Ijumaa, 19 Julai 2019

TCU KUHAKIKISHA MITAALA KATIKA VYUO VIKUU INAANDAA WAHITIMU WANAOENDANA NA MATAKWA YA TAIFA

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassimu Majaliwa (Mb) ameitaka Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) nchini kuhakikisha mitaala inayotumika katika vyuo vikuu iweze kuandaa wahitimu siyo tu kwa kuajiriwa, bali pia kuwa na uwezo wa kujiajiri na kutengeneza ajira kwa wengine.

Waziri Mkuu Majaliwa ametoa agizo hilo jijini Dar es Salaam wakati wa ufunguzi wa maonesho ya 14 ya elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia nchini ambapo amesema uwepo wa mitaala ya aina hiyo utasaidia kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu kwa ujumla.

“Nimeelezwa kuwa tayari baadhi ya Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu zimeshaanza kuchukua hatua za kutengeneza Mitaala mipya na kuhuisha ile ya zamani ili kuifanya iendane na mahitaji ya sasa ya taifa na soko la ajira, nitoe wito kwa Taasisi zote za Elimu ya Juu kuendelea kuhuisha na kuboresha mitaala yao kwa mwelekeo huo,” alisema Mhe Majaliwa.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akisalimiana na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa (MB) wakati alipowasili viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam ili kufungua maoesho ya 14 ya Elimu ya Juu Tanzania. 
Akizungumzia azma ya serikali ya kuongeza udahili katika Vyuo Vikuu, Waziri Mkuu ameitaka Tume ya Vikuu kutafuta mbinu za kuviwezesha vyuo zaidi ikiwa ni pamoja na kujengea uwezo vyuo vikuu binafsi ili visaidie katika kuongeza udahili pamoja na kufikia viwango vinavyotakiwa na siyo kuwapunguzia viwango vya matakwa ya usajili.

“Msimamo wa Serikali uko wazi na unataka Vyuo Vikuu Binafsi kuwa washirika muhimu kwenye maendeleo ya Sekta ya Elimu ya Juu nchini, hata hivyo nai vema nikaeleweka vizuri hakuna mbadala wa elimu bora, ni wajibu wetu  kuhahakikisha vyuo vyote vinatoa elimu bora. TCU endeleeni kutekeleza majukumu yenu  ya kimsingi ya kudhibiti na kushauri lakini zaidi jipambanue  katika uwezeshaji wa vyuo hivyo ili kuondoa taswira hasi iliyojengeka katika jamii kuwa kazi ya Tume  ni kuvifungia vyuo vikuu badala ya kutatua changamoto zinazowakabili.” Alisema Mhe. Majaliwa.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa (MB) akipata maelezo ya kazi zinazotekelezwa na Tume na Vyuo Vikuu nchini (TCU) kutoka kwa Katibu Mtendaji wa Tume hiyo Profesa Charles Kihampa. Taasisi hiyo ndio mratibu wa maoesho ya Taasisi ya Elimu ya Juu yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja  jijini Dar es Salaam.
Alisema ili kuongeza idadi ya watanzania wanaopata nafasi ya Elimu ya Juu, ni lazima kama nchi kupanga mikakati kwa kushirikiana na sekta binafsi, ambao ni wadau wakubwa sana katika Elimu ya Juu kwani ukiangalia kati ya wahitimu wote wa Vyuo vikuu kwa mwaka, asilimia 25 wanatoka katika vyuo vikuu binafsi.

Katika hatua nyingine Mhe. Majaliwa ameitaka TCU kuhakikisha wanakutana na taasisi binafsi zinaowasaidia watanzania kupata nafasi katika vyuo vikuu nje ya nchi ili ziweze kuwatambua, kuwasajili lakini pia kufanya nao kazi kwa karibu ili kuwaambia mahitaji halisi ya kwenda vyuo vikuu ni yapi na wao washiriki katika kumshauri kijana ni alama zipi za ufaulu zinafaa kwenda kwenye digrii, diploma na ama cheti ili kuepukana na changamoto ya kutotambulika kwa vyeti pindi wanapohitimu katika ngazi hizo za elimu akitolea mfano watanzania ambao wamesoma kwenye moja ya Chuo Kikuu kilichopo nchini Misri lakini vyeti vyao kutotambulika.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa (MB) akizungumza wakati wa ufunguzi wa maoesho ya 14 ya Elimu ya Juu Tanzania yaliyofanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam. 
 “Naona kundi kubwa la vijana wa kidato cha sita wanatafuta vyuo kupitia taasisi hizo ni vyema sasa TCU kwa kuwa mko katika maonesho hayo mshirikiane kuwasaidia vijana wetu hawa kupata vyuo vinavyostahiki ili wakienda kusoma akipata cheti na kurejea muweze kuvitambua vyeti hivyo,” alisema Mhe. Majaliwa

Awali Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William ole Nasha alimweleza Waziri Mkuu kuwa ili kuongeza idadi ya wahitimu watakaochochea ukuaji uchumi kwa kupitia sekta zinazochangia kwa kiasi kikubwa kukua kwa uchumi tayari baadhi ya vyuo vimefanya maboresho ya mitaala kutoka kwenye mfumo unaozingatia ufahamu na kwenda kwenye mfumo wa umahiri.

Pia Wizara kwa kushirikiana na Taasisi za sekta binafsi Tanzania imeanzisha mabaraza 6 ya kisekta ya ujuzi na maarifa katika Sekta za Kilimo, Ujenzi, Uchukuzi, Utalii, Nishati na TEHAMA kwa lengo la kushauri kuhusu mitaala na mahitaji halisi ya soko la ajira.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanafunzi waliotembelea banda la Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wakati wa maoesho ya 14 ya Elimu ya Juu Tanzania yanayofanyika Jijini Dar es Salaam.
Nae Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini Charles Kihampa amesema Maonesho ya Vyuo Vikuu kwa mwaka huu yamehudhuriwa na taasisi 81 ambapo taasisi 66 ni za ndani ya nchi na 15 ni taasisi za kutoka nje ya nchi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa maonesho ya 14 ya elimu ya Juu Mwenyeketi wa Kamati ya Wakuu wa Vyuo vikuu vya Umma nchini Prof. Raphael Chibunda ameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Serikali kwa Ujumla kwa kuhakikisha kuwa Mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu inaongezeka jambo ambalo limepunguza migogoro katika Vyuo.

Maonesho ya 14 ya Elimu ya Juu yana kauli mbiu isemayo Jukumu la Taasisi za Elimu ya Juu katika kuzalisha Ujuzi unaohitajika kwa ajili ya Viwanda.
Mmoja wa watumishi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia akitoa ufafanuzi kwa wadau waliotembelea banda la Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia katika maonesho ya 14 ya Elimu ya Juu Tanzania yanayofanyika jijini Dar es Salaam.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni