Jumamosi, 21 Desemba 2019

BILIONI 37 KUJENGA TAASISI YA TEKNOLOJIA DAR ES SALAAM (DIT) KAMPASI YA MWANZA

Serikali imezindua mradi wa ujenzi wa majengo mapya yenye thamani ya Sh. Bilioni 37 katika Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kampasi ya Mwanza kupitia ufadhili wa Benki ya Dunia (World Bank).

Uzinduzi huo umefanywa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha alipomuwakilisha Waziri wa wizara hiyo kwenye mahafali ya kwanza ya Taasisi hiyo katika kampasi ya Mwanza ambapo amesema ujenzi huo utaanza karibuni na unatarajiwa kukamilika Desemba 2024.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akihutubia hadhira iliyoshiriki katika mahafali ya  kwanza ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kampasi ya Mwanza.
Ole Nasha ameongeza kuwa mradi huo utaongeza udahili kwa zaidi ya asilimia 50 katika fani mbalimbali za ufundi na teknolojia na utawezesha kuhuisha mitaala katika fani ya ngozi ili kuzalisha mafundi mahiri watakaoweza kujiajiri na kuajiriwa.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akipewa maelezo ya mchoro unaoonesha majengo yatakavyokuwa baada ya kukamilika kwa Mradi wa Ujenzi mwaka 2024. Anayetoa maelezo hayo ni Mkurugenzi wa DIT kampasi ya Mwanza, Dkt. Albert Mmari.
Waziri Ole Nasha pia ametoa rai kwa wanafunzi waliopata mikopo kutumia fursa hiyo kusoma kwa bidii na kujiepusha na vurugu  kwani zinaweza kuwaletea matatizo ikiwemo kuchukuliwa hatua na kukosa fursa za mikopo.

"Wanafunzi waliopata mikopo wajione kuwa wana bahati sababu kati ya wanafunzi zaidi ya elfu 70 wa mwaka wa kwanza walioomba ni 49,485 ndio waliopata, kwahiyo mnapopata fursa ya mkopo muitumie vizuri kwa kusoma na kujiongezea elimu kwa ajili ya maisha yenu ya baadaye na taifa kwa ujumla," amesisitiza Ole Nasha.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Mradi wa ujenzi wa majengo mapya katika Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kampasi ya Mwanza.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la DIT, Prof. Apollinaria Pereka akisoma historia ya DIT kampasi ya Mwanza amesema taasisi hiyo ilikidhi vigezo vya usajili wa kudumu kutoka Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) mwaka 2016 na kupewa kibali cha kuanzisha kozi ya teknolojia ya ngozi na sayansi na teknolojia ya maabara katika ngazi ya Stashahada.

Amesema anaamini DIT kampasi ya Mwanza itatekeleza azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuhakikisha inatoa wataalamu ambao wataifikisha nchi katika uchumi wa kati kupitia viwanda ifikapo mwaka 2025.

Katika mahafali hayo jumla ya wahitimu 11 wametunukiwa Stashahada ya sayansi na teknolojia ya maabara, wakiwemo wasichana wanne na wavulana saba.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akimtunuku cheti mmoja wa wahitimu wa Stashahada ya sayansi na teknolojia ya maabara katika mahafali ya kwanza ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kampasi ya Mwanza.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akiwa katika picha ya pamoja na wahitimu wa Stashahada ya sayansi na teknolojia ya maabara waliotunukiwa vyeti katika mahafali ya kwanza ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kampasi ya Mwanza.

Alhamisi, 12 Desemba 2019

OLE NASHA: WAKUU WA SHULE HIMIZENI WANAFUNZI WASHIRIKI MASHINDANO YA UANDISHI WA INSHA

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amewataka Wakuu wa Shule zote za sekondari nchini kuwahimiza wanafunzi wao kushiriki katika mashindano ya uandishi wa insha za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Ole Nasha amesema mashindano hayo ni sehemu ya mkakati wa kujenga uelewa kwa wanafunzi juu ya kazi na mipango ya maendeleo ya Jumuiya hizo.

Ole Nasha ameyasema hayo leo jijini Dodoma katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC kwa mwaka 2019 na kuongeza kuwa mashindano haya yana faida kubwa zaidi ya kupata zawadi kwani washindi wanaweza kuyatumia kujiongezea wasifu wao siku za mbeleni na hivyo kuwaongezea sifa za kupata ajira.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akiongea na washiriki (hawapo pichani) waliohudhuria hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC, 2019 iliyofanyika jijini Dodoma.
"Niwaambie wanafunzi, kushinda sio suala la kupata zawadi tu bali kunakujengea wasifu ambao huko mbeleni utakusaidia unapoomba ajira unakuwa na wasifu wa ziada utakaokufanya upate ajira kirahisi," alisisitiza Ole Nasha.

Katika hatua nyingine Waziri Ole Nasha ameonesha  kushangazwa na wanaobeza kiwango cha elimu itolewayo nchini ambapo amesema ushindi unaopatikana kutoka kwa wanafunzi wa kitanzania unaonesha dhahiri kuwa elimu ya Tanzania ni bora.
Baadhi ya wanafunzi, walimu na wazazi walioshiriki katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC mwaka 2019 wakisikiliza hotuba ya mgeni rasmi ambaye ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani).
Mwanafunzi Ruvina D. Warimba kutoka shule ya sekondari Morogoro, ambaye pia ndio mshindi wa tatu wa shindano la uandishi wa insha za SADC Kanda akitunukiwa cheti na Mwakilishi toka SADC, Agnes Kayola. Katikati ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha na kulia ni Kaimu Kamishna wa Elimu, Augusta Lupokela.
Mratibu wa mashindano ya Uandishi wa Insha, Sylvia Chinguwile akiongea katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC mwaka 2019.
"Kuna maneno huko nje kuwa elimu yetu haina kiwango, kama ni kweli inawezekanaje mwanafunzi wetu anaibuka mshindi wa tatu katika mashindano yanayoshirikisha nchi zaidi ya 15," amehoji Ole Nasha.

Awali, akisoma risala katika hafla hiyo, Mratibu wa mashindano hayo, Sylvia Chinguwile amesema mashindano hayo yamekuwa chachu kwa vijana kufanya utafiti, kujifunza na kufahamu vizuri mchakato wa uimarishaji mahusiano kwa nchi wanachama wa SADC na EAC .

Akielezea zaidi kuhusu mashindano hayo, Chinguwile amesema mchakato wake huanza baada ya kikao cha wakuu wa nchi wanachama ambao hukubaliana mada zitakazoshindaniwa. Baada ya hapo kila nchi hutakiwa kutangaza na kubainisha vigezo vya ushiriki na kwamba insha za wanafunzi huwasilishwa wizarani baada ya kuteuliwa insha bora katika ngazi ya shule na kusahihishwa na jopo la wataalamu.

Chinguwile amewataja washindi wa mashindano hayo na shule wanazotoka kuwa ni Vanessa Lema (Longido), Thomas Kalisti (Kibasila), Monica Nyamhanga (Heritage), Dennis Mmuni (St. Maximillian), Hance Mwang'onda (Mbagala), Julieth Mpuya (Kilangalanga), Grant Mkonyi (Tanga Tech), Mandela Abel (Kibaha), Rebecca Thadayo (Loyola), Sharifa Hamadi (Benbella), Cynthia Masuka (Longido) na Ruvina Warimba (Morogoro) ambaye alishika nafasi ya tatu katika shindano la kanda la SADC.
Hafla hiyo pia imehudhuriwa na mwakilishi kutoka EAC, Dkt. James Jowi, mwakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Eliab Chodota na Mwakilishi kutoka SADC, Agnes Kayola ambao wamewapongeza wanafunzi hao kwa ushindi na kuwataka wanafunzi wengine nchini kushiriki mashindano hayo.

Washindi hao kutoka shule mbalimbali za serikali na binafsi wamezawadiwa fedha taslimu za kitanzania na dola za kimarekani pamoja na kutunukiwa vyeti. Fedha hizo zimetolewa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambapo wametoa kiasi cha Sh. 300,000 kwa washindi wote huku SADC na EAC wakitoa kati ya dola 500 hadi 50 kulingana na kiwango cha ushindi.
Kaimu Kamishna wa Elimu, Augusta Lupokela akiongea katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa Insha za SADC na EAC 2019 iliyofanyika jijini Dodoma.
Mwakilishi kutoka EAC, Dkt. James Otieno Jowi akiongea na washiriki katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa uandishi wa insha za SADC na EAC, 2019 iliyofanyika jijini Dodoma.

Mwanafunzi Dennis Mmuni akikabidhiwa cheti na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha katika  hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC, 2019 iliyofanyika jijini Dodoma.

Ijumaa, 29 Novemba 2019

NDALICHAKO AZINDUA CHUO CHA VETA NDOLAGE WILAYANI MULEBA - 380 KUDAHILIWA JANUARI 2020

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amezindua chuo kipya cha VETA Ndolage kilichopo Kamachumu Wilaya ya Muleba mkoani Kagera kilichojengwa kwa gharama ya shilingi milioni 281.

Ujenzi wa Chuo hicho ni utekelezaji wa azma ya Serikali ya kushirikiana na jamii kufikisha Elimu ya Ufundi karibu na Wananchi pamoja na kujenga Vyuo vya VETA katika kila Wilaya nchini ifikapo mwaka 2020, ambapo Wizara imetenga zaidi ya Sh. bilioni 40 katika mwaka huu wa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Vyuo vya VETA katika Wilaya 25 nchini.

Ujenzi wa Chuo cha Ndolage ulianzishwa na Wananchi kwa kushirikiana na Mbunge wa Jimbo la Muleba  Kaskazini, Charles Mwijage ambapo wananchi walitoa kiwanja na kuanza ujenzi wa madarasa kwa kutumia michango yao.

Akizungumza katika hafla hiyo Profesa Ndalichako amewataka VETA  kuhakikisha wanajenga majengo yote yanayohitajika  katika Chuo hicho kwa kutumia mapato ya ndani ya VETA.

"Nimezindua Chuo hiki lakini sijaridhishwa na majengo, ni machache na hayana hadhi kwani Wizara imetoa hela kulingana na mahitaji  yenu, inakuwaje bado kuna changamoto za majengo? Natoa miezi sita mkamilishe kwa fedha zenu," alisisitiza Ndalichako.

Wakati huo huo Ndalichako amewashukuru Wananchi wa Ndolage na Mbunge wa Jimbo hilo  kwa  hatua ya kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha watoto na Vijana katika eneo hilo wanapata Elimu kwa kujitolea ardhi bure kwa ajili ya ujenzi huo na kuchangia fedha za vifaa.

Aidha, Mkuu wa Mkoa Kagera, Brigedia Jenerali Marco Gaguti, ameishukuru Wizara ya Elimu kwa ujenzi wa Chuo hicho na ameahidi kuhamasisha Wananchi kuandikisha Vijana wao kujiunga na Chuo hicho.

Akitoa salamu za VETA, Mwenyekiti wa Bodi ya VETA, Peter Maduki amesema Chuo hicho kitadahili wanafunzi 80 wa kozi za muda mrefu na wanafunzi 300 wa kozi fupifupi ambao wanatarajiwa kuanza mafunzo Januari mwaka 2020.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mbunge wa Jimbo hilo la Muleba kaskazini, Charles Mwijage ameishukuru Serikali kwa kujenga Chuo  hicho huku akiushauri uongozi wa VETA kuongeza mafunzo ya fani ya usindikaji mazao  kwani wananchi wa eneo hilo wamejikita katika kilimo.

Mafunzo mengine yatakayotolewa katika Chuo hicho ni ya fani za  Uashi, Ushonaji, Uhazili, Urembo na Uungaji wa Vyuma.