Ijumaa, 22 Mei 2020

WAZIRI NDALICHAKO ATANGAZA TAREHE ZA MITIHANI KWA KIDATO CHA SITA NA VYUO VYA UALIMU

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako amezitaka  shule zote zenye wanafunzi wa kidato cha sita kuanza maandalizi ya kupokea wanafunzi hao ili waanze masomo Juni 1 2020 kama ilivyoelekezwa.

Waziri Ndalichako ametoa agizo hilo Jijini Dodoma wakati alipoongea na waandishi wa habari ambapo amesema ni vizuri kwa shule za bweni zikaanza kupokea wanafunzi hao Mei 30, 2020 ili waanze masomo katika muda uliopangwa.
 
Amesema wakati shule za bweni zikipokea wanafunzi Mei 30, 2020 shule za kutwa nazo zianze maandalizi huku akilitaka Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA) kusambaza ratiba za mtihani mapema kwa ajili ya maandalizi.

"Mitihani ya Kidato cha sita na Vyuo vya Ualimu inaanza Juni 29, 2020 na kukamilika Julai 16, 2020 hivyo NECTA sambazeni ratiba za mtihani mapema ili shule  na vyuo vianze maandalizi na kumbukeni mtapaswa kutoa  matokeo ya mtihani huo kabla ya Agosti 30, 2020,"alisema Wziri Ndalichako.

Kwa upande wa Vyuo vikuu na Vyuo vya Kati waziri   Ndalichako ameyataka mabaraza pamoja na Seneti ya Vyuo kupanga ratiba za masomo kwa lengo la kufidia muda wa masomo ambao wanafunzi wamepoteza wakiwa nyumbani na kuwasilisha ratiba hizo Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania(TCU) ili mwaka huu wa masomo ukamilike bila kuathiri ratiba za masomo kwa nwakali 2020/2021

Pia amevitaka vyuo hivyo kuwasilisha nyaraka muhimu zinazohitajika Bodi ya Mikopo ya wanafunzi wa Elimu ya Juu ili Mikopo kwa wanafunzi na ada zao ziweze kutolewa mapema kwa kuwa tayari Serikali imeshatoa jumla ya sh Bilioni 122.8  kwa ajili hiyo.

Itakumbukwa kwamba Mei 21 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli wakati akihutubia wananchi kupitia Vyombo vya habari alitangaza kufungua vyuo vya elimu ya Juu, Kati na Masomo kwa wanafunzi wa kidato cha sita.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni