Jumatatu, 9 Novemba 2015

USHAURI WANGU KWA SERIKALI JUU YA UBORESHAJI WA MIUNDOMBINU YA ELIMU.


Josias Charles.

Baada ya mchakato mzima wa Kampeni kukamilisha na hatimaye Serikali kuundwa na Chama cha Mapinduzi kupitia kwa aliyekua mgombea wake wa Urais Mh. Dkt. John Pombe Magufuli tunapaswa kuungana wote na kutoa mawazo yenye lengo la kujenga uchumi wa Nchi Yetu.

Kumekuwepo na tatizo sugu la ukosefu ama kuwa na miundombinu mibovu mbalimbali ya Elimu Kama Madarasa, Maktaba, Mabweni, Maabara, Madawati nk. Ukosefu wa miundombinu hii umekwamisha ama kudumaza utoaji wa Elimu nchini.

Binafsi napenda kuishauri Serikali ya awamu ya Tano kuwekeza katika kuimarisha Elimu ya ufundi (VETA) na kuweka sera madhubuti itakayowabana wahitimu wa vyuo vya ufundi kujitolea kama sehemu yao ya mafunzo lakini pia ikiwa kama sehemu ya Kujitolea kujenga Taifa.


Mitaala ya Elimu ya ufundi Kama itatolewa kwa kipindi cha miaka miwili basi mwaka mmoja utumike kwa mafunzo darasani na mwaka mmoja kwa mafunzo kwa vitendo yaani( FIELD). Wanachuo wote wa VETA hata kama watasoma bure lakini wakatakiwa kufanya field kwa mwaka mzima watakua wameshiriki kwa kiwango kikubwa katika Ujenzi wa Taifa letu.

Mfano wanafunzi 10,000 wakichukua mafunzo ya ufundi kwa mwaka kwa uwiano tuu wa mafundi uashi 5000 na mafundi seremala 5000 kisha baada ya masomo ya mwaka mmoja wakaenda field kwa Mwaka mmoja kujenga Shule, hospitali, vituo vya afya, kutengeneza samani za ofisi tutapunguza gharama kiasi gani?

Nchi Yetu tuna raslimali nyingi ikiwemo raslimali watu lakini hatujaweza kuiendeleza. Naomba tuwekeze katika  kuendeleza raslimali tulizo nazo kwa manufaa ya Taifa letu.

Baada ya kuhitimu mafunzo ya miaka miwili tunao uwezo wa kuwatengenezea ajira vijana hawa na kuwawezesha mitaji inayotokana na shughuri zao katika jamii kwa kujitolea kwa mwaka mzima.

Hebu fikiria Serikali inaagiza samani za ofisi kiasi gani kwa mwaka? Pesa kiasi gani inatumika? Vipi kama vijana waliohitimu VETA mafunzo ya miaka miwili tena kwa kujitolea kujenga Taifa kwa mwaka mzima wakisajiriwa na  kampuni na kupata soko la uhakika toka Serikali na kuachana na uagizwaji wa samani za kichina tutapunguza tatizo la ajira kwa kiwango gani?

Vipi kama vijana walio soma ufundi uashi na kujitolea kujenga Taifa kwa mwaka mzima  wakapewa mikataba ya kujenga nyumba kama za NHC na Majengo mengine mengi tutapunguza tatizo la ajira kwa kiwango gani?

Tuna amini Serikali ya awamu ya Tano ipo makini na inalenga kila MTU afanye kazi kutimiza kauli mbiu ya "HAPA KAZI TU"

Mawaziri, Wabunge, na viongozi wote wa Serikali onyesheni ubunifu kulifanya Taifa letu lisonge mbele.

Kwa Leo inatosha.

HapaKaziTu

Jumanne, 6 Oktoba 2015

WATAALAM WA ELIMU KUTOKA SWEDEN WAFANYA ZIARA YA KIKAZI NCHINI

 
Wataalam wa Elimu kutoka Sweden ambao ni Wajumbe wa Baraza la Elimu ya Juu nchini humo wameanza ziara ya kikazi nchini  kwa lengo la kujifunza mfumo wa elimu katika ngazi zote, mipango ya maendeleo pamoja na mageuzi mbalimbali ya Elimu.
 
Wataalam hao ni Wakaguzi wawili toka Kitengo cha Elimu ya Juu (Cecilia George na Petra Nord); Wakaguzi wawili kutoka Kitengo cha Elimu ya Sekondari (Eva Neihoff na Isabelle Nilsson); na Mkaguzi mmoja toka katika Kitengo cha Elimu ya Ufundi (Stefan Lofkvist).
 
Ujumbe huo umekutana na kufanya mazungumzo na watumishi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi wakiongozwa na Kamishna wa  Elimu nchini Prof. Eustella Bhalalusesa aliyemwakilisha Katibu Mkuu. Mazungumzo yao yalijikita zaidi katika kubadilishana uzoefu kuhusu mifumo ya elimu inayotumika katika nchi hizo mbili.
 
Aidha, wataalam hao katika ziara yao iliyoanza tarehe 5 hadi 7 Oktoba, 2015  wanatembelea taasisi zilizo chini ya Wizara zikiwemo; Taasisi ya Elimu Tanzania, Baraza la Mitihani, Tume ya Vyuo Vikuu, Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mamlaka ya Elimu ya Ufundi Stadi.  Pia watatembelea shule mbili za sekondari zenye kidato cha tano na cha sita kwa lengo la kuanzisha uhusiano wa kirafiki na shule kama hizo nchini Sweden.









Alhamisi, 1 Oktoba 2015

MAMLAKA YA ELIMU TANZANIA YATOA MKOPO WA SHILINGI BILIONI 3 KWA TAASISI YA ELIMU TANZANIA


 Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) imeingia makubaliano na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) ya Mkopo wa Shilingi Bilioni tatu. Mkopo huu umetolewa na TEA ili kuiwezesha Taasisi ya Elimu Tanzania Kufanya utafiti wa kubaini mahitaji ya maboresho kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali wa elimu, Kuandaa mitaala na  mihtasari ya masomo ya Elimu ya Msingi na Kuandika vitabu vya kiada kwa Darasa la III hadi la VI ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014.

Mkataba huo umetiwa saini tarehe 30 Septemba, 2015 na Joel Laurent Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TEA na Dkt. Leonard Akwilapo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TET na kushuhudiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Prof. Sifuni Mchome ambapo Mkopo  huo ni nafuu unatarajiwa kulipwa katika kipindi cha  miaka 6.
Matokeo tarajiwa kutokana na Mkopo huo ni Pamoja na uwepo wa Mitaala inayoendana na wakati na inayokidhi mahitaji ya sekta na shirikishi, uwepo wa mihutasari ya masomo itakayosambazwa katika kila shule kama ilivyoainishwa katika mitaala na uwepo wa vitabu vya kiada kulingana na mtaala ili kuepusha kuwa na vitabu vinavyotofautiana.


Aidha, ufadhili huu unalenga kuiongezea Taasisi ya Elimu Tanzania kutekeleza majukumu yake kwa njia yenye tija na kuongeza mapato ya Taasisi na utakuwa ni chachu ya kuboresha mfumo wa upatikanji wa vitabu sahihi kulingana na mitaala nchi nzima kupitia TIE.





MKUTANO WA KUTATHMINI SEKTA YA ELIMU NCHINI WAFANYIKA


Mkutano wa kutathmini Sekta ya Elimu nchini kwa mwaka 2015 umefanyika jijini Dar es Salaam katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere kuanzia tarehe 28 hadi 30 Septemba, 2015 ambapo Wadau mbalimbali wa Elimu ikiwa ni pamoja na Serikali, Washirika wa Maendeleo na Taasisi Zisizokuwa za Serikali zinazojihusisha na Elimu walikutana na kujadiliana kuhusu mafanikio, changamoto na mikakati ya kuboresha elimu nchini.

 Mkutano huo ambao ulifanyika sambamba na Maonesho ya Matumizi ya TEHAMA katika Elimu ya Msingi ulifunguliwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Profesa Sifuni Mchome ambae aliwataka washiriki wa mkutano huo kujadili kwa kina namna bora ya kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika Sekta ya Elimu nchini.









Mkutano huo umefungwa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anaeshughulikia Elimu Mhe. Kassimu Majaliwa ambae alisema ushirikiano ulioko kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo unasaidia kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika kuimarisha mahudhurio ya shule, kugharamia Elimu  Msingi  kwa wanafunzi wote, kupatikana kwa walimu wa masomo ya Sayansi na Hisabati katika Elimu Msingi.




Jumatano, 23 Septemba 2015

Waziri Kawambwa afanya ziara AIMS – Tanzania


Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dkt. Shukuru Kawambwa mwishoni mwa wiki alitembelea Taasisi ya  African  Institute for  Mathematical  Sciences - Next Einstein Initiative (AIMS-NEI) kampasi ya Tanzania na kuzungumza na viongozi na wanafunzi wa Shahada ya Uzamili katika masomo ya  Hisabati na Sayansi kwa mwaka 2015/16. Taasisi ya AIMS hapa nchini imeanzisha kampasi yake Bagamoyo, mkoani Pwani ambapo hivi sasa inatumia kwa muda majengo ya Alpha Zulu Villa na baadaye itatumia majengo ya Old Boma na Datoo yaliyoko Bagamoyo mjini baada ya kufanyiwa ukarabati.
Wanafunzi 45 kutoka nchi mbalimbali za Afrika wamedahiliwa kuanza masomo katika taasisi ya AIMS – Tanzania kwa mwaka 2015/16 wakiwemo Watanzania 17 na wengine wanatoka nchi za Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Cameroon, DRC, Msumbiji, Nigeria, Zimbabwe, Afrika Kusini, Sudani na mmoja anatoka Uingereza.
Kuanza kwa mafunzo hayo ni jitihada za Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete kuhakikisha kuwa Taifa linakuwa na wataalam wa kutosha katika Nyanja za Hisabati na Sayansi. Mheshimiwa Rais alikutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa taasisi hiyo alipokuwa ziarani nchini Canada mwishoni mwa mwaka juzi.
 
 






 

 

 

Jumatano, 16 Septemba 2015


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
MAONESHO YA MATUMIZI YA TEHAMA KATIKA ELIMU YA MSINGI
Wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi inaandaa maonesho ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa ajili ya kuongeza Ufanisi katika Ujifunzaji na Ufundishaji katika Elimu ya Msingi nchini.
Maonesho haya yanalenga kutoa fursa kwa wabunifu, wauzaji na wadau wa elimu kuonesha bunifu mbalimbali za teknolojia ya habari na mawasiliano zitakazoweza kutumiwa katika Elimu ya Msingi ili kuongeza ufanisi katika Ujifunzaji na Ufundishaji wa stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) na katika masomo mengine.
Maenesho haya yatafanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere mkoani Dar es Salaam, kuanzia tarehe 28/9/2015 hadi tarehe 02/10/2015
Washiriki wa maonesho haya wanatakiwa kujiandikisha kupitia wavuti: www.lanes-moe.go.tz, kabla ya tarehe 24/9/2015. Aidha, washiriki watakaokidhi vigezo vinavyotakiwa, kazi zao zitatumika katika Ujifunzaji na Ufundishaji katika Elimu ya Msingi Nchini.
Wizara inawahimiza wabunifu wote  wa ndani na nje ya nchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika maonesho haya.
Imetolewa na
Katibu Mkuu
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi
13/09/2015