Jumatano, 2 Septemba 2020

DR. LEONARD AKWILAPO ATAKA TAASISI ZA ELIMU YA JUU KUANZISHA PROGRAMU ZA VIPAUMBELE VYA TAIFA

 Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo ametoa wito kwa Vyuo Vikuu nchini kuhakikisha vinaanzisha programu za masomo zinazoendana na vipaumbele vya kitaifa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akifungua  maonesho  ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam

Dkt. Akwilapo ametoa wito huo Jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa maonesho ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia ambapo amesema kwa kuanzisha programu hizo nchi itaongeza ujuzi wa wataalamu na pato la taifa. 

Kiongozi huyo ametaja baadhi ya programu za kipaumbele kuwa ni mafuta na gesi, afya, hususani udaktari bingwa kwa ngazi za Uzamivu katika nyanja zote za magonjwa ya upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu, upandikizaji figo, ini na uboho (bone marrow), tiba za ndani za moyo, na uhudumiaji wa wagonjwa wa dharura na mahututi (emergency medicine and critical care).


 “Tusingependa kama nchi kupeleka wagonjwa wetu nchi za nje kutibiwa, bali nchi za nje waje kutafuta tiba kwetu (medical tourism). Kwa kufanya hivyo tutaongeza ujuzi wa wataalamu wetu pamoja na pato la taifa,” amesisitiza Dkt. Akwilapo. 

Katibu Mkuu Akwilapo ameongeza kuwa pamoja na kuanzisha programu za vipaumbele, nchi kwa sasa inatekeleza miradi mingi mikubwa ambayo inahitaji wasomi wa kuendesha na kusimamia miradi hiyo, hivyo ni jukumu la Taasisi za Elimu ya Juu kuhakikisha hili linafanyika kwa ufanisi wa hali ya juu kwa kuhakikisha wanatoa elimu bora na kwamba Serikali itaendelea kusomesha kwa wingi wataalamu katika fani na ujuzi adimu na maalum kwa mahitaji ya nchi. 

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na wakuu wa vyuo mbalimbali vya elimu ya Juu nchini mara baada ya kufungua maonesho  ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam

“Ni jambo la kutia moyo kuona kwamba hivi sasa baadhi ya vyuo vikuu vimeanza kuelekeza jitihada zao katika kutoa elimu ambayo inalenga kushughulikia changamoto za jamii na kuweka msisitizo katika maeneo ya kimkakati ya nchi kama vile Kilimo, Madini, Utalii, Uvuvi, Maliasili na Misitu na Afya,” amesema Dkt. Akwilapo.  

Katika hatua nyingine Dkt. Akwilapo ameendelea kuzitaka Taasisi za Elimu ya Juu kuona namna bora ya kupanua udahili wa wanafunzi wa elimu ya juu kutokana na ongezeko la udahili wa wanafunzi katika ngazi ya msingi na sekondari na kwamba wanapohitimu lazima wapate nafasi katika vyuo vya kati na vya juu ili kuweza kuwapa ujuzi wa kujiajiri na hivyo kuchangia kikamilifu katika ujenzi wa Taifa. 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Tume ya Vyuo Vikuu nchini, Profesa Mayunga Nkunya  amesema Tume pamoja na mambo mengine imefanikiwa kuimarisha mfumo wa utoaji ithibati ya mtaala, jambo ambalo lilionekana kuwa tatizo kwa muda mrefu na kwamba itaendelea kutekeleza majukumu yake ya kuwatumikia Watanzania katika sekta ya elimu ili kuhakikisha Watanzania wa ngazi zote wanapata elimu bora yenye kukidhi viwango vya ubora Kitaifa, Kikanda na Kimataifa.

Naye Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini, Profesa Charles Kihampa amesema lengo la maonesho hayo ni kutoa fursa kwa vyuo vikuu kujitangaza na kuonesha huduma na kazi wanazofanya pamoja na mchango wao katika ustawi wa elimu ya juu kwa mustakabali wa maendeleo ya sayansi, teknolojia na manuufaa yake kiuchumi na kijamii. 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi waliotembelea maonesho hayo wamesema wamefurahishwa na kuwepo kwa maonesho hayo kwani yanatoa fursa ya kuonana na wahusika na kupata taarifa zinazowawezesha kuomba programu zinazoendana na ufaulu wao.

Jumla ya taasisi 67 za elimu ya juu zimeshiriki katika maonesho hayo.

Brass Band ikitumbuiza wakati wa ufunguzi wa maonesho ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika Jijini Dar es Salaam

Jumanne, 1 Septemba 2020

WALIMU 100 NCHINI KUFUNDISHWA MBINU ZA KUFUNDISHIA LUGHA YA KIFARANSA

Serikali za Tanzania na Ufaransa zimeingia makubaliano ya kutoa mafunzo ya mbinu za kufundishia lugha ya Kifaransa kwa walimu 100 nchini ambao watakuwa na uwezo wa kufundisha wanafunzi 5,000 wa Kitanzania katika ngazi ya sekondari.

Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao kati ya Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Frederic Clavier na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo kilichofanyika Jijini Dar es Salaam ambapo jumla ya Dola za Kimarekani 250,000 zitatumika ili kufanikisha mpango huo.
Katika kikao hicho wamekubaliana kufanyika kwa vikao vya kitaalamu kati ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Kituo cha Ubalozi wa Ufaransa (Alliance Francais) ili kupanga utekelezaji wa mafunzo hayo ya walimu.

Aidha, Balozi Clavier ameonesha kuwepo kwa fursa za Watanzania kusoma programu zisizopungua 2,000 za Kiingereza nchini Ufaransa. Ameeleza kuwa  Ufaransa inaandaa Maonesho ya Elimu ya Juu (Higher Education Fair) yatakayofanyika nchini Mei 2021 ambapo vyuo 20 vya Ufaransa vitashiriki kutafuta ushirikiano na Vyuo Vikuu vya Tanzania na Sekta binafsi. 
Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu Akwilapo ameushukuru Ubalozi wa Ufaransa kwa kuendeleza ushirikiano katika kukuza na kuimarisha elimu ya Juu nchini kupitia ufadhili wa mafunzo hayo na kuagiza wahusika katika Wizara anayoisimamia kuhakikisha vikao vya kitaaluma vinafanyika ili mafunzo hayo yaweze kuanza kwa wakati uliopangwa.

Katibu Mkuu Akwilapo pia ameahidi kuweka wazi kwa Watanzania kuhusu kuwepo kwa fursa hiyo ya kusoma programu za Kiingereza nchini Ufaransa ili Watanzania waweze kuchangamkia fursa hiyo.

SEMAKAFU: VYUO VYA FDC TOENI MAFUNZO YENYE UHITAJI NA AJIRA

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu amevitaka Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDCs) kujikita katika kutoa mafunzo ya fani zinazopendwa na zinazotoa ajira badala ya kuendelea kuwa na fani ambazo hazina wanafunzi katika eneo husika.


Dkt. Semakafu ametoa agizo hilo alipofanya ziara ya kukagua ukarabati na uendeshaji wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same kilichopo Mkoani Kilimanjaro ambapo amesema ni vizuri vyuo  vikajiimarisha kwenye utoaji mafunzo kwa fani zenye wanafunzi  wengi na kuachana na zile zenye wanafunzi wachache.
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akizungumza na baadhi ya watumishi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same baada ya kukagua ujenzi na ukarabati wa miundombinu chuoni hapo.

“Kuanzia mwaka huu, kila chuo cha wananchi kitafundisha fani ambazo zinahitajika katika maeneo husika kwa maana ya kuwa na wanafunzi wa kutosha, hakuna chuo chochote kusajili fani ambazo zina wanafunzi wachache ama chini ya kumi na mbili, Serikali haiajiri walimu kufundisha wanafunzi wawili hivyo hakuna haja ya kuweka fani ambazo hazina wanafunzi wa kutosha,” amesisitiza Dkt. Semakafu.

Aidha, Naibu Katibu Mkuu huyo amesema mpango wa 'Elimu haina mwisho' unaotolewa katika vyuo hivyo ni utaratibu wa kutoa fursa kwa watoto waliokatisha masomo kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za kiuchumi na kijamii ili kuwasaidia kupata elimu na ujuzi wa kuwawezesha kuendelea na masomo na kuendesha maisha yao pindi watakapohitimu hivyo wanapaswa kufundishwa kama wanafunzi wengine bila kuwatenga.  
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akitoa maelekezo ya namna ya kuboresha eneo la utoaji wa mafunzo ya umeme wa magari kwa Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi, Edward Mdee.

Amesema Serikali iliamua watoto hao wasome katika vyuo hivyo kupitia mfumo usio rasmi bila malipo yoyote kwa lengo la kuhakikisha wanapata fursa nyingine ya kuendelea na masomo na kuutaka Uongozi wa chuo cha Maendeleo Same  kuwarudisha chuoni wanafunzi wote walioacha masomo kwa sababu mbalimbali ili waweze kumaliza masomo yao.

“Tumeanza programu hii kwa lengo la kupata watoto wote walioacha shule na ndio maana unaona hata wasichana walioacha shule kutokana na changamoto mbalimbali tumewarudisha katika mfumo huu ili waje waendelee na masomo na na wale wenye watoto hata tuna shule za chekechea kwa ajili ya watoto wao,” amesema Dkt. Semakafu.

Naibu Katibu Mkuu Dkt. Semakafu amekagua miundombinu iliyokarabatiwa na kuboreshwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambapo ameuagiza uongozi wa chuo hicho kufanya marekebisho katika baadhi ya miundombinu ambayo haikukarabatiwa vizuri.
Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Same, Edward Mdee akitoa taarifa  ya chuo hicho kwa Naibu Katibu Mkuu, Dkt. Ave Maria Semakafu alipofika chuoni hapo kukagua maendeleo ya chuo hicho.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same, Edward Mdee  ameishukuru Wizara kwa ukarabati ambao umefanyika chuoni hapo, na kusema kuwa chuo hicho chenye wanafunzi 301 kipo katika mkakati wa kuboresha utoaji wa mafunzo ili kuhakikisha kinatoa vijana wenye ujuzi na maarifa yatakayowawezesha vijana wa Same kujiajiri ama kuajiriwa.
Muonekano wa baadhi ya majengo ya miundombinu ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same yaliyojengwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Alhamisi, 2 Julai 2020

NDALICHAKO ATIMIZA AHADI ATOA VYEREHANI 10 VETA MPANDA

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja  na wanafunzi wa VETA Mpanda wanaotoka katika mazingira magumu mara baada ya kuwakabidhi cherehani alizoahidi kuwapatia

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako ametimiza ahadi ya kutoa vyerehani 10 kwa wanafunzi waliohitimu​ mafunzo ya ushonaji kutoka Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi​ Mpanda​ wanaotoka katika mazingira magumu.
Akizungumza katika halfa hiyo Mkoani Katavi, Profesa Ndalichako amesema ahadi hiyo aliitoa​ mwaka 2018 baada ya kuwakuta vijana wadogo wamemaliza masomo ya darasa la saba na kushindwa kuendelea na masomo ya sekondari​ na kujiunga na mafunzo ya ushonaji katika chuo hicho kupitia msaada wa kanisa.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiwa katika picha ya pamoja  na wanafunzi wadogo wa VETA Mpanda wanaotoka katika mazingira magumu mara baada ya kuwakabidhi cherehani alizoahidi kuwapatia

“Mwaka juzi nilifika katika chuo hiki na kuwakuta hawa vijana wawili wadogo wakiwa katika mafunzo ya ushonaji na nilipozungumza nao niligundua kuwa wametoka katika mazingira magumu, hivyo kushindwa kuendelea na masomo ya sekondari, ndipo nilipowaahidi kuwapatia vyerehani watakapomaliza ili viwawezeshe kujiajiri.​ Hata hivyo, nimetoa vyerehani 10 ili na wengine wenye mazingira ya namna hiyo waweze kupata,” amesema Waziri Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akikabidhi fedha taslimu kiasi cha Sh. 500,000 kwa mmoja wa wanafunzi wa VETA Mpanda aliowapati cherehani  kwa ajili ya kununulia vifaa vya kuwawezesha kuanza kushona ili waweze kujiingizia kipato.
Aidha, Waziri huyo amemuagiza Mkuu wa Chuo cha Ufundi Stadi Mpanda kuona namna ya kuwapatia nafasi ya kuendelea na ngazi nyingine ya mafunzo watoto hao​ ili kuwawezesha kuwa mahiri katika ushonaji na kuhakikisha anawasimamia na kuwashauri popote watakapokuwa wanafanya shughuli zao.
Mkuu wa Chuo cha Ufundi Mpanda Elisha amemshukuru waziri kwa kutimiza ahadi aliyoitoa mwaka 2018 kwani inakwenda kuinua watoto wanaotoka katika familia masikini, na kuahidi kuendelea kuwasimamia ili cherehani hizo ziwe na manufaa kwa watoto wenyewe na familia zao.
Mhitimu wa mafunzo ya Ushonaji kutoka VETA Mpanda Gift Giles (miaka 16) kutoka katika mazingira magumu akionesha chereheni aliyokabidhiwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako
Mmoja wa wanafunzi waliopatiwa cherehani Gift Giles amemshukuru Waziri kwa kuwapatia cherehani hizo ambazo zinakwenda kubadili maisha yao kwani zitawawezesha kupata fedha ambazo zitawasaidia kujiendeleza katika masomo
Naye mmoja wa walezi wa wanafunzi hao Bibi Flora Cosmas amemshukuru Mhe. Ndalichako na kuahidi kuwasimamia ili waweze kutumia machine hizo vizuri ikiwa ni pamoja na kuwaendeleza zaidi kiujuzi.
Thabitha Venance mwenye umri wa miaka 14 aliyemaliza mafunzo ya ushonaji katika chuo cha ugundi VETA Mpanda na  anayetoka katika mazingirs magumu akiwa na cherehani aliyojabidhiwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako
"Sisi walezi wa vijana hawa tunamahukuru sana Mhe. Waziri​ kwa kuguswa kwake kuamua kwa moyo wake kufanya jambo hili kubwa maana anakwenda badili naisha ya vijana hawa ambao hawakuwa na uwezo wa kununua hizi cherehani" amesema bi Cosmas.

Jumatano, 1 Julai 2020

WAZIRI NDALICHAKO AKAGUA MIRADI YA ELIMU HALMASHAURI YA KASULU MKOANI KIGOMA

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako amekagua miradi ya elimu inayotekelezwa katika Halmashauri ya Kasulu mkoani Kigoma yenye thamani ya zaidi ya Sh. bilioni 12.

Miradi hiyo ni pamoja na  ujenzi wa Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Kasulu, Chuo cha Ualimu Kabanga na jengo la Utawala la shule ya Sekondari Grand.

Akizungumzia maendeleo​ ya ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga mara baada ya kukagua, Waziri Ndalichako amesema chuo hicho kinajengewa upya miundombinu yote​ baada ya ile ya awali kuchakaa sana na kushindwa kukarabatiwa.
Msimamizi wa Mradi wa ujenzi wa Chuo cha Ualimu Kabanga, Luteni Kanali Onesmo Njau akimweleza jambo Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako alipofanya ziara ya kukagua mradi huo mkoani Kigoma
Ameongeza kuwa ujenzi wa miundombinu ya​ chuo  hicho unagharimu zaidi ya bilioni 10, na kuwa utakapokamilika utabadili taswira ya mji huo kwa kuwa majengo yanayojengwa ni ya kisasa na imara ambayo yatadumu kwa muda mrefu.
Akizungumzia mradi wa ujenzi wa jengo jipya la utawala na utengenezaji wa mfumo wa maji katika shule ya sekondari ya Grand, Profesa Ndalichako amesema umegharimu zaidi ya Shilingi milioni 534 na kwamba utakapokamilika utaongeza morali ya walimu​ kufundisha na kusaidia wanafunzi waliopo katika shule hiyo.
Mradi mwingine uliotembelewa na Waziri wa Elimu ni ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi cha wilaya ya Kasulu ambao upo katika hatua za mwisho ambao umegharimu zaidi ya Shilingi bilioni 2.97. Jumla ya majengo 15 yatajengwa​ na kitachukua wanafunzi 320 watakaokuwa wakilala chuoni hapo.
Mhandisi Faraja Magania kutoka Chuo cha Ufundi Arusha akifafanua jambo wakati Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako alipofanya ziara ya kukagua Mradi wa Ujenzi wa Chuo cha Ufundi Kasulu.
Waziri Ndalicahko amewataka wananchi wa wilaya ya Kasulu na mkoa wa Kigoma kwa ujumla kutumia fursa ya kuwepo kwa vyuo mbalimbali katika Halmashauri hiyo kujipatia maarifa na ujuzi utakaowawezesha kuajiriwa ama kujiajiri ili kujiletea maendeleo binafsi na ya mkoa wa Kigoma.


Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Simon Anange ameishukuru Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia​ kwa namna ilivyojikita katika kupanua wigo wa elimu. Amesema kuwa katika wilaya yake kuna maeneo ambayo ni ya wafugaji na watoto hawakuwa wakienda shule lakini kwa sasa zimejengwa shule shikizi katika maeneo hayo ya mbali hivyo kuwezesha watoto kusoma na kuleta matokeo chanya.
Kanali Anange amesema baada ya Serikali kutekeleza Sera ya Elimu bila ada kumekuwa na ongezeko kubwa la wanafunzi, hivyo kupelekea Serikali kupanua​ miundombinu katika ngazi zote za elimu ili kuwezesha fursa za masomo kwa wanafunzi ikiwemo na kuongeza walimu.​
Muonekano wa hatua ya ujenzi wa moja ya jengo la Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Kasulu kilichopo Halmashauri ya Kasulu, Kigoma

Aliongeza kuwa  ujenzi wa miundombinu mbalimbali katika sekta ya elimu itawezesha vijana wa Kitanzania kupata elimu katika mazingira bora.
Naye Mratibu wa Mradi wa Uendelezaji wa Elimu ya Ualimu (TESP), Ignas Chonya amesema ujenzi wa miundombinu katika Chuo cha Ualimu Kabanga awamu ya kwanza unatarajiwa kukamilika Oktoba 2020 na chuo kitakuwa na uwezo wa kuchukua wanachuo 400 kwa wakati mmoja na kwamba chuo kinatarajiwa kuanza mafunzo mwaka huu.