Jumatatu, 30 Julai 2018

WATHIBITI UBORA WA SHULE NCHINI WAPATIWA MAFUNZO YA MFUMO MPYA WA UKAGUZI WA SHULE


Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeanza kutoa mafunzo kwa wathibiti ubora wa shule kote nchini ya namna ya kutekeleza mfumo mpya wa Uthibiti Ubora wa Elimu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Jijini Dodoma Mthibiti Mkuu wa Shule kutoka Wizara hiyo Euphrasia Buchuma amesema mfumo huo unaondoa mfumo ambao wathibiti ubora wamekuwa wakitazamwa kama polisi pindi wanapofika shuleni na kuwa watu ambao wanatakiwa kutoa msaada katika shule.

Buchuma amesema mfumo huo mpya unashirikisha jamii nzima ya shule Viongozi wote, Wazazi, Kamati za Shule, Bodi ya shule na walimu ambao wanapaswa kufahamu Mthibiti Ubora wa Shule anapoingia katika Shule anafanya nini katika shule hiyo na taarifa za ukaguzi ni lazima ziwafikie viongozi wote wenye mamlaka na kutoa maamuzi.

Amesema kwa kuwa mfumo huu ni shirikishi unaleta uwazi zaidi na kuondoa usiri ambao ulikuwapo katika mfumo uliokuwa ukitumika zamani katika kukagua shule ambao uliitaji usiri kuanzia unapokagua shule uandikaji wa ripoti na hata uwasilishaji wa taarifa ya ukaguzi.

Mthibiti Mkuu wa Shule kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Euphrasia Buchuma akiongea na Wathibiti Ubora wa Shule wakati wa ufunguzi wa mafunzo eelekezi ya namna ya kutumia mfumo mpya wa ukaguzi wa Shule Jijini Dodoma.

Amewataka wathibiti ubora wa shule kushiriki mafunzo hayo kikamilifu kwa kuwa wana dhamana kubwa ya Elimu na kwamba kila mmoja kwa nafasi yake atambue wajibu wake, abadili mtizamo, afanye kazi kwani kunahitajika mabadiliko makubwa katika kuhakikisha Elimu ya nchi hii inatolewa kama inavyopaswa kutolewa.

“Tumekuwa tukinyooshewa vidole sana kwamba hatufanyi kazi na ni kwa sababu matokeo yanaonekana kama hatupo kumbe tupo, hatuonekani katika utendaji kazi na ndio maana kila panapotokea tatizo tunaonekana hatupo na hatufanyi kazi tubadilike tufanye kazi kwa moyo, bidii na weledi,” alisisitiza Buchuma
Baadhi ya Wathibiti Ubora wa Shule wakifuatilia hotuba ya Mthibiti Mkuu wa Shule kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Euphrasia Buchuma wakati wa ufunguzi wa mafunzo elekeze kwa Wathibiti Ubora wa Shule ya nama ya kutumia mfumo mpya wa ukaguzi wa Shule.
                                    
Katika hatua nyngine Buchuma amewataka wathibiti ubora wa shule mara baada ya mafunzo hayo kukamilika, wahakikishe wanakagua Shule zote za Sekondari ambazo ni Kongwe kwani zinaonesha kutofanya vizuri katika miaka ya hivi karibuni.

“leo ukienda katika shule nyingi ukiukwaji wa sheria za Shule ni mkubwa lakini na sisi tupo na hatusemi tunasema hatuhusiki, kimsingi sisi ndio wasimamia Sera, Miongozo, taratibu na kanuni zote za uendeshaji wa shule kuanzia ngazi ya Shule za Awali, Msingi, Sekondari na Vyuo vya Ualimuhivyo tukafanye kazi,” aliongeza Buchuma

Mafunzo elekezi ya namna ya kufanya ukaguzi kwa mfumo mpya wa uthibiti ubora wa Shule yanafanyika kwa siku nne kuanzia Julai 30, mwaka huu nchi nzima.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni