Ijumaa, 27 Septemba 2019

OLE NASHA: MSIWAGEUZE WATOTO WA KIKE MITAJI

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amewataka wazazi kuacha kuwageuza mitaji watoto wao wa kike kwa kuwaozesha mapema na badala yake wawasaidie katika kupata elimu ili baadaye wawe msaada  kwao na taifa kwa ujumla.

Ole Nasha ameyasema hayo leo alipofanya  ziara ya kikazi wilayani Itilima mkoani Simiyu ambapo amekagua  ujenzi wa mabweni mawili ya wasichana katika shule ya sekondari Nkoma yenye uwezo wa kuchukua watoto 160 kwa wakati moja.

"Niwaambie kitu wazazi, kama unataka kumfanya mwanao wa kike mtaji basi mtaji mkubwa ni kumpa elimu na sio kumuozesha," alisema Ole Nasha.
 
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akiongea na wazazi, walezi na wanafunzi wa shule ya sekondari Nkoma iliyopo wilaya ya Itilima mkoani Simiyu.
Baadhi ya wazazi na walezi wa wanafunzi wa shule ya Nkoma wakimsikiliza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani) alipokuwa akiongea nao shuleni hapo.
Aidha Naibu Waziri Ole Nasha amewataka wazazi kuwekeza kwenye elimu ya watoto wao huku akisisitiza kuwa mtoto wa kike ana haki ya kupata elimu sawa na mtoto wa kiume, ambapo amesema katika jamii nyingi bado hawajawapa kipaumbele cha kupata elimu watoto wa kike.

"Kuna baadhi ya wazazi bado wanashawishi watoto wao kufanya vibaya katika mitihani yao ya mwisho ili wasiendelee na masomo. Nawaomba wazazi msishawishi watoto wa kike na kuwatilia vikwazo vya kukatisha masomo ili muwaozeshe. Mtoto wa kike ana nafasi ya kupata elimu sawa na mtoto wa kiume," alisema Naibu Waziri Ole Nasha.
Mwalimu Mkuu wa shule ya sekondari Nkoma, Sarah Matonya akisoma taarifa ya ujenzi wa mabweni mawili mapya mbele ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani).
Ole Nasha aliongeza kuwa serikali na wadau wa elimu wanatakiwa waendelee kutoa hamasa ya elimu kwa jamii, wanafunzi na wazazi ili miundombinu ya elimu inayojengwa iweze kutumika kwa faida ya wananchi wote katika kuboresha na kukuza elimu.

Naibu Waziri Ole Nasha amepongeza  usimamizi wa fedha za miradi ya elimu katika wilaya hiyo kutokana na kutokuwepo kwa malalamiko yoyote ya matumizi mabaya ya fedha hizo.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akizindua mabweni katika shule ya sekondari Nkoma ya wilayani Itilima mkoani Simiyu.
Awali, akisoma taarifa ya ujenzi wa mabweni hayo, Mwalimu Mkuu wa shule ya sekondari Nkoma, Sara Matonya alisema mabweni hayo yamegharimu zaidi ya shilingi milioni 300 na kwamba kukamilika kwa mradi huo wa ujenzi wa mabweni kumechochea hamasa ya wanafunzi wa kike kusoma kwa bidii kutokana na kuboreshwa kwa mazingira ya kujifunzia.


"Mabweni haya mawili yana uwezo wa kubeba wanafunzi 80 kila moja na yamesaidia wanafunzi kuondokana na adha ya kutembea umbali mrefu wa zaidi ya kilometa 10 kufika shuleni. Wanafunzi wa kike pia wameepukana na vishawishi na mimba zilizokuwa zikiwasababishia kukatisha masomo," alisema Mwalimu Matonya.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (katikati) akikagua moja ya mabweni mapya katika shule ya sekondari Nkoma iliyopo wilayani Itilima mkoani Simiyu.  Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Benson Kilangi na kulia ni Mbunge wa Itilima, Njalu Silanga.
Kwa upande wao wazazi na wanafunzi wameipongeza serikali kwa kutoa elimu bila malipo pamoja na kuwajengea mabweni, hali iliyopelekea kuongezeka kwa mahudhurio ya wanafunzi darasani, ufaulu na mwitikio wa elimu katika jamii.

"Tunaipongeza serikali kwa ujenzi wa mabweni haya ambayo yametupunguzia changamoto ya kutembea umbali mrefu na pia tumekuwa na muda mwingi wa kujifunza na kujisomea, na hivyo kutuwezesha kufanya vizuri katika masomo yetu," alisema Myano Ngusa, mwanafunzi wa shule ya sekondari Nkoma.
Mojawapo ya chumba katika bweni jipya la shule ya sekondari Nkoma ya wilayani Itilima mkoani Simiyu.
Katika ziara hiyo Ole Nasha pia alikagua ofisi ya Uthibiti Ubora wilaya ya Itilima ambazo ujenzi wake umekamilika pamoja na majengo ya VETA yanayoendelea kujengwa katika kijiji cha Kanadi wilayani humo.
Muonekano wa nje wa moja kati ya mabweni yaliyojengwa katika shule ya sekondari Nkoma ya Itilima mkoani Simiyu lenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 80 kwa wakati mmoja.
Muonekano wa nje wa jengo la ofisi za Uthibiti Ubora wilaya ya Itilima mkoani Simiyu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akikagua ofisi ya Uthibiti Ubora wilaya ya Itilima mkoani Simiyu.
Muonekano wa ndani wa chumba kimojawapo katika majengo ya VETA, Itilima mkoani Simiyu.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (mwenye skafu) akisikiliza maelezo kuhusu VETA kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Benson Kilangi.
Muonekano wa nje wa jengo la VETA la wilayani Itilima mkoani Simiyu.

Ijumaa, 20 Septemba 2019

WIZARA YA ELIMU KUWAKUTANISHA WADAU WA ELIMU ILI KUJADILI MASUALA YA ELIMU NCHINI


Waziri wa Eimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amefungua na kushiriki Mdahalo juu sekta ya Elimu uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Mjadala huo ulioandaliwa na Mwanachi Communications Ltd., (MCL) kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ulihusisha majadiliano juu ya uwezeshaji vijana katika kukuza maarifa na ujuzi mahususi.

Akifungua mdahalo huo Waziri Ndalichako amesema Serikali ya awamu ya Tano imewekeza kiasi kikubwa cha rasilimali ili kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji katika ngazi zote za elimu ili vijana wanaosoma wapate mafunzo katika mazingira yatakayowawezesha kuwa mahiri katika fani wanazosomea.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza wakati wa ufunguzi wa mjadala juu ya uwezeshaji vijana katika kukuza maarifa ulioandaliwa na Mwananchi Communications Ltd., kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia jijini Dar es Salaam.
Prof. Ndalichako ameongeza kuwa katika ngazi ya elimu ya ufundi na elimu ya juu serikali inaboresha maabara na karakana na kuweka vifaa vya kisasa ili mafunzo kwa vitendo yafanyike kwa tija na kulingana na mazingira ya sasa. Aidha ametolea mfano wa maktaba ya kisasa inayojengwa katika Chuo Kikuu cha Teknolojia Mbeya (MUST) itakayokuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 2,500 kwa mara moja ambayo inagharimu fedha za ndani zaidi ya shilingi bilioni 11.

Ndalichako amewashukuru MCL kwa kufungua njia ya kuwa na mijadala ya wazi juu ya maendeleo ya elimu na kuahidi kuandaa mjadala mwingine wa Elimu utakaohusisha wadau.  Pia amepongeza washiriki kwa kutoa maoni ambayo yana tija katika kuboresha elimu, huku akisisitiza kuwa elimu yetu inaandaa vijana mahiri ambao wanashiriki kujenga taifa.

"Humu ndani tumesikia fikra mahiri zinazotokana na vijana ambao wanasoma hapa hapa nchini na mitaala ni hii hii, hivyo tujiamini kuwa elimu yetu ni bora na inawezesha vijana kuwa mahiri katika fani mbalimbali," alisema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako akiwa na baadhi ya wadau wa Elimu wakifuatilia mjadala juu ya uwezeshaji vijana katika kukuza maarifa uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Ndalichako amesisitiza juu ya uboreshaji elimu ya ufundi ambapo amesema katika mwaka huu wa fedha vyuo vipya vya VETA 25 vinajengwa kwa shilingi bilioni 40.

Ndalichako pia amesema Serikali kupitia VETA inaendelea na programu ya kutambua na kurasimisha ujuzi kwa vijana ambapo amesema mwaka huu zaidi ya vijana 10,000 watapatiwa mafunzo kutokana na ujuzi walio nao na kupatiwa vyeti vya kurasimisha ujuzi huo. Amesema lengo la kurasimisha ni kuwatambua, kuwapa stadi na kuwaongezea ujuzi vijana walioko katika maeneo mbalimbali ambao wamekuwa wakifanya kazi za ujuzi bila vyeti.

Awali, akizungumza katika mjadala huo Mkurugenzi Mtendaji wa MCL, Francis Nanai amemshukuru Waziri Ndalichako na Viongozi wa wizara kwa kukubali kushiriki mjadala na kupokea maoni.  Amesema wao kama sekta binafsi wanalo jukumu la kushirikiana na serikali katika kusukuma mbele maendeleo kulingana na eneo lao la biashara.

Akiongea katika Mjadala huo, Prof. Lughano Kusiluka ambaye ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe amesema Vyuo Vikuu vinaandaa mitaala kulingana na uhitaji wa soko na mahitaji ya wakati.  Amewaasa vijana pia kuona umuhimu wa kutumia elimu wanayopata na vipaji walivyo navyo kubuni biashara na kujiajiri badala ya kusubiri ajira.

Kusiluka amesema Vyuo vikuu vina programu za kukuza bunifu za wanafunzi na kuziendeleza kuwa biashara kupitia Vituo Atamizi na kambi za ujasiriamali.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akibadilishana mawazo na Mkurugenzi Mtendaji wa Mwananchi Communications Ltd., Francis Nanai wakati wa  mjadala juu ya uwezeshaji vijana katika kukuza maarifa uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Naye mmoja wa washiriki, Abel Nyengo ameiomba Serikali kuhakikisha kila kijana aliyeko katika chuo anapata nafasi ya mafunzo kwa vitendo.

"Nishauri serikali kuwa mafunzo kwa vitendo iwe ni lazima na ipewe umuhimu mkubwa katika kutahini wanafunzi badala ya kutegemea mitihani,” alisema Nyengo.

Wananchi na wadau mbalimbali wametoa maoni mengi juu ya mada hiyo wakihusisha mitaala, utoaji elimu na ujuzi.

SERIKALI KUSHIRIKIANA NA WADAU WA ELIMU KUONDOA CHANGAMOTO DHIDI YA ELIMU KWA MTOTO WA KIKE

Serikali inatambua na kuthamini mchango wa Asasi za Kijamii, ikiwemo HakiElimu, katika kuweka mkazo kuhusu umuhimu wa elimu kwa mtoto wa kike kwa maendeleo ya jamii na taifa kwa jumla.
 
Kauli hiyo ya Serikali imetolewa Jijini Dodoma na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo wakati wa uzinduzi wa ripoti ya utafiti ya HakiElimu kuhusu changamoto za Elimu ya mtoto wa Kike.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo akikata utepe kuashiria uzinduzi wa ripoti ya Utafiti kuhusu wasichana kushindwa kuendelea na masomo iliyofanyika jijini Dodoma.
Dkt. Akwilapo amesema nia ya Serikali ni kushirikiana na wadau wa elimu ili kuona kuwa vikwazo vyote dhidi ya elimu kwa mtoto wa kike vinapatiwa suluhisho sahihi.

“Ili kufanya maamuzi sahihi, Wizara ninayoiongoza hutumia uthibitisho unaotokana na tafiti mbalimbali zinazofanywa na Wizara yenyewe na wadau wengine wa elimu. Sisi kama watunga sera hatuwezi kufanya kazi kwa ufanisi bila ya kutumia matokeo ya utafiti,” Alisema Dkt. Akwilapo.

Dkt Akwilapo ameipongeza Taasisi ya HakiElimu kwa kuwa mstari wa mbele katika kufanya tafiti mbalimbali ambazo zinatoa mchango mkubwa katika sekta ya elimu.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa ripoti ya Utafiti kuhusu wasichana kushindwa kuendelea na masomo iliyofanyika  jijini Dodoma. Utafiti huo umefanywa na HakiElimu ikiwa ni utekelezaji wa Mpango Mkakati wao katika kumsaidia mtoto wa kike kupata elimu bora.
“Ripoti ya utafiti ninayoizindua leo ni mfano hai wa kile ninachokisema kuhusu mchango wa Sekta binafsi kwani inahusu changamoto zinazosababisha wasichana kushindwa kuendelea na masomo na kuvuka katika hatua nyingine. Utafiti huu unaendana na lengo la Serikali la kuhakikisha kuwa wasichana wanaoandikishwa katika Elimumsingi wanamaliza safari yao ya elimu kwa mafanikio makubwa,” aliongeza Dkt. Akwilapo.

Akizungumzia jitihada zinazofanywa na Serikali katika kuhakikisha mtoto wa kike anapata elimu Dkt. Akwilapo amesema Serikali imekuja na Sera ya Elimu bila malipo katika ngazi ya Elimumsingi ambayo imewezesha wasichana wengi kuandikishwa katika shule ikiwa ni pamoja na Ujenzi wa mabweni ambayo yamesaidia kuwaweka wasichana karibu na shule na kuepuka vishawishi vya barabarani wakati wa kwenda na kurudi shule.
Baadhi ya Wanafunzi na Wajumbe walioshiriki katika hafla ya uzinduzi wa ripoti ya Utafiti kuhusu wasichana kushindwa kuendelea na masomo wakifuatilia hotuba ya Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo jijini Dodoma.
Jitihada nyingine ni kutunga sheria ambayo inawabana watu wanaotaka kuoa watoto wa shule au kushirikiana nao kimapenzi, na hivyo kuwaharibia masomo kwa kuwapa ujauzito pamoja na kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa elimu kwa mtoto wa kike.
Mkurugenzi Mtendaji HakiElimu, Dkt. John Kalaghe akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa ripoti ya Utafiti kuhusu wasichana kushindwa kuendelea na masomo iliyofanyika Jijini Dodoma.
Naye Mkurugenzi Mtendaji HakiElimu, Dkt. John Kalaghe amesema azma ya kufanya utafiti huu imechagizwa na kampeni ya Elimu ya mtoto wa kike ambayo HakiElimu inaifanya.  Amesema kampeni hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango mkakati wa mwaka 2017 hadi 2021 ambao wamejiwekea na umejikita katika kushirikiana na Serikali pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha kwamba watoto wa kitanzania wakiwemo watoto wa kike wanapata elimu bora itakayowawezesha kukabili changamoto katika maisha yao na kusaidia ujenzi wa Taifa letu.

“HakiElimu tunatilia mkazo katika kuhamasisha utolewaji wa elimu jumuishi yenye ubora na usawa pamoja na elimu kwa watoto wa kike ikiwa ni pamoja na kupunguza au kuondoa kabisa unyanyasaji wa watoto shuleni na nje ya mipaka ya shule,” Alisema Dkt. Kalaghe.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa hafla ya uzinduzi wa ripoti ya Utafiti kuhusu wasichana kushindwa kuendelea na masomo iliyofanyika Jijini Dodoma.