Ijumaa, 27 Septemba 2019

OLE NASHA: MSIWAGEUZE WATOTO WA KIKE MITAJI

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amewataka wazazi kuacha kuwageuza mitaji watoto wao wa kike kwa kuwaozesha mapema na badala yake wawasaidie katika kupata elimu ili baadaye wawe msaada  kwao na taifa kwa ujumla.

Ole Nasha ameyasema hayo leo alipofanya  ziara ya kikazi wilayani Itilima mkoani Simiyu ambapo amekagua  ujenzi wa mabweni mawili ya wasichana katika shule ya sekondari Nkoma yenye uwezo wa kuchukua watoto 160 kwa wakati moja.

"Niwaambie kitu wazazi, kama unataka kumfanya mwanao wa kike mtaji basi mtaji mkubwa ni kumpa elimu na sio kumuozesha," alisema Ole Nasha.
 
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akiongea na wazazi, walezi na wanafunzi wa shule ya sekondari Nkoma iliyopo wilaya ya Itilima mkoani Simiyu.
Baadhi ya wazazi na walezi wa wanafunzi wa shule ya Nkoma wakimsikiliza Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani) alipokuwa akiongea nao shuleni hapo.
Aidha Naibu Waziri Ole Nasha amewataka wazazi kuwekeza kwenye elimu ya watoto wao huku akisisitiza kuwa mtoto wa kike ana haki ya kupata elimu sawa na mtoto wa kiume, ambapo amesema katika jamii nyingi bado hawajawapa kipaumbele cha kupata elimu watoto wa kike.

"Kuna baadhi ya wazazi bado wanashawishi watoto wao kufanya vibaya katika mitihani yao ya mwisho ili wasiendelee na masomo. Nawaomba wazazi msishawishi watoto wa kike na kuwatilia vikwazo vya kukatisha masomo ili muwaozeshe. Mtoto wa kike ana nafasi ya kupata elimu sawa na mtoto wa kiume," alisema Naibu Waziri Ole Nasha.
Mwalimu Mkuu wa shule ya sekondari Nkoma, Sarah Matonya akisoma taarifa ya ujenzi wa mabweni mawili mapya mbele ya Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani).
Ole Nasha aliongeza kuwa serikali na wadau wa elimu wanatakiwa waendelee kutoa hamasa ya elimu kwa jamii, wanafunzi na wazazi ili miundombinu ya elimu inayojengwa iweze kutumika kwa faida ya wananchi wote katika kuboresha na kukuza elimu.

Naibu Waziri Ole Nasha amepongeza  usimamizi wa fedha za miradi ya elimu katika wilaya hiyo kutokana na kutokuwepo kwa malalamiko yoyote ya matumizi mabaya ya fedha hizo.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akizindua mabweni katika shule ya sekondari Nkoma ya wilayani Itilima mkoani Simiyu.
Awali, akisoma taarifa ya ujenzi wa mabweni hayo, Mwalimu Mkuu wa shule ya sekondari Nkoma, Sara Matonya alisema mabweni hayo yamegharimu zaidi ya shilingi milioni 300 na kwamba kukamilika kwa mradi huo wa ujenzi wa mabweni kumechochea hamasa ya wanafunzi wa kike kusoma kwa bidii kutokana na kuboreshwa kwa mazingira ya kujifunzia.


"Mabweni haya mawili yana uwezo wa kubeba wanafunzi 80 kila moja na yamesaidia wanafunzi kuondokana na adha ya kutembea umbali mrefu wa zaidi ya kilometa 10 kufika shuleni. Wanafunzi wa kike pia wameepukana na vishawishi na mimba zilizokuwa zikiwasababishia kukatisha masomo," alisema Mwalimu Matonya.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (katikati) akikagua moja ya mabweni mapya katika shule ya sekondari Nkoma iliyopo wilayani Itilima mkoani Simiyu.  Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Benson Kilangi na kulia ni Mbunge wa Itilima, Njalu Silanga.
Kwa upande wao wazazi na wanafunzi wameipongeza serikali kwa kutoa elimu bila malipo pamoja na kuwajengea mabweni, hali iliyopelekea kuongezeka kwa mahudhurio ya wanafunzi darasani, ufaulu na mwitikio wa elimu katika jamii.

"Tunaipongeza serikali kwa ujenzi wa mabweni haya ambayo yametupunguzia changamoto ya kutembea umbali mrefu na pia tumekuwa na muda mwingi wa kujifunza na kujisomea, na hivyo kutuwezesha kufanya vizuri katika masomo yetu," alisema Myano Ngusa, mwanafunzi wa shule ya sekondari Nkoma.
Mojawapo ya chumba katika bweni jipya la shule ya sekondari Nkoma ya wilayani Itilima mkoani Simiyu.
Katika ziara hiyo Ole Nasha pia alikagua ofisi ya Uthibiti Ubora wilaya ya Itilima ambazo ujenzi wake umekamilika pamoja na majengo ya VETA yanayoendelea kujengwa katika kijiji cha Kanadi wilayani humo.
Muonekano wa nje wa moja kati ya mabweni yaliyojengwa katika shule ya sekondari Nkoma ya Itilima mkoani Simiyu lenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 80 kwa wakati mmoja.
Muonekano wa nje wa jengo la ofisi za Uthibiti Ubora wilaya ya Itilima mkoani Simiyu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akikagua ofisi ya Uthibiti Ubora wilaya ya Itilima mkoani Simiyu.
Muonekano wa ndani wa chumba kimojawapo katika majengo ya VETA, Itilima mkoani Simiyu.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (mwenye skafu) akisikiliza maelezo kuhusu VETA kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Benson Kilangi.
Muonekano wa nje wa jengo la VETA la wilayani Itilima mkoani Simiyu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni