafunzi wa shule za msingi kwani kufanya hivyo inawezesha kuwaandaa wabunifu tangu wakiwa katika umri mdogo.

Akizungmzia mkakati wa serikali wa kutambua na kukuza ubunifu nchini Waziri Ndalichako amesema kupitia Tume ya Sayansi na Teknolojia inazo atamizi ambazo zinatumika kuendeleza ubunifu lakini pia imeona si rahisi kila mtu kuweza kufika katika Tume hiyo hivyo imeanza utaratibu wa kuanzisha katika ngazi za Halmashauri ambapo mwaka huu mwongozo umetoka wa kuangalia namna gani wabunifu wakitambulika wanaweza kuendelezwa.

“Pia katika vyuo vikuu vyetu kuna hatamizi kwa mfano Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Nelson Mandela kuna atamizi ambazo zinafanya vizuri sana na wao wamejikita katika mazao na kuangalia vitu ambavyo vinaweza kuweka sumu katika mazao lengo ni kuhakikisha tunaongeza wigo ili vipaji wa watanzania viweze kuendelezwa,” amesema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiangalia kipeperushi kilichotengenezwa na wanafunzi Dar es Salaam International Academy wakati wa maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano.
Naye Mkuu wa Shule hiyo, Fawzya Hirji amesema shule hiyo imejipanga kuhakikisha kunakuwa na ushirikiano  kati ya walimu, wanafunzi na wazazi katika kuwawezesha wanafunzi hao kuwa na uwezo wa ubunifu, kujiamini na kutumia mitandao katika kutafuta taarifa mbalimbali zinazowapatia maarifa ya kujua mambo mbalimbali duniani.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisikiliza maelezo kutoka kwa wanafunzi wa shule ya Dar es Salaam International Academy wakati wa maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano.

Jumatano, 8 Mei 2019

WAZIRI NDALICHAKO AIPONGEZA UDSM KWA KUTENGA BILIONI MOJA ZA KUENDELEZA UTAFITI


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako ameupongeza uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kutenga kiasi cha shilingi bilioni moja katika bajeti yake ya mwaka 2019/20 kwa ajili ya kutoa fursa kwa  wahadhiri na wanafunzi kendeleza tafiti

Waziri Ndalichako ametoa pongezi hizo jijini Dar es Salaam wakati akifunga maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambapo amesema utafiti una mchango katika ukuaji wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akihutubia washiriki wa maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakati wa kufunga Wiki hiyo jijini Dar es Salaam

Prof. Ndalichako amesema serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda lengo likiwa kuhakikisha kunakuwa na viwanda ambavyo vinatumika kuzalisha bidhaa na kutoa huduma zitakazotosheleza jamii ya Kitanzania na kusaidia kuongeza ajira kwa vijana.

“Serikali kupitia Tume ya Sayansi na Teknolojia ilizipatia Taasisi nane za Tanzania Bara kiasi cha shilingi bilioni tatu na milioni mia mbili wakati upande wa Zanzibari shilingi milioni 960 zilitolewa kwa ajili ya utafiti, Taasisi hizo zilishinda uandishi wa tungo za miradi ya uboreshaji wa miundombinu ambayo ina uwezo wa kutoa mchango madhubuti katika Dira ya nchi yetu ya uendeshaji wa viwanda kwa lengo la kuimarisha uchumi wa nchi yetu” amesisitiza Waziri Ndalichako.

Akizungumzia Wiki ya Utafiti Waziri Ndalichako amesema inawapa wadau wa utafiti na ubunifu jukwaa la kufahamu aina za shughuli za utafiti zinazofanyika; sehemu gani kuna mapengo na changamoto; na mikakati gani ya kimipango inahitajika ili kuziba mapengo pamoja na kutatua changamoto zilizobainika.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikabidhi tunzo kwa washindi wa auandishi wa miradi ya tafiti wakati wa kufunga  maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. 

"Kama taifa, tuna wajibu mkubwa na fursa nyingi za kuweza kutumia utafiti, ubunifu na ujasiriamali hususan kupitia sekta ya elimu ili kuongeza kasi ya maendeleo ya viwanda nchini. Kwa kufanya hivyo, kutawezesha kutekeleza azma ya Serikali ya awamu ya tano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Dira ya Taifa ya 2015, ya kuhakikisha kuwa Tanzania inafikia hadhi ya kuwa na uchumi wa kati na unaoendeshwa na sekta ya viwanda," amesisitiza Waziri Ndalichako.

Aidha, Waziri amesema wizara imeandaa mwongozo wa kutamba na kuendeleza ugunduzi, ubunifu na maarifa hasilia nchini ili kujenga na kukuza hamasa ya matmizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu katika shughuli za jamii na maendeleo na hivyo kuongeza mchango wake katika uchumi wa nchi.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiangalia baadhi ya maandiko ya tafiti mbalimbali zinazoonyeshwa katika maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakati wa kufunga Wiki hiyo jijini Dar es Salaam
Akizungumza katika sherehe hizo Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Prof. William Anangisye amesema chuo hicho kitaendelea kusimamia  ufanyaji wa tafiti kwani ndo kigezo kimojawapo kinatmika katika kupima ubora wa vyuo Duniani.

“Katika kuhakikisha chuo hiki kinarudi katika falsafa yake, tumetenga kiasi cha shilingi bilioni moja katika bajeti ya mwaka 2019/20 ili kuwawezesha wahadhiri na wataalam kufanya tafiti,” amesema Makamu Mkuu wa Chuo.


Baadhi ya washiriki wa maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakifatilia kwa makini hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako (Hayupo Pichami) wakati wa kufunga maadhimisho hayo.

Jumatatu, 6 Mei 2019

WATANZANIA WATAKIWA KUTHAMINI ELIMU INAYOTOLEWA NCHINI

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu amesema Elimu inayotolewa nchini ina ubora unaokubalika ambapo amewataka wale wanaoibeza na kuidhalilisha kuacha kufanya hivyo.

Dkt. Semakafu ametoa kauli hiyo Jijini Dodoma wakati wa hafla ya kutunuku vyeti kwa wanafunzi washindi wa kitaifa ambao wameshiriki uandishi wa shindano la Insha za Jumuiya ya Maendeleo nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

“Yapo mengi yanasemwa kuhusu Elimu yetu, tuache kujidhalilisha maana wanafunzi wetu ambao wanawakilisha nchi nje ya Tanzania katika masuala ya kielimu wamekuwa wakifanya vizuri,” alisema Dkt. Semakafu.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. AveMari Sekafu akizungumza wakati wa hafla ya kutunuku vyeti kwa washindi wa Kitaifa wa shindano la uandishi wa Insha za Jumuiya ya Maendeleo nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC). Amewataka walimu kuwasaidia wanafunzi  kufuata taratibu wakati wa uandishi wa insha.

Kiongozi huyo amesema mashindano hayo ni sehemu ya mkakati mkubwa wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika katika kujenga uelewa kwa wanafunzi juu ya kazi na mipango ya Jumuiya hizo.

Aliongeza kuwa uandishi wa insha unawapa wanafunzi hamasa ya kutafiti na kupata taarifa zaidi, kuelewa na kuwawezesha kujadili masuala mbalimbali kwa kina.

Kwa upande wake Mratibu wa mashindano hayo ambaye ni Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Ithibati ya shule Sylivia Chingwile ametoa wito kwa walimu na wazazi kuwahimiza wanafunzi kushiriki mashindano hayo ya insha na mengine yanayojitokeza, kwani uzoefu unaonesha wanafunzi wanaoshiriki katika mashindano hayo wamekuwa wakifanya vizuri katika mitihani yao ya mwisho.

Mshindi wa kwanza kikanda wa shindano la uandishi wa  Insha za Jumuiya ya Afrika Mashariki Innocent Shirima ambae ni mlemavu wa macho kutoka shule ya Sekondari  Moshi iliyoko Mkoa wa Kilimanjaro akipokea zawadi  na cheti wakati wa hafla ya kutunuku washindi  wa shindano la insha, hafla hiyo hao imefanyika jijini Dodoma.

Naye Mwanafunzi mshindi wa insha za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kikanda kwa mwaka 2018 Innocent Shirima kutoka shule ya Sekondari ya Moshi, iliyopo mkoani Kilimanjaro ameshauri mashindano ya insha ya Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) ziwe zinatoa fursa kwa wanafunzi kuchagua aina ya lugha wanayoweza kuitumia wakati wa kuandika insha hizo.

“Ili tuendelee kufanya vizuri katika masuala mbalimbali ya kijamii, nashauri kama ilivyo kwenye mashindano ya Insha za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wanatoa machaguzi ya lugha kama vile Kifaransa, Kiingereza au Kiswahili, hivyo hivyo ningeomba ifanyike kwa mashindano mengine kwa lengo la kutangaza lugha zetu hususan Kiswahili, ili siku moja tuje kuona Sudan Kusini wanaandika insha kwa lugha ya Kiswahili,” alisisitiza mwanafunzi Innocent Shirima.

Kwa maelezo zaidi kuhusu  taarifa za  mashindano hayo ya uandishi wa insha na namna ya kushiriki tembelea tovuti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (www.moe.go.tz).

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Sekafu akiwa katika picha ya pamoja na washindi wa Kitaifa wa shindano la uandishi wa Insha za Jumuiya ya Maendeleo nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).