Jumatatu, 25 Machi 2019

OLE NASHA: SERA YA KUWALINDA WABUNIFU YAJA


SERIKALI imesema iko katika hatua za mwisho kukamilisha Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ambayo itatoa mwongozo wa namna ya utekelezaji wa masuala ya ubunifu na kuwatambua wabunifu kwa ajili ya maendeleo ya nchi.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. William Ole Nasha jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa Wiki ya Ubunifu iliyoandaliwa na Mfuko wa Ubunifu kwa Maendeleo ya Watu (HDIF) kwa kushirikiana na Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH).

 
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mh. William Ole Nasha akizungumza na wabunifu (hawapo pichani) katika ufunguzi wa maonesho ya Wiki ya Ubunifu yanayofanyika jijini Dar es Salaam.
Ole Nasha amesema, serikali ya Awamu ya Tano imeweka kipaumbele katika teknolojia ili kuongeza chachu ya maendeleo na ipo tayari kufadhili bunifu mbalimbali zitakazochangia maendeleo ya uchumi wa Viwanda ifikapo 2025.

Naibu Waziri Ole Nasha amewataka waandaji wa maonesho hayo kuyapeleka katika maeneo ya wazi na rahisi kufikika ili wananchi wengi wapate fursa ya kujionea bunifu hizo.

"Wabunifu wengi ni wale wanaokumbana na changamoto za kila siku na kujaribu kuangalia namna ya kuzitatua hivyo wakati mwingine mtakapoandaa wiki ya ubunifu muhakikishe kwamba mnaweka katika maeneo ya wazi kwa ajili ya kuwakutanisha wabunifu wengi na wananchi ili waweze kujua kinachofanyika," ameeleza.

Baadhi ya wabunifu wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mh. William Ole Nasha (hayupo pichani) wakati wa ufunguzi wa maonesho ya Wiki ya Ubunifu yanayofanyika jijini Dar es Salaam.
Aidha Ole Nasha amewaasa wabunifu kufanya bunifu zitakazoendana na changamoto za maisha zilizopo nchini na siyo kufanya bunifu za kujifurahisha sababu wanaweza kukosa soko.

Naye, Kiongozi Mkuu wa Mfuko (HDIF), David McGinty amesema wadau wa maendeleo nchini, wamekuwa wakichangia Tanzania kupanda viwango vya kimataifa vya ubunifu kwani mpaka wanafunzi wa vyuo na sekondari wanahamasishwa kutumia teknolojia kwa ajili ya kujifunzia.

Wiki ya Ubunifu inatekelezwa na Mfuko wa Ubunifu kwa Maendeleo ya Watu (HDIF) kwa kushirikiana na Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) pamoja na wadau wengine.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mh. William Ole Nasha na Naibu Katibu Mkuu Prof. James Mdoe wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wadau wa ubunifu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni