Jumatatu, 11 Machi 2019

SERIKALI IMEIMARISHA USIMAMIZI NA UDHIBITI WA MATUMIZI SALAMA YA TEKNOLOJIA YA NYUKLIA NCHINI



Serikali ya Tanzania kupitia Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) imefanikiwa kuimarisha usimamizi na udhibiti wa matumizi ya Teknolojia ya Nyuklia nchini.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekenolojia Mheshimiwa William Ole Nasha wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa kimataifa wa waratibu wa miradi ya Sayansi na Teknolojia ya Nyuklia kutoka nchi 46 wanachama wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (IAEA) unaofanyika jijini Arusha.
Mkurugenzi wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania, Profesa Lazaro Busagala akitoa taarifa na neno la ukaribisho kwa Wajumbe wa Mkutano wa Kimataifa wa Waratibu wa Miradi ya Sayansi na Teknolojia ya Nyuklia kutoka nchi 46 wanachama wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (IAEA).
Naibu Waziri Ole Nasha amesema Shirika hilo linafadhili miradi mingi katika sekta mbalimbali hapa nchini ikiwemo sekta ya afya ambapo imewezesha kupatikana kwa vifaa mbalimbali vya uchunguzi wa tiba na maradhi ya saratani ambavyo vimefungwa katika hospitali ya Rufaa ya kanda ya ziwa, Bugando jijini Mwanza na Hospitali ya Ocean Road jijini Dar es Salaam.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe William Ole Nasha (Kushoto) akifurahia jambo na Mkurugenzi wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki, Profesa Shaukat Abdulrazak katika Mkutano huo.
Pamoja na vifaa vya uchunguzi katika hospitali hizo mbili, pia taasisi nyingine mbalimbali zimepata vifaa vya maabara ambapo kwa ujumla wake vifaa vyote vina thamani ya kiasi cha Shilingi za Tanzania Bilioni 6.2 na pia kutoa mafunzo kwa wataalamu katika eneo la matumizi ya mionzi na teknolojia ya Nyuklia, mpango ambao uligharimu Shilingi za Tanzania Bilioni 3.3.

Mhe Ole Nasha amelishukuru na kulipongeza shirika hilo kwa kuendelea kuimarisha ushirikiano baina ya mataifa wanachama hususan kwa utaratibu wake wa kuwa na mikutano inayowezesha kubadilishana uzoefu baina ya wanachama.  Amewataka washiriki wa mkutano huo kuhakikisha wanafanya majadiliano yenye tija kwa lengo la kusaidia nchi zao kwenye udhibiti na matumizi salama ya teknolojia ya Nyuklia.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe William Ole Nasha akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano wa kimataifa wa Waratibu wa miradi ya Sayansi na Teknolojia ya Nyuklia kutoka nchi 46 za Kanda ya Afrika, wanachama wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (IAEA).

“Majadiliano yenu yalenge katika kuhakikisha mionzi na teknolojia ya Nyuklia katika Afrika inatumika vizuri kwa maendeleo,” alisema Ole Nasha.

Mheshimiwa Naibu Waziri ametumia nafasi hiyo pia kuwakaribisha sana washiki nchini Tanzania na kuwashauri kutembelea vivutio vya kitalii zikiwemo Mbuga za wanyama.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Nguvu za Atomiki Duniani (IAEA), Profesa Shaukat Abdulrazak amesema wataendelea kushirikiana na serikali ya Tanzania katika kuhakikisha kunakuwa na matumizi salama ya teknolojia ya Nyuklia kwenye sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya Afya, Kilimo, Mifugo, Maji, Viwanda na Ujenzi.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe William Ole Nasha akiwa katika picha ya pamoja na Washiriki wa Mkutano wa kimataifa wa Waratibu wa miradi ya Sayansi na Teknolojia ya Nyuklia kutoka katika nchi wanachama 46 wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (IAEA).
Nae Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania, Profesa Lazaro Busagala amesema taasisi yake imeendelea kudhibiti na kuwachukulia hatua za kuwafungia taasisi zinazokiuka taratibu za matumizi salama ya mionzi na teknolojia ya Nyuklia hapa nchini ikiwemo kutokuwa na leseni, kutokuwa na wafanyakazi wenye utaalamu wa matumizi ya mionzi na teknolojia ya Nyuklia na Mionzi.
 
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe William Ole Nasha akisalimiana na Waziri Msaidizi, anayeshughulikia Mashirika ya Nje katika Wizara ya Mambo ya Nje nchini Liberia, Mhe Yaba Freeman Thompson ambaye pia ni Mratibu wa mradi nchini humo na mshiriki katika Mkutano wa kimataifa wa Waratibu wa miradi ya Sayansi na Teknolojia ya Nyuklia Kanda ya Afrika mara baada ya ufunguzi wa Mkutano huo.
Akitoa mfano wa Hospitali amesema mwaka 2018 walifungia hospitali 112 zilizoshindwa kufuata masharti hayo, katika hizi tayari hospitali 40 zimekidhi na kufunguliwa huku hospitali 72 zikiwa bado zimefungiwa kutumia vifaa vinavyotumia mionzi.

Mkutano huo wa siku tano utamalizika tarehe15 Machi, 2019.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni