Alhamisi, 6 Septemba 2018

ALIYOYASEMA WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA PROF. JOYCE NDALICHAKO LEO WAKATI WA MAHOJIANO NA TBC TAIFA KUHUSU MUSWADA WA SHERIA YA BODI YA KITAALAMU YA WALIMU


- Lengo la Bodi ni kuwa na Muundo na Chombo Cha Kisheria ili kutambua rasmi taaluma ya Ualimu kama zilivyo taaluma nyingine

- Ili kutimiza malengo yaliyowekwa na Serikali katika Elimu, thamani ya walimu ni jambo ambalo linapewa kipaumbele sana.

-Muswada wa Sheria ya bodi ya kitaalamu ya walimu umekuwa shirikishi katika hatua zote ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha Walimu,Maafisa Elimu wa Wilaya, Mikoa,Wathibiti Ubora,Chama Cha Walimu Tanzania,Taasisi mbalimbali na Wizara ikiwemo ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI).

- Wadau wengine walioshirikishwa Kuanzia hatua za awali ni pamoja na Haki Elimu, CHAKAMWAKA, TAPIE, TAMONGSCO na Mtandao wa Elimu Tanzania(TEN/MET)

- Malengo ya Bodi hii ya walimu hayafanani na chombo kingine, vyama vingine vinaangalia maslahi ya walimu wakati bodi inaenda kuleta hadhi kwa kutambua walimu wote waliopo na wasiokuwepo madarasani.

-Tume ya Utumishi wa walimu imejikita katika utumishi kwa maana ya kuangalia orodha ya walimu walioajiriwa na serikali na uratibu wa masomo wakati bodi itaangalia mabadiliko mbalimbali katika dunia ikiwa ni pamoja na kuangalia nafasi za kuwaendeleza walimu.

-Bodi pia itasimamia vigezo kwa kuhakikisha mwalimu lazima awe amehitimu katika Chuo kinachotoa mafunzo, pia bodi itasimamia suala la maadili kwa walimu.

-Bodi ya kitaalamu ya walimu itakuwa na jukumu la kupokea malalamiko, kuchambua na kuyapatia ufumbuzi malalamiko ya Walimu wachache ambao wamekuwa wakifanya matendo ambayo ni kinyume na maadili ya Ualimu.

-Bodi itatoa fursa kwa walimu kujadili kwa kina masuala yao ya kitaalamu kwa lengo la kuyapatia ufumbuzi.

-Waziri Ndalichako pia amelaani vikali vitendo vinavyofanywa na baadhi ya walimu vya kutoa adhabu kwa wanafunzi na ameonya walimu kuacha kumalizia hasira zao kwa wanafunzi.

-Waziri amesema uchapaji  hovyo  wa viboko kwa wanafunzi ni kinyume na taratibu za Wizara, sasa kuwepo kwa Bodi ya kitaalamu itahakikisha inawabana walimu watakaokwenda kinyume na taratibu.

- Waziri amewataka walimu kuacha mara moja tabia za kuchapa wanafunzi hovyo na badala yake wawapende watoto na wahakikishe wanawasidia katika kuwakuza kwenye maadili na malezi yanayokubalika kwenye Taifa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni