Jumanne, 26 Machi 2019

HALMASHAURI ZATAKIWA KUWEKA MIKAKATI YA KUMOTISHA WALIMU

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa amezitaka Halmashauri zote nchini kuhakikisha zinaweka mikakati ya kuwamotisha walimu wapya wanaoripoti kazini kwa kuwafikisha katika vituo vyao vya kazi ikiwa ni pamoja na kuwalipa maslahi yao yote.

Waziri Mkuu ameyasema hayo jijini Dodoma wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa sita wa Umoja wa Maafisa Elimu Mikoa na Wilaya (REDEOA) na kusisitiza kuwa hatua hiyo iende sambamba na kuendelea kuwatembelea walimu hao katika vituo vyao vya kazi kuwasikiliza, kushauriana na kupatia ufumbuzi changamoto walizo nazo.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akifungua Mkutano Mkuu wa  sita wa Maafisa Elimu Mikoa na Wilaya (hawapo pichani) Jijini Dodoma.
Amesema walimu hao wanaporipoti wanakuwa ni wageni katika wilaya hizo hivyo kuwaelekeza tu kuripoti katika shule walizopangwa haitoshi ni vyema kuweka utaratibu wa kutumia magari ya Halmashauri kuwafikisha walimu hao katika vituo vyao vipya vya kazi.

“Ninyi Maafisa Elimu hakikisheni walimu hao wanaporipoti wanalipwa maslahi yao ya msingi, lakini pia hamasisheni Halmashauri zenu kuwamotisha walimu kwa kuwapa vianzilishi vya maisha kama ambavyo Wilaya nyingine zinafanya. Wilaya za Mkoa wa Njombe tangu mwaka 2013 zimekuwa zikitoa motisha kwa walimu wapya wanaoripoti kwa kuwapa kitanda, godoro, gunia la mahindi, viazi na maharage, hii inamfanya mwalimu kujisikia yuko nyumbani, muige mfano huu,” aliongeza Waziri Mkuu Majaliwa.
Baadhi ya Maafisa Elimu wa Mikoa na Wilaya wakifuatilia Hotuba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa sita wa Umoja wa Maafisa Elimu hao uliofanyika jijini Dodoma.
Katika hatua nyingine Mhe. Majaliwa amewataka Maafisa Elimu hao kutumia mkutano huo kukumbushana wajibu wao katika kusimamia Elimu na kubadilishana uzoefu na mbinu mbalimbali za kusimamia elimu ili kuongeza ubora wa elimu hiyo.

“Mkutano huu umekuja kipindi muafaka kwa sababu matokeo ya upimaji wa Taifa wa ngazi mbalimbali yameshatoka, wote tunakumbuka upimaji umefanyika kwa mitihani ya darasa la nne, la saba, kidato cha nne na ile ya kidato cha sita, hii itoe fursa kwenu kujipima na kuona kama hatua mliyofikia ni nzuri na kama bado ni ya chini basi mbainishe changamoto zilizopelekea kuwa hivyo na kuweka mipango ya kuboresha,” alisema Mhe. Majaliwa.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akimkabidhi tuzo Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako kwa kusimamia vizuri Sekta ya Elimu. Tuzo hiyo imetolewa na Umoja wa Maafisa Elimu Mikoa na Wilaya (REDEOA) kwa kutambua mchango wa Waziri huyo katika kusimamia ubora wa Elimu nchini.
Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amewataka Maafisa Elimu kusimamia Sera, Miongozo na Taratibu zinazosimamia utoaji wa elimu nchini huku akiwasihi maafisa hao kutoa taarifa zilizo sahihi kwani wakati mwingine taarifa zinazotolewa zinatofautiana na zile zinawasilishwa baada ya kufanyika kwa ukaguzi katika maeneo mnayoyasimamia.
   
“Wakati mwingine mnatoa taarifa zisizo sahihi, kwa sababu kaguzi ambazo  zimekuwa zikifanyika zinaonesha kuna baadhi ya maeneo ambayo bado kuna mrundikano mkubwa wa wanafunzi kati ya 73 hadi 200 kwa upande wa sekondari na mazingira yanapokuwa katika hali hiyo si rahisi kutoa elimu bora, hivyo tutoe taarifa zilizo sahihi na taarifa hizi zikiwa sahihi itasaidia hata wakati wa uchaguzi wa wanafunzi wanaojiunga na kidato cha kwanza na kile cha tano,” aliongeza Waziri Ndalichako.

Nae Mwenyekiti wa Umoja wa Maafisa Elimu Mikoa na Wilaya Germana Mng’ao ameipongeza Serikali kwa kuboresha mazingira ya kufundishia  na kujifunzia na kuahidi kufanya kazi kwa bidii katika nafasi yao ya kusimamia Elimu Tanzania.


Kauli mbiu ya mkutano huo ni “ELIMU BORA ITATUFIKISHA KATIKA UCHUMI WA KATI IFIKAPO 2025.”
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akisalimiana na   Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa sita wa Umoja wa Maafisa Elimu hao uliofanyika jijini Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni