Alhamisi, 11 Aprili 2019

ZAIDI YA SHILINGI MILIONI 700 KUKARABATI KARAKANA SUA


Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeahidi kutumia kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 700 kufanya ukarabati mkubwa wa karakana mbalimbali hasa zile za ndaki ya kilimo katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kilichopo mkoani Morogoro.

Ahadi hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Leonard Akwilapo wakati wa ufunguzi wa wiki ya Kumbukizi ya kifo cha Hayati Edward Moringe Sokoine iliyofanyika SUA Mkoani Morogoro ambapo amesema lengo la kuzifanyia ukarabati karakana  hizo ni kuziboresha ili ziendane na mwenye jina na kuboresha utendaji kazi.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akitembela shamba darasa la mazao ya papai na nanasi katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Mkoani Morogoro.

Dkt. Akwilapo alisisitiza kuwa Hayati Edward Moringe Sokoine katika utumishi wake kama Waziri Mkuu wa Tanzania aliongoza nchi kwa moyo wa uwajibikaji, kufuata sheria huku akitanguliza uzalendo mbele kwa ajili ya nchi yake hivyo ni vizuri kutafakari mawazo ya Hayati Sokoine ambayo yalichangia katika kujenga msingi kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi na kuyaenzi kwa vitendo.

“Leo imetimu miaka 35 tangu tulipompoteza mtoto wa kweli wa ardhi yetu, katika maadhimisho ya kifo chake tutafakari mawazo yake ambayo yalichangia kujenga msingi kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi nchini,” alisema Dkt. Akwilapo.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akiangalia samani zilizotengenezwa kwa kutumia miti ya mianzi wakati akitembelea mabanda ya maonesho katika viwanja vya SUA Mkoani Morogoro

Miongoni mwa mambo ambayo Hayati Edward Moringe Sokoine ambaye Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kimepewa jina lake aliyapa msisitizo katika kuliletea Taifa maendeleo ni pamoja na uzalishaji na maendeleo ya viwanda katika kilimo.

Nae Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo, Prof. Raphael Chibunda amesema maonesho ya wanasayansi na wabunifu ni sehemu ya kumuenzi Hayati Moringe Sokoine kwa kuendeleza mambo mazuri aliyoyafanya kwa maendeleo ya Tanzania na kufanya maono yake kuwa hai kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo akiangalia shamba kisasa la samaki na mbogamboga alipotembelea mabanda ya maonesho SUA wakati wa maadhimisho ya wiki ya Hayati Edward Moringe Sokoine.

Profesa Chibunda aliongeza kuwa kumbukizi hiyo kwa mwaka huu imechagizwa na maonesho hayo yanayolenga kukuza uzalishaji katika kilimo na viwanda nchini kama ilivyoainishwa katika Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Kilimo awamu ya II (2015/16-2024/25) na Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano awamu ya II, (2016/17-2020/21).

Kumbukizi ya Hayati Edward Moringe Sokoine ya mwaka huu imechagizwa na mada juu ya Uzalishaji wa Viwanda kwa Maendeleo ya Tanzania: Mambo ya kujifunza kutoka kwa  Hayati Edward Moringe Sokoine na Matarajio ya siku zijazo.
 
Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kimekuwa kikiandaa kumbukizi ya kifo chake tangu mwaka 1992 ikihusisha uwasilishaji wa mihadhara ambayo imekuwa ikiakisi mambo ya kiongozi huyo.

Moja ya shamba darasa la papai lililopo katika Chuo Kikuu cha Kilimo (SUA) Mkoani Morogoro


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni