Ijumaa, 13 Oktoba 2017

Waziri: Ndalichako: Shule ya nyasi zitabaki kuwa historia

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako leo amekagua na kufungua ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule ya msingi kilole, Matondoro,  na Kilimani na kuweka jiwe la msingi bweni la wasichana katika shule ya Sekondari Semkiwa  Wilayani Korogwe Mkoani Tanga.

Akizungumza Mara baada ya kukagua utekelezaji wa miradi hiyo Waziri Ndalichako amesema  suala la nchi kuwa na shule au vyumba vya madarasa vya nyasi litabaki kuwa historia kwa kuwa serikali ya awamu ya Tano inahitaji wanafunzi wapate Elimu bora inayoenda sambamba na uboreshaji wa miundombinu na hicho ndicho kinachofanyika hivi sasa.

Akizindua bweni moja la wasichana katika shule ya Sekondari Semkiwa waziri Ndalichako ameahidi kutoa kiasi cha shilingi milioni kumi kwa ajili ya kununulia vitanda na magodoro ili bweni hilo lianze  kutumika mara moja.

Pia amewataka watanzania kwa ujumla kuendelea kumuunga mkono Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli kwa namna anavyojitoa  katika kuwatumikia Wananchi wanyonge kwa lengo la kuliletea Taifa Maendeleo.

Ujenzi wa vyumba hivyo vya madarasa,na  vyoo umetekelezwa  na Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia kupitia mradi wa Lipa kulingana na matokeo, (EP4R).




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni