Jumanne, 30 Oktoba 2018

PROF NDALICHAKO: TATUENI CHANGAMOTO ZENU KIMIFUMO


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amewashauri watumishi wa Bodi ya Mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kuhakikisha kuwa wanatatua changamoto za mikopo ya Wanafunzi kwa njia ya mifumo.
Waziri Ndalichako amesema hayo jijini Dar Es Salaam alipotembelea ofisi ya HESLB lengo la kujiridhisha na hali ya mwenendo wa utoaji mikopo kwa Wanafunzi wa mwaka wa kwanza na wale wanaoendelea na masomo kwa mwaka 2018/2019.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako (mwenye koti la samawati) akiongea na wateja waliofika Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) jijini Dar es Salaam kurejesha madeni yao ya mikopo ya Elimu ya juu.
Katika ziara hiyo licha ya kukutana na Menejimenti ya HESLB, Prof. Ndalichako pia aliongea na Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU) Profesa Charles Kihampa kuhusu hali ya udahili wa Wanafunzi wa Elimu ya juu ambapo Kihampa alitumia nafasi hiyo pia kukabidhi orodha ya Wanafunzi 2,600 ambao udahili wao umethibitishwa.
Awali katika taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) Abdul-Razaq Badru ilisema kiasi cha shilingi bilioni 98.12 mpaka sasa kimetolewa kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu wapatao 27,929 kati ya wanafunzi 40,485 wa mwaka wa kwanza waliotarajiwa kupatiwa mikopo kwa mwaka wa masomo 2018/2019.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako (Katikati) akitambulishwa kwa Maafisa Mikopo wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi hiyo Abdul-Razaq Badru.
Badru alisema kuwa idadi ya wanafunzi waliobaki wapatao 12,556 watapangiwa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 42 katika awamu inayofuata ili kukamilisha idadi iliyokusudiwa.

Aliongeza kuwa idadi ya wanafunzi 27,929 waliokwishapangiwa mikopo na ambao wamedahiliwa katika vyuo mbalimbali vya elimu ya juu vinavyotambulika ni asilimia 69 ya wanafunzi 40,485 wanaotarajiwa kunufaika na mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2018/2019.

Orodha ya majina ya wanafunzi hao  27,929 (Awamu ya kwanza 25,532 na awamu ya pili 2,397) waliokwishapangiwa mikopo inapatikana kwenye tovuti ya HESLB www.heslb.go.tz  na itatumwa kwenye vyuo husika kwa ajili ya hatua zaidi za kukamilisha malipo ya mikopo hiyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni