Jumanne, 30 Oktoba 2018

WABUNGE WAIPONGEZA WIZARA YA ELIMU KUSIMAMIA VIZURI PROGRAMU YA LIPA KULINGANA NA MATOKEO


Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo leo amewasilisha taarifa ya tathmini ya Ubora wa elimu kutokana na Utekelezaji wa Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R) kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.


Akiwasilisha tathmini ya programu ya EP4R kwenye Kamati hiyo ya Bunge Dkt. Akwilapo ameeleza kuwa programu imekuwa na mafanikio tangu ilipoanza kutekelezwa mwaka 2014.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akiwasilisha taarifa ya tathmini ya ubora wa Elimu kutokana na utekelezaji wa Programu ya Lipa Kulingana na Matokeo wakati wa kikao na Kamati ya kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii jijini Doodma.

Dkt. Akwilapo amesema fedha zinazopatikana kutokana na utekelezaji wa vigezo (DLRs) katika ngazi ya Serikali kuu na serikali za Mitaa ni kuwa fedha hizo hutumika katika kuboresha utoaji wa elimu nchini kwa kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya elimu ikiwemo ukarabati na ujenzi wa miundombinu mipya.

Dkt. Akwilapo ameieleza kamati hiyo ya Bunge kuwa programu ya EP4R ni ya miaka minne na inatekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania, Serikali ya Sweden (SIDA) na Serikali ya Uingereza (DFID) na kuwa mradi huo utakamilika 2020.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati hiyo ya Bunge Peter Serukamba na Mbunge wa Nzega Mhe. Hussein Bashe wameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kusimamia vizuri utekelezaji wa mradi huo wa EP4R ambao umekuwa na matokeo chanya katika nchi.

“Katika kusimamia Programu hii ya EP4R, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imefanya kazi nzuri na matokeo yanaonekana. Miundombinu imeboreka sana,” alisema Mhe. Hussein Bashe.

Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii wakifuatilia Taarifa ya Utekelezaji wa Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R) Jijini Dodoma


Taarifa zinazowasilishwa kwenye kamati hiyo ni pamoja na ile ya mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo, taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mkwawa na utekelezaji wa shughuli za Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere kilichopo Kigamboni, jijini Dar es salaam.

Kikao hicho cha siku tatu kimeanza leo na kitakamilika Novemba 1, mwaka huu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni