Alhamisi, 12 Desemba 2019

OLE NASHA: WAKUU WA SHULE HIMIZENI WANAFUNZI WASHIRIKI MASHINDANO YA UANDISHI WA INSHA

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amewataka Wakuu wa Shule zote za sekondari nchini kuwahimiza wanafunzi wao kushiriki katika mashindano ya uandishi wa insha za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Ole Nasha amesema mashindano hayo ni sehemu ya mkakati wa kujenga uelewa kwa wanafunzi juu ya kazi na mipango ya maendeleo ya Jumuiya hizo.

Ole Nasha ameyasema hayo leo jijini Dodoma katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC kwa mwaka 2019 na kuongeza kuwa mashindano haya yana faida kubwa zaidi ya kupata zawadi kwani washindi wanaweza kuyatumia kujiongezea wasifu wao siku za mbeleni na hivyo kuwaongezea sifa za kupata ajira.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha akiongea na washiriki (hawapo pichani) waliohudhuria hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC, 2019 iliyofanyika jijini Dodoma.
"Niwaambie wanafunzi, kushinda sio suala la kupata zawadi tu bali kunakujengea wasifu ambao huko mbeleni utakusaidia unapoomba ajira unakuwa na wasifu wa ziada utakaokufanya upate ajira kirahisi," alisisitiza Ole Nasha.

Katika hatua nyingine Waziri Ole Nasha ameonesha  kushangazwa na wanaobeza kiwango cha elimu itolewayo nchini ambapo amesema ushindi unaopatikana kutoka kwa wanafunzi wa kitanzania unaonesha dhahiri kuwa elimu ya Tanzania ni bora.
Baadhi ya wanafunzi, walimu na wazazi walioshiriki katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC mwaka 2019 wakisikiliza hotuba ya mgeni rasmi ambaye ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha (hayupo pichani).
Mwanafunzi Ruvina D. Warimba kutoka shule ya sekondari Morogoro, ambaye pia ndio mshindi wa tatu wa shindano la uandishi wa insha za SADC Kanda akitunukiwa cheti na Mwakilishi toka SADC, Agnes Kayola. Katikati ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha na kulia ni Kaimu Kamishna wa Elimu, Augusta Lupokela.
Mratibu wa mashindano ya Uandishi wa Insha, Sylvia Chinguwile akiongea katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC mwaka 2019.
"Kuna maneno huko nje kuwa elimu yetu haina kiwango, kama ni kweli inawezekanaje mwanafunzi wetu anaibuka mshindi wa tatu katika mashindano yanayoshirikisha nchi zaidi ya 15," amehoji Ole Nasha.

Awali, akisoma risala katika hafla hiyo, Mratibu wa mashindano hayo, Sylvia Chinguwile amesema mashindano hayo yamekuwa chachu kwa vijana kufanya utafiti, kujifunza na kufahamu vizuri mchakato wa uimarishaji mahusiano kwa nchi wanachama wa SADC na EAC .

Akielezea zaidi kuhusu mashindano hayo, Chinguwile amesema mchakato wake huanza baada ya kikao cha wakuu wa nchi wanachama ambao hukubaliana mada zitakazoshindaniwa. Baada ya hapo kila nchi hutakiwa kutangaza na kubainisha vigezo vya ushiriki na kwamba insha za wanafunzi huwasilishwa wizarani baada ya kuteuliwa insha bora katika ngazi ya shule na kusahihishwa na jopo la wataalamu.

Chinguwile amewataja washindi wa mashindano hayo na shule wanazotoka kuwa ni Vanessa Lema (Longido), Thomas Kalisti (Kibasila), Monica Nyamhanga (Heritage), Dennis Mmuni (St. Maximillian), Hance Mwang'onda (Mbagala), Julieth Mpuya (Kilangalanga), Grant Mkonyi (Tanga Tech), Mandela Abel (Kibaha), Rebecca Thadayo (Loyola), Sharifa Hamadi (Benbella), Cynthia Masuka (Longido) na Ruvina Warimba (Morogoro) ambaye alishika nafasi ya tatu katika shindano la kanda la SADC.
Hafla hiyo pia imehudhuriwa na mwakilishi kutoka EAC, Dkt. James Jowi, mwakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Eliab Chodota na Mwakilishi kutoka SADC, Agnes Kayola ambao wamewapongeza wanafunzi hao kwa ushindi na kuwataka wanafunzi wengine nchini kushiriki mashindano hayo.

Washindi hao kutoka shule mbalimbali za serikali na binafsi wamezawadiwa fedha taslimu za kitanzania na dola za kimarekani pamoja na kutunukiwa vyeti. Fedha hizo zimetolewa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambapo wametoa kiasi cha Sh. 300,000 kwa washindi wote huku SADC na EAC wakitoa kati ya dola 500 hadi 50 kulingana na kiwango cha ushindi.
Kaimu Kamishna wa Elimu, Augusta Lupokela akiongea katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa Insha za SADC na EAC 2019 iliyofanyika jijini Dodoma.
Mwakilishi kutoka EAC, Dkt. James Otieno Jowi akiongea na washiriki katika hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa uandishi wa insha za SADC na EAC, 2019 iliyofanyika jijini Dodoma.

Mwanafunzi Dennis Mmuni akikabidhiwa cheti na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha katika  hafla ya utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la uandishi wa insha za SADC na EAC, 2019 iliyofanyika jijini Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni