Jumatano, 16 Septemba 2015


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
MAONESHO YA MATUMIZI YA TEHAMA KATIKA ELIMU YA MSINGI
Wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi inaandaa maonesho ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ajili ya kuongeza Ufanisi katika Ujifunzaji na Ufundishaji katika Elimu ya Msingi nchini.
Maonesho haya yanalenga kutoa fursa kwa wabunifu, wauzaji na wadau wa elimu kuonesha bunifu mbalimbali za teknolojia ya habari na mawasiliano zitakazoweza kutumiwa katika Elimu ya Msingi ili kuongeza ufanisi katika Ujifunzaji na Ufundishaji wa stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) na katika masomo mengine.
Maenesho haya yatafanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere mkoani Dar es Salaam, kuanzia tarehe 28/9/2015 hadi tarehe 02/10/2015
Washiriki wa maonesho haya wanatakiwa kujiandikisha kupitia wavuti: www.lanes-moe.go.tz, kabla ya tarehe 24/9/2015. Aidha, washiriki watakaokidhi vigezo vinavyotakiwa, kazi zao zitatumika katika Ujifunzaji na Ufundishaji katika Elimu ya Msingi Nchini.
Wizara inawahimiza wabunifu wote  wa ndani na nje ya nchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika maonesho haya.
Imetolewa na
Katibu Mkuu
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi
13/09/2015

Jumatatu, 10 Agosti 2015

Serikari yakabidhiwa Shule ya Sekondari

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Mhe.Dkt. Shukuru Kawambwa amekabidhiwa shule ya sekondari na Balozi wa Korea Kusini Mhe. Chung Il iliyojengwa na Shirika la Good Neighbors International na Washirika wake. Shule hiyo ya sekondari ya Fukayosi imejengwa wilayani Bagamoyo, mkoani Pwani kwa msaada wa mashirika mbalimbali ikiwemo KOICA kutoka Korea ya Kusini.











Ijumaa, 24 Julai 2015

Ziara ya Viongozi wa Elimu kutoka Nigeria walipotembelea Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na Taasisi zake. Ziara hiyo ilianza Jumatatu, Julai 20, 2015.







Alhamisi, 2 Julai 2015


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI
 
TAARIFA KWA UMMA KUHUSU MATAPELI WANAOOMBA RUSHWA KWA KUJITAMBULISHA KAMA VIONGOZI WA ELIMU
Kumejitokeza kundi la watu ambao ni matapeli wanaoomba rushwa kwa kujitambulisha kama viongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na kutumia namba za simu zilizoandikishwa kwa kutumia majina ya viongozi hao. Namba hizo hutumika kwa muda na baada ya kufanikisha  lengo lao, watu hao huzifunga na hivyo kutokupatikana tena hewani.
Majina ya viongozi yanayotumika katika utapeli huo ni ya Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Katibu Mkuu, Kamishna wa Elimu na ya baadhi ya Wakurugenzi katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.
Namba hizo za simu hutumika na matapeli hao kwa kuwapigia watu wanaohitaji huduma katika ofisi za elimu na kuwaomba wawatumie  fedha kupitia namba hizo ili kufanikisha upatikanaji wa huduma wanazozihitaji kutoka katika ofisi hizo. Huduma zinazotajwa ni pamoja na kufanikisha usajili wa shule na vyuo.
 Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi inawatahadharisha wananchi kujiepusha na kundi hili la matapeli na ifahamike kuwa huduma zote zinazotolewa katika ofisi za elimu zikiwemo za usajili wa shule hazitolewi kwa rushwa au malipo ya aina yoyote.
Maelezo kamili kuhusu usajili wa shule yanapatikana katika ofisi za Ukaguzi wa Shule za Wilaya na Kanda na ofisi za Makao Makuu ya Wizara, au chumba namba 21 na 36 hapa wizarani. Tafadhali wasiliana na Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu au Kamishna wa Elimu endapo utapigiwa simu na  mtu  usiyemfahamu atakayejitambulisha kwako na kudai fedha ili afanikishe usajili wa shule au kupata huduma zingine wizarani. Usikubali kudanganywa na kutoa fedha kwa huduma inayopatikana bure.
Imetolewa na:
Katibu Mkuu,
WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI
02 Julai, 2015
 
 

Jumanne, 12 Mei 2015

Waziri Mkuu afungua Maadhimisho ya Wiki ya Elimu Kitaifa

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mizengo Peter Pinda amewataka wazazi na jamii kutambua umuhimu wa watoto kupata elimu na kuhakikisha watoto wote wenye umri wa kwenda shule wanaandikishwa na wanahudhuria bila kukosa hadi kuhitimu elimu ya msingi. Aidha almewataka walimu kufundisha ipasavyo ili elimu itolewayo iwe bora kwa maendeleo ya Taifa.

Waziri Mkuu alisema hayo wakati wa ufunguzi wa maadhimisho ya wiki ya elimu kitaifa yanayofanyika kwa mara ya pili nchini katika uwanja wa Jamhuri, Mjini Dodoma. Maadhimsho haya yaliyoanza tarehe Mei 11 yanakwenda sambamba na maonesho ya wadau mbalimbali wa Elimu na  yanatarajiwa kuhitimishwa siku ya Ijuma tarehe Mei 15 na Rais wa Jamhuri ya Muungano Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.

Aidha, katika ufunguzi huu Mhe. Waziri Mkuu ametoa tuzo kwa Shule, Mikoa na Halmashauri zenye ufaulu uliotukuka na zilizoongeza ufaulu kwa kiwango cha juu katika mitihani 2014 ikilinganisha na matokeo ya 2013. Sambamba na utoaji wa tuzo pia alitoa pikipiki kwa Waratibu Elimu Kata sita waliowakirisha Waratibu Elimu Kata wa nchi nzima