Jumapili, 27 Septemba 2020

KAMUSI YA KWANZA YA LUGHA YA ALAMA YA KIDIJITALI YAZINDULIWA

KAMUSI YA KWANZA YA LUGHA YA ALAMA YA KIDIJITALI YAZINDULIWA

 Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imezindua Kamusi ya kwanza ya lugha ya alama ya kidijitali yenye lengo la kupunguza changamoto ya mawasiliano katika ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi viziwi. 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu akizungumza wakati wa  uzinduzi wa Kamusi ya kwanza ya Lugha ya Alama ya kidijitali ya Tanzania na Mwongozo wa Utekelezaji wa Mtaala wa Elimu ya Sekondari kwa wanafunzi viziwi wakati wa kikele cha maadhimisho ya viziwi yaliyofanyika Mkoani Tabora

Akizindua kamusi hiyo Mkoani Tabora, katika kilele cha maadhimisho ya wiki ya viziwi yenye kauli mbiu “Kuhakikisha upatikanaji wa haki za binadamu kwa Viziwi”, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Ave Maria Semakafu amesema serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa makundi yote yenye ulemavu kupata elimu na huduma nyingine za kijamii. 

Dkt Semakafu amesema pamoja na maboresho makubwa yaliyofanyika katika sekta ya elimu, kundi la viziwi lilikuwa limeachwa nyuma huku changamoto kubwa ikiwa ni mawasiliano na kutokuwepo kwa walimu wa kutosha hasa katika ngazi ya sekondari ndio maana imeandaa kamusi hiyo kuwe na lugha moja ya alama na kutoa mafunzo kwa walimu wanaofundisha katika shule zinazopokea watoto viziwi. 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu akizindua Kamusi ya kwanza ya Lugha ya Alama ya kidijitali ya Tanzania na Mwongozo wa Utekelezaji wa Mtaala wa Elimu ya Sekondari kwa wanafunzi viziwi wakati wa kilele cha maadhimisho ya wiki ya viziwi  yaliyofanyika Mkoani Tabora

“Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na lugha moja ya alama kwa ajili ya kuwezesha mawasiliano ya watumiaji wa lugha hiyo, hivyo itaendelea kusimamia uendelezaji na usanifishaji wa lugha ya alama ili kuwezesha utoaji elimu, kurahisisha ujifunzaji na kuboresha mawasiliano katika jamii.,”alisema Naibu Katibu Mkuu huyo.

Nae Kamisha wa Elimu Dkt. Lyabwene Mtahabwa amesema kilele cha maadhimisho ya wiki ya viziwi duniani ndio mwanzo wa mafanikio katika mchakato wa ujifunzaji na ufundishaji nchini kwani ni siku ambayo kamusi ya lugha ya alama ya kwanza nchini tena ya kidijitali inazinduliwa pamoja na mwongozo wa utekelezaji wa mtaala wa elimu ya sekondari kwa wanafunzi viziwi.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu akionesha kishkwambi chenye kamusi huku Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Elimu Tanzania Dkt. Magret Komba akionesha Mwongozo wa Utekelezaji wa Mtaala wa Elimu ya Sekondari kwa wanafunzi viziwi mara baada ya kuzinduliwa katika kilele cha maadhimisho ya viziwi yaliuofanyika Mkoani Tabora

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu Tanzania(TET)Dkt. Aneth Komba  anasema Taasisi anayoisimamia ndio walipewa jukumu la kuandaa Kamusi hiyo  na kwamba imeandaliwa kwa kufata taratibu zote ikishirikisha wadau wote na kwamba itatumiwa na wanafunzi viziwi kutoka Tanzania Bara na Visiwani. 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ave Maria Semakafu akiwa kwenye picha ya pamoja na wanafunzi viziwi walioshika vishkwambi vyenye Kamusi ya Lugha ya Alama mara  baada ya kuzindua kamusi hiyo katika kilele cha maadhimisho viziwi yaliyofanyika  Mkoani Tabora

Mkurugenzi wa Kitengo cha Elimu Maalum kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Magret Matonya amesema uzinduzi wa Kamusi hiyo ni muendelezo wa jitihada za Serikali kuhakikisha wanafunzi wenye mahitaji maalum nchini wakiwemo viziwi wanapata elimu bora. Aidha ameongeza kuwa  Wizara imeanza ujenzi wa shule ya mfano ya viziwi  katika Halmashauri ya Masasi Mkoani Mtwara ikiwa ni jitihada za kuboresha mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji wanafunzi viziwi ambapo ujenzi wake utagharimu bilioni 1.5.

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Viziwi Taifa (CHAVITA) Selina Mlemba amesema wanaishukuru Serikali kwa hatua hiyo na kwamba wanaamini miaka michache ijayo watapata wataalamu wengi katika maeneo mbalimbali wakiwemo madaktari kwa kuwa sasa wamepata kamusi itakayowawezesha kusoma bila changamoto.

Mtaalamu elekezi wa uandaaji wa Kamusi ya lugha ya alama kutoka Archbishop Mihayo University College (AMUCTA) Profesa Henry Muzale amasema uaandaji wa kamusi hiyo umezingatia changamto zote za viziwi na hii ni kutokana na utafiti uliofanyika katika shule zenye watoto viziwi ikiwemo Njombe viziwi ambao  ufaulu wao uliendelea kushuka.

Wadau, wanachama wa Chama cha Viziwi Taifa wakiwa kwenye maandamano wakati wa kilele cha maadhimisho ya wiki ya viziwi iliuofanyika Mkoani Tabora

Kilele cha maadhimisho ya wiki ya Viziwi duniani kitaifa yamefanyika mkaoni Tabora ikiwa ni hatua ya kuenzi historia ya chimbuko la elimu kwa viziwi kwani shule ya kwanza ya viziwi nchini Tanzania ilianzishwa katika mkoa huo katika shule ambapo maadhimisho yamefanyika.

Jumamosi, 26 Septemba 2020

UZINDUZI WA MKAKATI WA KITAIFA WA KUKUZA NA KUENDELEZA KISOMO NA ELIMU KWA UMMA

 Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) imezindua Mkakati wa miaka mitano wa Kitaifa wa Kukuza na Kuendeleza Kisomo na Elimu kwa Umma.

Uzinduzi wa Mkakati huo ambao unaanza kutumika mwaka 2020 hadi 2025 umefanywa na Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa James Mdoe Jijini Dar es Salaam katika Ofisi za Tasisi ya Elimu ya Watu Wazima.(TEWW)

Akiongea katika uzinduzi huo, Prof. Mdoe amesema kuwa anaamini Mkakati huo utapunguza au kumaliza kwa kiasi kikubwa idadi ya Watanzania wasiojua Kusoma, Kuandika na Kuhesabu.

“Naamini Mkakati huu uliozinduliwa leo utakwenda kumaliza au kupunguza kwa kiasi kikubwa idadi ya watu wasiojua kusoma, kuandika na kuhesabu," amesema Prof. Mdoe.

Naibu Katibu Mkuu Mdoe pia ameitaka TEWW kuhakikisha kuwa wanaendesha programu ambazo zinaendana na mahitaji ya jamii na mabadiliko ya teknolojia.

"Niwaombe Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima mjiongeze, muwe wabunifu, muendeshe programu zinazoendana na mahitaji ya jamii na mabadiliko ya teknolojia ambayo kwa sasa inakua kwa kasi," amesisitiza Prof. Mdoe.

Naye Mkurugenzi wa TEWW, Dkt. Michael Ng'umbi akiongea katika uzinduzi huo amesema Taasisi yake imeboresha mtaala ambapo sasa wanafunzi watakaosoma chuoni hapo watafanya mafunzo kwa vitendo kwa kipindi cha Semista nzima na watatakiwa kuanzisha vituo vya kufundisha vijana na watu wazima.

"Tumeboresha mtaala ambapo kwa sasa wataalamu wanaopata elimu hapa chuoni, kila mmoja atatakiwa kuanzisha kituo cha kufundisha elimu ya watu wazima. Hata kama kila mmoja atamfundisha mtu mmoja, tukiwa wanafunzi 6,000 tuna uhakika idadi kama hiyo ya watu wazima watapata mafunzo na kuondokana na kutokujua kuandika, kusoma na kuhesabu," amesema Dkt. Ng'umbi.

Jumatatu, 14 Septemba 2020

MKUTANO WA BARAZA LA WAFANYAKAZI

 Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo amewataka wajumbe wa Baraza la  Wafanyakazi wa Wizara hiyo kutambua kuwa wana wajibu wa kuishauri Wizara na Serikali ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kunakuwa na utekelezaji sahihi wa Dira, Dhima na Majukumu ya Wizara. 

Dkt. Akwilapo ameyasema hayo Jijini Mwanza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 27 wa Baraza la 10 la Wafanyakazi wa Wizara hiyo ambapo amesema wajibu wa mabaraza kama vyombo vya ushauri na usimamizi ni kuhakikisha kuwa waajiri na watumishi wanatambua wajibu na haki zao na wanazingatia maadili ya utumishi wao ili kuleta matokeo makubwa ya utendaji kazi yenye tija.

“Moja ya kazi za Baraza ni kuhakikisha kuwa watumishi wanatekeleza wajibu wao kwanza kabla ya kudai maslahi na wanapodai maslahi wanatakiwa kufuata misingi ya sheria na taratibu zilizopo,” alisema Dkt. Akwilapo.

Kiongozi huyo aliongeza kuwa kuwepo kwa Baraza la wafanyakazi ni matokeo ya Sera ya kuwashirikisha Wafanyakazi katika uongozi wa pamoja mahali pa kazi na kwamba kufanyika kwa Mkutano wa Baraza ni kutekeleza maagizo, Sheria na Kanuni mbalimbali za ushirikishwaji na Majadiliano ya pamoja katika Utumishi wa Umma za mwaka 2003, 2004 na 2005.

Dkt Akwilapo amewataka wajumbe wa Baraza pindi watakaporejea katika vituo vyao vya kazi kuwaelimisha watumishi wenzao umuhimu wa kutimiza wajibu wao ili kufikia malengo mapana ya wizara kwani njia pekee ya kufikia malengo hayo ni kila mmoja kufanya kazi kwa bidii na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma. 

Katibu Mkuu Akwilapo ametumia fursa hiyo kuwapongeza Viongozi na Watumishi wa Wizara hiyo kwa kuwa sehemu kubwa ya kuwezesha utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya kuboresha Sekta ya Elimu hususan katika kipindi hiki cha uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.

Kwa upande wake Katibu wa Baraza Graciana Shirima  ameishukuru Menejimenti ya Wizara kwa kuhakikisha Mkutano wa Baraza unafanyika kwa wakati na kwamba Baraza jipya lina jumla ya wajumbe 66 waliopatikana kufuatia makubaliano yaliyosainiwa kwa  mkataba wa Baraza la Wafanyakazi kati ya Vyama vya Wafanyakazi TUGHE na CWT kwa upande mmoja  na menejimenti ya Wizara kwa upande mwingine.

KATIBU MKUU DKT AKWILAPO AAGIZA KUFANYIKA TATHMINI YA MAZINGIRA NA MIUNDO MBINU YA SHULE ZOTE

 Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt Leonard Akwilapo amewataka Wathibiti Ubora wa shule nchini kufanya tathmini ya mazingira na miundombinu ya shule katika kudhibiti majanga ya moto yaliyokithiri katika siku za hivi karibuni.

 Dkt Akwilapo amesema hayo kufuatia tukio la moto lililosababisha vifo vya wanafunzi 10 na kujeruhi wengine lililotokea katika shule ya Msingi Byamungu Islamic iliyoko Kyerwa Mkoani Kagera.

Akwilapo amewataka Wathibiti ubora wa shule kushirikiana na wataalamu kubaini vyanzo vya moto katika shule  na amesema sheria zipo na pindi shule itakapogundulika kukiuka taratibu wasisite kuzichukulia hatua.

 “Asubuhi ya leo tumepokea taarifa ya kuungua kwa shule ya msingi ya Byamungu  na watoto wamepoteza maisha, lakini matukio haya yamekuwa yanaongezeka hivyo kama Wizara tunawajibu kuhakikisha hili linapatiwa suluhisho kwa kutumia wataalamu,"aliongeza Dkt. AKwilapo

Aidha Dkt.Akwilapo amesema Wathibiti Ubora wa shule zaidi ya 400 wameajiriwa mmepewa ofisi na vitendea kazi, nataka kuona mabadiliko ya namna tunavyosimamia shule”alisisitiza Dkt. Akwilapo.

Katibu Mkuu Akwilapo ametumia fursa hiyo kutoa pole kwa wazazi, walezi na Shule ya Msingi Byamungu iliyopo mkoani Kagera kwa kuondokewa na wanafunzi na kuwatakia uponyaji wa haraka majeruhi 6 ambao wanaendelea na matibabu.

Jumatano, 2 Septemba 2020

DR. LEONARD AKWILAPO ATAKA TAASISI ZA ELIMU YA JUU KUANZISHA PROGRAMU ZA VIPAUMBELE VYA TAIFA

 Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo ametoa wito kwa Vyuo Vikuu nchini kuhakikisha vinaanzisha programu za masomo zinazoendana na vipaumbele vya kitaifa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akifungua  maonesho  ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam

Dkt. Akwilapo ametoa wito huo Jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa maonesho ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia ambapo amesema kwa kuanzisha programu hizo nchi itaongeza ujuzi wa wataalamu na pato la taifa. 

Kiongozi huyo ametaja baadhi ya programu za kipaumbele kuwa ni mafuta na gesi, afya, hususani udaktari bingwa kwa ngazi za Uzamivu katika nyanja zote za magonjwa ya upasuaji wa ubongo na mishipa ya fahamu, upandikizaji figo, ini na uboho (bone marrow), tiba za ndani za moyo, na uhudumiaji wa wagonjwa wa dharura na mahututi (emergency medicine and critical care).


 “Tusingependa kama nchi kupeleka wagonjwa wetu nchi za nje kutibiwa, bali nchi za nje waje kutafuta tiba kwetu (medical tourism). Kwa kufanya hivyo tutaongeza ujuzi wa wataalamu wetu pamoja na pato la taifa,” amesisitiza Dkt. Akwilapo. 

Katibu Mkuu Akwilapo ameongeza kuwa pamoja na kuanzisha programu za vipaumbele, nchi kwa sasa inatekeleza miradi mingi mikubwa ambayo inahitaji wasomi wa kuendesha na kusimamia miradi hiyo, hivyo ni jukumu la Taasisi za Elimu ya Juu kuhakikisha hili linafanyika kwa ufanisi wa hali ya juu kwa kuhakikisha wanatoa elimu bora na kwamba Serikali itaendelea kusomesha kwa wingi wataalamu katika fani na ujuzi adimu na maalum kwa mahitaji ya nchi. 

Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akiwa katika picha ya pamoja na wakuu wa vyuo mbalimbali vya elimu ya Juu nchini mara baada ya kufungua maonesho  ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam

“Ni jambo la kutia moyo kuona kwamba hivi sasa baadhi ya vyuo vikuu vimeanza kuelekeza jitihada zao katika kutoa elimu ambayo inalenga kushughulikia changamoto za jamii na kuweka msisitizo katika maeneo ya kimkakati ya nchi kama vile Kilimo, Madini, Utalii, Uvuvi, Maliasili na Misitu na Afya,” amesema Dkt. Akwilapo.  

Katika hatua nyingine Dkt. Akwilapo ameendelea kuzitaka Taasisi za Elimu ya Juu kuona namna bora ya kupanua udahili wa wanafunzi wa elimu ya juu kutokana na ongezeko la udahili wa wanafunzi katika ngazi ya msingi na sekondari na kwamba wanapohitimu lazima wapate nafasi katika vyuo vya kati na vya juu ili kuweza kuwapa ujuzi wa kujiajiri na hivyo kuchangia kikamilifu katika ujenzi wa Taifa. 

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Tume ya Vyuo Vikuu nchini, Profesa Mayunga Nkunya  amesema Tume pamoja na mambo mengine imefanikiwa kuimarisha mfumo wa utoaji ithibati ya mtaala, jambo ambalo lilionekana kuwa tatizo kwa muda mrefu na kwamba itaendelea kutekeleza majukumu yake ya kuwatumikia Watanzania katika sekta ya elimu ili kuhakikisha Watanzania wa ngazi zote wanapata elimu bora yenye kukidhi viwango vya ubora Kitaifa, Kikanda na Kimataifa.

Naye Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini, Profesa Charles Kihampa amesema lengo la maonesho hayo ni kutoa fursa kwa vyuo vikuu kujitangaza na kuonesha huduma na kazi wanazofanya pamoja na mchango wao katika ustawi wa elimu ya juu kwa mustakabali wa maendeleo ya sayansi, teknolojia na manuufaa yake kiuchumi na kijamii. 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi waliotembelea maonesho hayo wamesema wamefurahishwa na kuwepo kwa maonesho hayo kwani yanatoa fursa ya kuonana na wahusika na kupata taarifa zinazowawezesha kuomba programu zinazoendana na ufaulu wao.

Jumla ya taasisi 67 za elimu ya juu zimeshiriki katika maonesho hayo.

Brass Band ikitumbuiza wakati wa ufunguzi wa maonesho ya 15 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika Jijini Dar es Salaam

Jumanne, 1 Septemba 2020

WALIMU 100 NCHINI KUFUNDISHWA MBINU ZA KUFUNDISHIA LUGHA YA KIFARANSA

Serikali za Tanzania na Ufaransa zimeingia makubaliano ya kutoa mafunzo ya mbinu za kufundishia lugha ya Kifaransa kwa walimu 100 nchini ambao watakuwa na uwezo wa kufundisha wanafunzi 5,000 wa Kitanzania katika ngazi ya sekondari.

Makubaliano hayo yamefikiwa katika kikao kati ya Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Frederic Clavier na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo kilichofanyika Jijini Dar es Salaam ambapo jumla ya Dola za Kimarekani 250,000 zitatumika ili kufanikisha mpango huo.
Katika kikao hicho wamekubaliana kufanyika kwa vikao vya kitaalamu kati ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Kituo cha Ubalozi wa Ufaransa (Alliance Francais) ili kupanga utekelezaji wa mafunzo hayo ya walimu.

Aidha, Balozi Clavier ameonesha kuwepo kwa fursa za Watanzania kusoma programu zisizopungua 2,000 za Kiingereza nchini Ufaransa. Ameeleza kuwa  Ufaransa inaandaa Maonesho ya Elimu ya Juu (Higher Education Fair) yatakayofanyika nchini Mei 2021 ambapo vyuo 20 vya Ufaransa vitashiriki kutafuta ushirikiano na Vyuo Vikuu vya Tanzania na Sekta binafsi. 
Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu Akwilapo ameushukuru Ubalozi wa Ufaransa kwa kuendeleza ushirikiano katika kukuza na kuimarisha elimu ya Juu nchini kupitia ufadhili wa mafunzo hayo na kuagiza wahusika katika Wizara anayoisimamia kuhakikisha vikao vya kitaaluma vinafanyika ili mafunzo hayo yaweze kuanza kwa wakati uliopangwa.

Katibu Mkuu Akwilapo pia ameahidi kuweka wazi kwa Watanzania kuhusu kuwepo kwa fursa hiyo ya kusoma programu za Kiingereza nchini Ufaransa ili Watanzania waweze kuchangamkia fursa hiyo.

SEMAKAFU: VYUO VYA FDC TOENI MAFUNZO YENYE UHITAJI NA AJIRA

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu amevitaka Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDCs) kujikita katika kutoa mafunzo ya fani zinazopendwa na zinazotoa ajira badala ya kuendelea kuwa na fani ambazo hazina wanafunzi katika eneo husika.


Dkt. Semakafu ametoa agizo hilo alipofanya ziara ya kukagua ukarabati na uendeshaji wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same kilichopo Mkoani Kilimanjaro ambapo amesema ni vizuri vyuo  vikajiimarisha kwenye utoaji mafunzo kwa fani zenye wanafunzi  wengi na kuachana na zile zenye wanafunzi wachache.
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akizungumza na baadhi ya watumishi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same baada ya kukagua ujenzi na ukarabati wa miundombinu chuoni hapo.

“Kuanzia mwaka huu, kila chuo cha wananchi kitafundisha fani ambazo zinahitajika katika maeneo husika kwa maana ya kuwa na wanafunzi wa kutosha, hakuna chuo chochote kusajili fani ambazo zina wanafunzi wachache ama chini ya kumi na mbili, Serikali haiajiri walimu kufundisha wanafunzi wawili hivyo hakuna haja ya kuweka fani ambazo hazina wanafunzi wa kutosha,” amesisitiza Dkt. Semakafu.

Aidha, Naibu Katibu Mkuu huyo amesema mpango wa 'Elimu haina mwisho' unaotolewa katika vyuo hivyo ni utaratibu wa kutoa fursa kwa watoto waliokatisha masomo kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za kiuchumi na kijamii ili kuwasaidia kupata elimu na ujuzi wa kuwawezesha kuendelea na masomo na kuendesha maisha yao pindi watakapohitimu hivyo wanapaswa kufundishwa kama wanafunzi wengine bila kuwatenga.  
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu akitoa maelekezo ya namna ya kuboresha eneo la utoaji wa mafunzo ya umeme wa magari kwa Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi, Edward Mdee.

Amesema Serikali iliamua watoto hao wasome katika vyuo hivyo kupitia mfumo usio rasmi bila malipo yoyote kwa lengo la kuhakikisha wanapata fursa nyingine ya kuendelea na masomo na kuutaka Uongozi wa chuo cha Maendeleo Same  kuwarudisha chuoni wanafunzi wote walioacha masomo kwa sababu mbalimbali ili waweze kumaliza masomo yao.

“Tumeanza programu hii kwa lengo la kupata watoto wote walioacha shule na ndio maana unaona hata wasichana walioacha shule kutokana na changamoto mbalimbali tumewarudisha katika mfumo huu ili waje waendelee na masomo na na wale wenye watoto hata tuna shule za chekechea kwa ajili ya watoto wao,” amesema Dkt. Semakafu.

Naibu Katibu Mkuu Dkt. Semakafu amekagua miundombinu iliyokarabatiwa na kuboreshwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambapo ameuagiza uongozi wa chuo hicho kufanya marekebisho katika baadhi ya miundombinu ambayo haikukarabatiwa vizuri.
Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii Same, Edward Mdee akitoa taarifa  ya chuo hicho kwa Naibu Katibu Mkuu, Dkt. Ave Maria Semakafu alipofika chuoni hapo kukagua maendeleo ya chuo hicho.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same, Edward Mdee  ameishukuru Wizara kwa ukarabati ambao umefanyika chuoni hapo, na kusema kuwa chuo hicho chenye wanafunzi 301 kipo katika mkakati wa kuboresha utoaji wa mafunzo ili kuhakikisha kinatoa vijana wenye ujuzi na maarifa yatakayowawezesha vijana wa Same kujiajiri ama kuajiriwa.
Muonekano wa baadhi ya majengo ya miundombinu ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Same yaliyojengwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.