Jumatano, 22 Mei 2019

SERIKALI KUENDELEA NA MIKAKATI YA KUMLINDA MTOTO WA KIKE ILI AWEZE KUMALIZA ELIMUMSINGI



Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha amesema serikali inaendelea na mikakati ya kumlinda mtoto wa kike ili aweze kupata elimumsingi bila kukatiza.

Naibu Waziri ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam alipokutana na Waziri wa Maendeleo na Mahusiano ya Kimataifa kutoka Sweden, Peter Erickson ambapo amesema mikakati  hiyo inamuwezesha mtoto wa kike kusoma katika mazingira  salama.

"Mikakati tunayoendelea nayo ya kuwawezesha watoto wa kike wasikatishe masomo yao ni kutoa ushauri nasaha na kuwawezesha kutambua kuwa elimu ni muhimu kwao na wazazi wao ili kuwaepusha na vikwazo vyovyote ambavyo vinaweza kusababisha kukatisha masomo yao,"  amesisitiza Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha akisalimiana na Waziri wa Maendeleo na Mahusiano ya Kimataifa kutoka Sweden, Peter Erickson aliyefika na ujumbe wake katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.
Ole Nasha amesema serikali ina mifumo mizuri ambayo imekuwa ikitumika kwa miaka mingi katika kumsaidia mtoto wa kike aliyepata ujauzito kuweza kuendelea na masomo yake katika kupata ujuzi na utaalamu utakaomsaidia kujiletea maendeleo yake.

"Mtoto wa kike anapopata mimba akiwa shuleni ametengenezewa mifumo mingine itakayomuwezesha kupata ujuzi na utaalamu huku akiendelea kulea mtoto wake, mifumo hiyo ni pamoja na elimu ya ufundi na elimu ya watu wazima," ameelezea Ole Nasha.

Akizungumzia mahusiano yaliyopo kati ya Tanzania na Sweden Naibu Waziri amesema  ni ya  miaka mingi inayokaribia 50 ambapo katika miaka yote hiyo nchi ya Sweden imeweka alama  katika kufadhili miradi na programu mbalimbali za elimu.

Ole Nasha ameitaja baadhi ya miradi hiyo kuwa ni pamoja na mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo (P4R) ambao umewezesha kujengwa na kukarabati miundombinu mbalimbali ya shule na Mradi wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (LANES) ambao umesaidia  katika  kuinua ubora wa elimu nchini.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha akizungumza na Waziri wa Maendeleo na Mahusiano ya Kimataifa kutoka Sweden, Peter Erickson aliyefika na ujumbe wake katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri ameongeza kuwa mbali na miradi hiyo pia Sweden imesaidia kujenga uwezo katika maeneo ya utafiti katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS) ambapo jumla ya wahadhiri 63 wanaosoma Shahada ya Umahiri na 43 wanaosoma Shahada ya Uzamili wamefadhiliwa na Sweden.

Akizungmza katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo amesema mradi wa LANES unaofadhiliwa kwa kiwango kikubwa na Sweden umesaidia katika kuwajengea uwezo walimu wa madarasa ya chini kwa kuwapa mbinu za kufundisha madarasa yenye watoto wengi na kuandaa vifaa ya kufundishia na kujifunzia kwa wanafunzi wa madarasa ya chini.

Naye Waziri wa Maendeleo na Mahusiano ya Kimataifa kutoka Sweden, Peter Erickson amesema Sweden imekuwa na mahusiano mazuri na Tanzania kwa muda mrefu ambapo imekuwa ikifadhili miradi mbalimbali ya Elimu yenye kulenga kuinua ubora wa Elimu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wiliam Ole Nasha, Katibu Mkuu Dkt. Leonard Akwilapo, Naibu Katibu Mkuu Ave Maria Semakafu wakiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Maendeleo na Mahusiano ya Kimataifa kutoka Sweden, Peter Erickson pamoja na ujumbe alioongozana nao katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.
Aidha, waziri huyo amesema ameridhishwa na jinsi serikali inavyoendelea kuboresha elimu na kuahidi kuendelea na programu za kuisaidia serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu imetekeleza vizuri miradi mbalimbali inayofadhiliwa na nchi yake.

"Nimeongea na Viongozi wa elimu ambao wameelezea vizuri jinsi mtoto wa kike anavyowezeshwa katika kupata ujuzi na utaalamu baada ya kupata mimba, hivyo wafadhili mbalimbali kupitia GPE wamekubali kutoa kiasi cha dola za kimarekani milioni 90 kuboresha Elimu ya msingi," amesema Peter Erickson.

NDALICHAKO AVUTIWA NA WANAFUNZI WA SHULE YA DAR ES SALAAM INTERNATIONAL ACADEMY KWA UWEZO WA KUJIAMINI

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako ameupongeza Uongozi wa shule ya Dar es Salaam International Academy kwa kuwajengea uwezo na kuona umuhimu wa kuwafundisha na kuwapa nafasi wanafunzi kujifunza wenyewe.


Prof. Ndalichako ametoa pongezi hizo jijini Dar es Salaam aliposhiriki katika maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano katika shule hiyo ambapo amesema wanafunzi hao wamefundishwa kutafuta taarifa mbalimbali kutokana na mada walizopewa.

“Nimefurahi kuona wanafunzi wa darasa la tano wanaonesha ubunifu katika kuangalia matatizo ya jamii kwani hata mada walizoangalia zinaendana na hali halisi ya sasa ambayo serikali imekuwa ikiwekea msisitizo kama masuala ya jinsia, magonjwa ya homa ya ini na Ebola, dawa za kulevya pamoja na Teknolojia,” amesema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wanafunzi, walimu na wazazi (Hawapo Pichani) wa shule ya Dar es Salaam International Academy wakati wa maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano.
Waziri Ndalichako amesema katika kutafuta taarifa wanafunzi hao wameonyesha vipaji vya hali ya juu wakati wa kuandaa mada za maonyesho kwani wametumia mitandao pamoja na kuwahoji watu waliowaona muhimu kuwapatia taarifa zilizowawezesha kukamilisha mada zao kwa ajili ya maonyesho hayo.  

Aidha, Waziri Ndalichako ametoa wito kwa walimu kuwawezesha na kuwapa nafasi wanafunzi katika kuwa na ubunifu, kujiamini na kuweza kutafuta taarifa mbalimbali katika kujifunza kwani wanafunzi wa kitanzania wana uwezo wa kufanya mambo makubwa sana lakini wanakwama kutokana na kushindwa kujiamini na uoga wakati shuleni ni sehemu ambayo vipaji hivyo vinaweza kuendelezwa.

“Suala la kujiamini ni changamoto kubwa kwa watanzania wengi, wana uwezo, akili na vipaji lakini wanakuwa hawajiamini hili ni tatizo,  kwa hiyo tuendelee kuwa na maonyesho kama haya ambayo yatawajengea wanafunzi wetu uwezo, kujiamini, kuonyesha yale wanayoweza na kutoogopa kusema mbele za watu,” amesisitiza  Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na kusalimiana na walimu wa shule ya Dar es Salaam International Academy wakati wa maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano.
Aidha, Waziri Ndalichako amesema hata katika shule za serikali maonyesho kama hayo yanafanyika  katika ngazi ya shule za sekondari ambayo yanaanza katika ngazi ya shule, wilaya na kilele inakuwa katika ngazi ya Kitaifa hata hivyo wameahidi kuangalia namna ya kuanza kushirikisha wanafunzi wa shule za msingi kwani kufanya hivyo inawezesha kuwaandaa wabunifu tangu wakiwa katika umri mdogo.

Akizungmzia mkakati wa serikali wa kutambua na kukuza ubunifu nchini Waziri Ndalichako amesema kupitia Tume ya Sayansi na Teknolojia inazo atamizi ambazo zinatumika kuendeleza ubunifu lakini pia imeona si rahisi kila mtu kuweza kufika katika Tume hiyo hivyo imeanza utaratibu wa kuanzisha katika ngazi za Halmashauri ambapo mwaka huu mwongozo umetoka wa kuangalia namna gani wabunifu wakitambulika wanaweza kuendelezwa.

“Pia katika vyuo vikuu vyetu kuna hatamizi kwa mfano Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Nelson Mandela kuna atamizi ambazo zinafanya vizuri sana na wao wamejikita katika mazao na kuangalia vitu ambavyo vinaweza kuweka sumu katika mazao lengo ni kuhakikisha tunaongeza wigo ili vipaji wa watanzania viweze kuendelezwa,” amesema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiangalia kipeperushi kilichotengenezwa na wanafunzi Dar es Salaam International Academy wakati wa maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano.
Naye Mkuu wa Shule hiyo, Fawzya Hirji amesema shule hiyo imejipanga kuhakikisha kunakuwa na ushirikiano  kati ya walimu, wanafunzi na wazazi katika kuwawezesha wanafunzi hao kuwa na uwezo wa ubunifu, kujiamini na kutumia mitandao katika kutafuta taarifa mbalimbali zinazowapatia maarifa ya kujua mambo mbalimbali duniani.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akisikiliza maelezo kutoka kwa wanafunzi wa shule ya Dar es Salaam International Academy wakati wa maonesho mbalimbali ya wanafunzi wa darasa la tano.

Jumatano, 8 Mei 2019

WAZIRI NDALICHAKO AIPONGEZA UDSM KWA KUTENGA BILIONI MOJA ZA KUENDELEZA UTAFITI


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako ameupongeza uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kutenga kiasi cha shilingi bilioni moja katika bajeti yake ya mwaka 2019/20 kwa ajili ya kutoa fursa kwa  wahadhiri na wanafunzi kendeleza tafiti

Waziri Ndalichako ametoa pongezi hizo jijini Dar es Salaam wakati akifunga maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambapo amesema utafiti una mchango katika ukuaji wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akihutubia washiriki wa maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakati wa kufunga Wiki hiyo jijini Dar es Salaam

Prof. Ndalichako amesema serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda lengo likiwa kuhakikisha kunakuwa na viwanda ambavyo vinatumika kuzalisha bidhaa na kutoa huduma zitakazotosheleza jamii ya Kitanzania na kusaidia kuongeza ajira kwa vijana.

“Serikali kupitia Tume ya Sayansi na Teknolojia ilizipatia Taasisi nane za Tanzania Bara kiasi cha shilingi bilioni tatu na milioni mia mbili wakati upande wa Zanzibari shilingi milioni 960 zilitolewa kwa ajili ya utafiti, Taasisi hizo zilishinda uandishi wa tungo za miradi ya uboreshaji wa miundombinu ambayo ina uwezo wa kutoa mchango madhubuti katika Dira ya nchi yetu ya uendeshaji wa viwanda kwa lengo la kuimarisha uchumi wa nchi yetu” amesisitiza Waziri Ndalichako.

Akizungumzia Wiki ya Utafiti Waziri Ndalichako amesema inawapa wadau wa utafiti na ubunifu jukwaa la kufahamu aina za shughuli za utafiti zinazofanyika; sehemu gani kuna mapengo na changamoto; na mikakati gani ya kimipango inahitajika ili kuziba mapengo pamoja na kutatua changamoto zilizobainika.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akikabidhi tunzo kwa washindi wa auandishi wa miradi ya tafiti wakati wa kufunga  maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. 

"Kama taifa, tuna wajibu mkubwa na fursa nyingi za kuweza kutumia utafiti, ubunifu na ujasiriamali hususan kupitia sekta ya elimu ili kuongeza kasi ya maendeleo ya viwanda nchini. Kwa kufanya hivyo, kutawezesha kutekeleza azma ya Serikali ya awamu ya tano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Dira ya Taifa ya 2015, ya kuhakikisha kuwa Tanzania inafikia hadhi ya kuwa na uchumi wa kati na unaoendeshwa na sekta ya viwanda," amesisitiza Waziri Ndalichako.

Aidha, Waziri amesema wizara imeandaa mwongozo wa kutamba na kuendeleza ugunduzi, ubunifu na maarifa hasilia nchini ili kujenga na kukuza hamasa ya matmizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu katika shughuli za jamii na maendeleo na hivyo kuongeza mchango wake katika uchumi wa nchi.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akiangalia baadhi ya maandiko ya tafiti mbalimbali zinazoonyeshwa katika maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakati wa kufunga Wiki hiyo jijini Dar es Salaam
Akizungumza katika sherehe hizo Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Prof. William Anangisye amesema chuo hicho kitaendelea kusimamia  ufanyaji wa tafiti kwani ndo kigezo kimojawapo kinatmika katika kupima ubora wa vyuo Duniani.

“Katika kuhakikisha chuo hiki kinarudi katika falsafa yake, tumetenga kiasi cha shilingi bilioni moja katika bajeti ya mwaka 2019/20 ili kuwawezesha wahadhiri na wataalam kufanya tafiti,” amesema Makamu Mkuu wa Chuo.


Baadhi ya washiriki wa maadhimisho ya tano ya Wiki ya Utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakifatilia kwa makini hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako (Hayupo Pichami) wakati wa kufunga maadhimisho hayo.