Ijumaa, 15 Novemba 2019

TANZANIA MWENYEJI MKUTANO WA KIMATAIFA WA *GIRL*GUIDES*


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi ambayo imejizatiti  na ina dhamira ya dhati ya kuhakikisha kwamba  inaondoa fikra potofu kuhusiana na masuala ya kijinsia.

Waziri Ndalichako ameyasema hayo jijni Dar e Salaam alipomuwakilisha Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan katika ufunguzi wa Semina ya Kimataifa ya kuwajengea uwezo vijana wa kike (Girl Guides) katika masuala ya Uongozi ijulikanayo kama Julitte Low Seminar.

Amesema lengo la semina ni kupanua na kuimarisha ushiriki wa wasichana katika masuala ya girl guides lakini pia kuwawezesha kushirikiana katika masula ya kiutamaduni na uongozi ikiwa ni pamoja na kuwatia moyo wasichana hao ili wazidi kufanya vizuri zaidi katika Jamii wanazotoka.

“Naamini baada ya semina hii ya siku saba wasichana watakuwa na uwezo kushiriki katika masuala ya uongozi na kukemea imani potofu ambazo zinakuwa zikionesha kuwa mwanamke ni kiumbe dhaifu na kutengeneza mtazamo chanya kuwa wanawake ni viumbe kama wanaume na wana uwezo mkubwa wa kuleta mabadiliko katika ulimwengu huu,”Alisema Prof Ndalichako.

Prof Ndalichako amesema Nchi ya Tanzania inatekeleza mipango inayozingatia usawa wa kijinsia na kuwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanawake na wanaume wana fursa sawa katika maendeleo.

“Mhe Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu asingeweza kupata nafasi aliyo nayo kama nchi ingekuwa bado ina dhana potofu , uwepo wake ktk nafasi ya Makamu wa Rais, viongozi na wataamu  wengine katika nyanja mbalimbali  inaonesha kuwa nchi yetu imepiga hatua katika kuweka usawa wa kijinsia ”aliongeza Prof ndalichako

Amewapongeza Waandaaji wa Semina hiyo kwa kuchagua Tanzania kuwa nchi mwenyeji na kwamba Tanzania ina historia ya kutoa wanawake ambao ni wa nguvu akiwataja viongozi hao kwa uchache  kuwa ni marehemu bibi Titi Mohamed ambaye amekuwa kiongozi wa nchi yetu wakati wa uongozi wa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Getrude Mongela ambaye alishiriki kwenye mkutano wa Beijing, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Asha-Rose Migiro, Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Anna makinda na  sasa Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Nae Mwenyekiti wa Chama cha Girl Guides Taifa Prof Martha Qorro amesema semina  ya mafunzo ya uongozi kwa vijana wa kike (Girl Guides) inafanyika ulimwengu mzima na itasaidia wasichana hao  kujitegemea, kujitambua, kujithamini, kupenda taifa lao kumpenda Mungu kuhesimu wengine na kusaidia mahali popote panapohitaji msaada.

Kwa upande wake mwakilishi wa Bodi ya Dunia katika "World Association of Girl Guide and Girl Scout" kwa kanda ya Afrika  Florentina Mganga amesema semina hii inaendelea ulimwenguni kote na vijana wa kike 700 watapata mafunzo juu wa uongozi  na itawawezesha kujua kuwa mtoto wa kike anaweza kuwa kiongozi wanachotakiwa ni kujiamini.

Semina ya Kimataifa ya kuwajengea uwezo vijana wa kike juu ya masula ya uongozi inashirikisha nchi 17 ambazo ni Marekani, Uingereza, Ujerumani  Swizaland, Ghana, Zimbawe, Malawi, Rwanda, Burundi, Kenya, Madagascar, Egypt, Germany,Uganda,  Sierra Leone, Poland, Hong Kong, Philippines na Tanzania ikiwa kama Mwenyeji wao.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako na Prof Martha Qorro ambae ni Mwenyekiti wa Chama cha Girl Guides Taifa wakifurahia ngoma kutoka kwa wanafunzi wa shule ya msingi Diomond (hawapo pichani)wakati wa ufunguzi wa semina ya kimataifa ya kuwajengea uwezo vijana wa kike juu ya masuala ya uongozi inayofanyika jijini Dar es Salaam
Girl Guides kutoka shule ya Msingi Oasis ya jijini Dar es Salaam wakiimba ngonjera mbele ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako wakati wa ufunguzi wa semina ya kimataifa ya kuwajengea uwezo vijana hao  iliyofanyika Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako akiwa kwenye picha ya pamoja na Girl Guides   wa shule ya msingi Oasisi ya jijini Dar es salaam mara baada ya kufungua semina ya kuwajengea uwezo vijana wa kike kwenye masuala ya uongozi inayofanyika jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya Makamishna na Volunteers wa Girl Guides Tanzania wakipita mbele ya mgeni rasmi (hayupo pichani)wakiwa wameshika bendera za nchi mbalimbali wakati wa ufunguzi wa semina ya kimataifa ya kuwajengea uwezo vijana wa kike juu ya uongozi iitwayo Juliette Low Seminar Jijini Dar es Salaam
Baadhi  ya Girl Guides kutoka nchi mbalimbali wanaoshiriki semina ya kimataifa ya kuwajengea uwezo watoto wa kike juu ya masuala ya uongozi ijulikanayo kama Juliette Low  inayofanyika jijini Dar es Salaam wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako wakati wa ufunguzi wa seminia hiyo


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni