Ijumaa, 20 Septemba 2019

WIZARA YA ELIMU KUWAKUTANISHA WADAU WA ELIMU ILI KUJADILI MASUALA YA ELIMU NCHINI


Waziri wa Eimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amefungua na kushiriki Mdahalo juu sekta ya Elimu uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Mjadala huo ulioandaliwa na Mwanachi Communications Ltd., (MCL) kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ulihusisha majadiliano juu ya uwezeshaji vijana katika kukuza maarifa na ujuzi mahususi.

Akifungua mdahalo huo Waziri Ndalichako amesema Serikali ya awamu ya Tano imewekeza kiasi kikubwa cha rasilimali ili kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji katika ngazi zote za elimu ili vijana wanaosoma wapate mafunzo katika mazingira yatakayowawezesha kuwa mahiri katika fani wanazosomea.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza wakati wa ufunguzi wa mjadala juu ya uwezeshaji vijana katika kukuza maarifa ulioandaliwa na Mwananchi Communications Ltd., kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia jijini Dar es Salaam.
Prof. Ndalichako ameongeza kuwa katika ngazi ya elimu ya ufundi na elimu ya juu serikali inaboresha maabara na karakana na kuweka vifaa vya kisasa ili mafunzo kwa vitendo yafanyike kwa tija na kulingana na mazingira ya sasa. Aidha ametolea mfano wa maktaba ya kisasa inayojengwa katika Chuo Kikuu cha Teknolojia Mbeya (MUST) itakayokuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 2,500 kwa mara moja ambayo inagharimu fedha za ndani zaidi ya shilingi bilioni 11.

Ndalichako amewashukuru MCL kwa kufungua njia ya kuwa na mijadala ya wazi juu ya maendeleo ya elimu na kuahidi kuandaa mjadala mwingine wa Elimu utakaohusisha wadau.  Pia amepongeza washiriki kwa kutoa maoni ambayo yana tija katika kuboresha elimu, huku akisisitiza kuwa elimu yetu inaandaa vijana mahiri ambao wanashiriki kujenga taifa.

"Humu ndani tumesikia fikra mahiri zinazotokana na vijana ambao wanasoma hapa hapa nchini na mitaala ni hii hii, hivyo tujiamini kuwa elimu yetu ni bora na inawezesha vijana kuwa mahiri katika fani mbalimbali," alisema Ndalichako.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako akiwa na baadhi ya wadau wa Elimu wakifuatilia mjadala juu ya uwezeshaji vijana katika kukuza maarifa uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Ndalichako amesisitiza juu ya uboreshaji elimu ya ufundi ambapo amesema katika mwaka huu wa fedha vyuo vipya vya VETA 25 vinajengwa kwa shilingi bilioni 40.

Ndalichako pia amesema Serikali kupitia VETA inaendelea na programu ya kutambua na kurasimisha ujuzi kwa vijana ambapo amesema mwaka huu zaidi ya vijana 10,000 watapatiwa mafunzo kutokana na ujuzi walio nao na kupatiwa vyeti vya kurasimisha ujuzi huo. Amesema lengo la kurasimisha ni kuwatambua, kuwapa stadi na kuwaongezea ujuzi vijana walioko katika maeneo mbalimbali ambao wamekuwa wakifanya kazi za ujuzi bila vyeti.

Awali, akizungumza katika mjadala huo Mkurugenzi Mtendaji wa MCL, Francis Nanai amemshukuru Waziri Ndalichako na Viongozi wa wizara kwa kukubali kushiriki mjadala na kupokea maoni.  Amesema wao kama sekta binafsi wanalo jukumu la kushirikiana na serikali katika kusukuma mbele maendeleo kulingana na eneo lao la biashara.

Akiongea katika Mjadala huo, Prof. Lughano Kusiluka ambaye ni Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mzumbe amesema Vyuo Vikuu vinaandaa mitaala kulingana na uhitaji wa soko na mahitaji ya wakati.  Amewaasa vijana pia kuona umuhimu wa kutumia elimu wanayopata na vipaji walivyo navyo kubuni biashara na kujiajiri badala ya kusubiri ajira.

Kusiluka amesema Vyuo vikuu vina programu za kukuza bunifu za wanafunzi na kuziendeleza kuwa biashara kupitia Vituo Atamizi na kambi za ujasiriamali.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akibadilishana mawazo na Mkurugenzi Mtendaji wa Mwananchi Communications Ltd., Francis Nanai wakati wa  mjadala juu ya uwezeshaji vijana katika kukuza maarifa uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Naye mmoja wa washiriki, Abel Nyengo ameiomba Serikali kuhakikisha kila kijana aliyeko katika chuo anapata nafasi ya mafunzo kwa vitendo.

"Nishauri serikali kuwa mafunzo kwa vitendo iwe ni lazima na ipewe umuhimu mkubwa katika kutahini wanafunzi badala ya kutegemea mitihani,” alisema Nyengo.

Wananchi na wadau mbalimbali wametoa maoni mengi juu ya mada hiyo wakihusisha mitaala, utoaji elimu na ujuzi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni