Jumamosi, 29 Januari 2022

WAZIRI MKENDA AITAKA DIT KUANZA KUTENGENEZA VIPURI


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi kutoka Wizarani na Menejimenti ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) wakati alipotembelea taasisi hiyo Januari 28, 2022.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda ameitaka Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kujitanua zaidi kwa kutengeneza vipuri vya vyombo vya moto ikiwemo vya bajaji na pikipiki.

Ameyasema hayo leo Januari 28, 2022 Jijini Dar es Salaam wakati alipotembelea Taasisi hiyo ili kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa hapo ambapo amesema tunaweza kukua kiteknolojia kwa kuboresha vitu ambavyo tayari vimeshatengenezwa na nchi nyingine.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda akizungumza na Menejimenti ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) wakati alipotembelea taasisi hiyo Januari 28, 2022.

"Nimefurahi sana kuona mna kampuni inayosaidia kubiasharisha bidhaa za ubunifu ila niwatake mboreshe kwa kutengeneza vipuri ambavyo vinahitajika sana kama vya bajaji na pikipiki," amesema Prof. Mkenda.

Aidha Waziri Mkenda ameipongeza taasisi hiyo kwa kuwa na kampuni inayosaidia kubiasharisha bunifu mbalimbali na kuwataka  DIT kuhamisha ujuzi wa kiteknolojia kutoka nchi nyingine na kuja kuutumia hapa nchini katika uzalishaji wa bidhaa zitakazokidhi mahitaji ya jamii.

"Tunaweza tukaleta nchini kitu ambacho kimezalishwa mfano nchi ya Uturuki kisha tukaangalia uwezekano wa kukitengeneza na kukiuza ndani na nje ya nchi ili kukuza uchumi wetu," amesema Prof. Mkenda.

Katika hatua nyingine Waziri Mkenda ameusisitiza uongozi wa DIT kuendelea kujenga na kukuza ushirikiano na taasisi nyingine hasa za nje ya nchi ili kubadilishana wataalamu watakaosaidia kuendelea kukuza teknolojia nchini.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda (mwenye tai) akiwa ameongozana na Mkuu wa Taasisi ya DIT, Prof. Preksedis Ndomba (kushoto) na maafisa wengine kutoka Wizarani na DIT,  wakati Waziri huyo alipotembelea taasisi hiyo Januari 28, 2022.

Kwa upande wake Mkuu wa Taasisi hiyo, Prof. Preksedis Ndomba amesema wamepokea maelekezo hayo na kuahidi kuyafanyia kazi ili kuboresha utendaji wa taasisi hiyo.

Jumanne, 30 Novemba 2021

ELIMU YA MICHEZO NA SANAA KUIMARISHWA KATIKA VYUO VYA UALIMU

Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul akiongea na wananchi (hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa mashindano ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania (UMISAVUTA) uliofanyika mkoani Mtwara Novemba 29, 2021. Mashindano hayo yanaendelea hadi Desemba 5, 2021.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Profesa Joyce Ndalichako amesema kuwa Sera, Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo vitasimamiwa ipasavyo ili kuimarisha ufundishaji na  ujifunzaji wa michezo shuleni na katika Vyuo vya Ualimu.

Hayo yamesemwa kwa niaba yake Novemba 29, 2021 mkoani Mtwara na Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul wakati akifungua mashindano ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania (UMISAVUTA) yanayoendelea mkoani humo hadi Desemba 5, 2021.

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. James Mdoe akiongea na wananchi (hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa mashindano ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania (UMISAVUTA) uliofanyika mkoani Mtwara Novemba 29, 2021. Mashindano hayo yanaendelea hadi Desemba 5, 2021

Amesema Rais Samia Suluhu alitoa maelekezo ya kuboresha mitaala na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa katika nyakati tofauti ameagiza kutekelezwa kwa ufundishaji wa masomo ya sanaa na michezo,  hivyo Wizara inaendelea kutekeleza maagizo hayo ili kufikia azma ya Serikali ya kuhakikisha vipawa vya wanamichezo na Sanaa vinakuzwa kuanzia shuleni  na pia Taifa linakuwa na wananchi wenye nguvu na afya njema kuweza kulitumikia Taifa.

Baadhi ya wananchi wakimsikiliza mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul (hayupo pichani) wakati wa uzinduzi wa mashindano ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Vyuo vya Ualimu Tanzania (UMISAVUTA) uliofanyika mkoani Mtwara Novemba 29, 2021. Mashindano hayo yanaendelea hadi Desemba 5, 2021.

Aidha, katika hatua nyingine Naibu Waziri Gekul amewataka washiriki wote wa mashindano hayo kuhakikisha wanachukua tahadhari zote za maambukizi ya ugonjwa wa Uviko-19 katika kipindi chote cha mashindano hayo, na kuwahimiza kupata chanjo ya ugonjwa huo.

Mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul akipita kukagua timu mbalimbali zinazoshiriki mashindano ya UMISAVUTA yanayoendelea mkoani Mtwara.

Awali, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. James Mdoe alisema lengo la mashindano hayo ni kukuza na kuendeleza vipaji kwa walimu tarajali ili nao waweze kwenda kukuza vipaji vya wanafunzi katika michezo na sanaa.

Aidha Naibu Katibu Mkuu huyo amemuhakikishia mgeni rasmi kuwa Wizara itahakikisha mashindano hayo yatafanyika kwa nidhamu na maadili hadi yanapofikia tamati.

Naye Mwenyekiti wa Walimu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali Tanzania Bara, Mwl. Dorothy Mhaiki amesema mashindano hayo yamehusisha wanachuo 665 kutoka vyuo 36  vya ualimu vikiwemo 35 vya Serikali na kimoja binafsi.

Timu za mpira wa miguu kutoka Kanda ya Ziwa na Kanda ya Kati ndizo zilizofungua dimba la mashindano hayo ambapo timu ya Kanda ya Ziwa iliibuka na ushindi wa mabao 3 - 0.