Jumatano, 17 Oktoba 2018

BARAZA LA TAIFA LA ELIMU YA UFUNDI (NACTE) LATAKIWA KUHUISHA MITAALA ILI IENDANE NA SOKO LA AJIRA


Serikali imelitaka Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) kuhakikisha Vyuo inavyovisimamia vinahuisha mitaala yake kila baada ya miaka mitatu kwa mujibu wa sheria ili kile kinachofundishwa kiweze kuendana na mahitaji halisi ya soko kwa sasa ikiwa ni pamoja na mabadiliko ya sayansi na Teknolojia.

Kauli hiyo ya Serikali imetolewa  na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha jijini Dar Es Salaam alipofanya ziara katika Taasisi hiyo ikiwa ni utaratibu aliojiwekea wa kutembelea Taasisi zilizo chini ya Wizara na kuona namna wanavyotekeleza majukumu yao.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akizungumza na watumishi wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi NACTE (hawapo pichani) alipofanya ziara katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam kuona namna wanavyotekeleza majukumu yao.

Ole Nasha alisema ufundi ni taaluma ambayo inabadilika kila siku hivyo ni vyema mitaala ikahuishwa ili kozi zinazotolewa ziendana na ushindani wa soko la ajira. 

Pia Naibu Waziri Ole Nasha amelitaka Baraza hilo kuendelea kufanya ukaguzi wa vyuo vyake na kuvifutia usajili vyuo vyote ambavyo havifuati sheria, kanuni na taratibu ikiwa ni pamoja na kuvichukulia hatua vinavyoendelea kufanya makosa kwa mujibu wa sheria.

“Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) tangu mwaka 2016 imefungia vyuo 74 ambavyo havifuati taratibu wakati mwaka huu vyuo 3 vimefungiwa huku vingine 21 vikizuiliwa kutoa baadhi ya kozi hii ni kutokana na dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Tano iliyo nayo ya kuhakikisha Elimu itolewayo ni bora na sio bora Elimu” aliongeza Naibu Waziri Ole Nasha.
Watumishi wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha alipofanya ziara katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es salaam

Katika hatua nyingine ameipongeza NACTE kwa kusimamia vizuri udahili wa wanafunzi kwa mwaka huu ikiwa ni pamoja na kutengeneza mifumo 14 ya TEHAMA ambayo imesaidia zoezi la udahili kufanyika kwa ufanisi hatua iliyopelekea kuongeza idadi ya wanafunzi elfu kumi zaidi kutoka ile ya mwaka jana ambayo walidahili wanafunzi 110,000.

Amesema Serikali ya Awamu ya Tano ni Serikali ambayo imejipambanua katika kufikia uchumi wa kati na wa Viwanda ambao ili uweze kufanikiwa uanahitaji mafundi waliosoma vizuri, hivyo elimu ya ufundi ni moja ya vipaumbele vya Serikali na kuzitaka Mamlaka hizo kusimamia elimu itolewayo ili tolewe kama inavyostahili.

Naibu Waziri amehitimisha ziara yake ya siku moja jijini Dar es Salaam kwa kutembelea Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi stadi VETA ambapo amewataka kuandaa vijana ambao ni mahiri na wabobezi katika fani mbalimbali watakaofanya kazi katika viwanda ili kujenga uchumi wa viwanda.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiwa katika picha ya pamoja na viongozi pamoja na watumishi wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Makao makuu jijini Dar es Salaam.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni