Ijumaa, 26 Oktoba 2018

SERIKALI YAAHIDI KUTOA MILIONI 700 KUBORESHA SHULE ALIYOSOMA BABA WA TAIFA MWALIMU NYERERE


Serikali imeahidi kutoa kiasi cha Shilingi Milioni 700 kwa ajili ya kujenga na kukarabati Miundombinu mbalimbali katika shule ya msingi Mwisenge aliyosoma Baba wa Taifa Mwalimu Jullius K. Nyerere iliyopo manispaa ya Musoma mkoani Mara.

Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako mara baada ya kutii maelekezo yaliyotolewa na Rais John Magufuli ya kuitembelea shule hiyo na kufanya tathmini kwa lengo la kuikarabati ili iendane na hadhi ya Baba wa Taifa.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Mara Adam Malima wakiwa wamekaa kwenye dawati alilokuwa anatumia Baba wa Taifa Mwalimu Jullius Nyerere wakati akisoma katika shule ya Msingi Mwisenge iliyopo manispaa ya Musoma, Mkoani Mara.


Waziri Ndalichako amesema, kipaumbele cha Serikali ya awamu ya Tano ni Elimu, hivyo amemwelekeza Mkuu wa mkoa huo Adam Malima kuhakikisha kuwa fedha ambazo zitaelekezwa katika shule hiyo basi zisimamiwe ili zifanye kazi iliyokusiduwa na si kutumika vinginevyo.

“Rais John Magufuli akiwa katika ziara zake alifika na kuona kuwa shule hii inahitaji kuboreshwa hivyo alinielekeza nifike na kufanya tathmini kwa lengo la kuboresha Miundombinu ya Shule hii, sasa Mkuu wa mkoa mimi na wewe tuhakikishe uboreshaji unafanyika tena kwa kiwango kitakachoendana na hadhi ya Baba wa Taifa letu,” alisisitiza Waziri Ndalichako.

Waziri wa Elimu  na Mkuu wa mkoa wa Mara wakiwa nje ya bweni alilokuwa analala Baba wa Taifa Mwalimu Jullius K. Nyerere katika shule ya msingi aliyokuwa anasoma ya Mwisenge iliyopo manispaa ya Musoma.


Waziri Ndalichako amesema fedha hizo zitatumika kujenga mabweni mawili mapya, vyumba vitano vya madarasa, kukarabati Nyumba za walimu na kuboresha Miundombinu ya maji.

Kwa upande wake Mkuu wa mkoa huo Adam Malima ameahidi kusimamia fedha zitakazotolewa kwa ajili ya kuboresha Miundombinu katika shule hiyo na kuwa shule hiyo itakuwa mfano na pia kumbukumbu nzuri kwa Taifa.

Waziri Ndalichako pamoja na viongozi mbalimbali wa mkoa huo pia wametembelea Shule ya sekondari ya Ufundi Musoma, Shule ya sekondari Mara na Chuo Kikuu Cha kilimo na Teknolojia cha Mwalimu Nyerere kilichopo Wilayani Butiama kwa lengo la kukagua hali ya Miundombinu katika Taasisi hizo.
Darasa ambalo Baba wa Taifa Mwalimu Jullius K. Nyerere alilitumia kwa ajili ya kusoma kuanzia mwaka 1934 - 1936, shule hiyo ipo kwenye manispaa ya Musoma mkoani Mara.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni